Tuesday, September 22, 2015

Nimenunua Kitabu cha Golding, "Lord of the Flies"

Zimepita siku nyingi kidogo tangu niandike ujumbe kuhusu vitabu nilivyonunua, au nilivyojipatia kwa namna nyingine. Viko vitabu kadhaa, hasa riwaya, ambavyo sikuvielezea.

Leo, baada ya kufundisha vipindi vyangu viwili, nilipita kwenye duka la vitabu la hapa chuoni. Niliangalia sehemu vinapouzwa vitabu kwa bei nafuu, nje ya duka, nikaona, kati ya vitabu vingi, kitabu cha William Golding, Lord of the Flies. Hapo hapo nilikumbuka miaka ya ujana wangu. Tulisoma kitabu hiki tulipokuwa kidatu tano Mkwawa High School, mjini Iringa. Huku nikikumbuka hayo yote, nilikinunua hima, ingawa nina hakika ninayo nakala nyingine niliyonunua zamani, ila itakuwa vigumu kuigundua ilipo katika utitiri wa vitabu vyangu.

Lord of the Flies ni riwaya niliyoipenda sana na ambayo ninaikumbuka sana. Ilinigusa kwa namna ya pekee kwa jinsi ilivyowachora wahusika, ambao ni watoto wa shule waliojikuta kwenye kisiwa peke yao baada ya ndege waliyokuwa wanasafiria kuanguka kisiwani humo na wao wakawa abiria pekee waliosalimika. Riwaya inaonyesha jinsi watoto hao, waliokulia katika jamii ya maadili na ustaarabu, walivyoanza kubadilika, wakawa wabaya na katili kupindukia.

Miaka ile, nilikuwa najikongoja katika uandishi wa hadithi fupi. Lord of the Flies ilinigusa kwa namna ya pekee, kwa ustadi wake wa kuelezea mazingira, ikachangia katika uandishi wa hadithi yangu, "A Girl in the Bus," ambayo ilichapishwa katika jarida la Busara. Hili lilikuwa ni jarida maarufu Afrika Mashariki, lililokuwa linachapishwa Nairobi.

Kuchapishwa kwa hadithi hii kulinipa furaha isiyoelezeka. Nilikuwa na mazoea ya kwenda katika maktaba ya mkoa Iringa, na daima nilikuwa napendezwa kuona jarida hili lenye hadithi yangu. Hata nilipoingia Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kusoma, mwaka 1973, nilikuwa najisikia raha kuliona jarida hili  katika maktaba.

Lord-Flies of the Flies ni riwaya iliyowagusa watu ulimwenguni. Wanadamu kwa ujumla tunaamini kuwa watoto wana silika ya wema na usafi wa moyo. Wanafalsafa kama Jean-Jacques Rousseau walichangia kujenga imani hiyo. Lakini William Golding, katika riwaya yake hii ameelezea jinsi watoto wanavyobadilika na kuwa wabaya. Ni hadithi iliyowashtua walimwengu kwa namna ilivyoihoji dhana ya kwamba watoto ni kama malaika.

Nikizingatia kuwa Lord of the Flies ni moja kati ya riwaya maarufu kabisa katika lugha ya ki-Ingereza, nitaisoma kwa furaha, nikikumbuka ilivyonigusa enzi za ujana wangu. Miaka ilivyopita, nimesoma hadithi na tamthilia mbali mbali ambazo zimeelezea dhamira hii ya watu waliopotelea kwenye kisiwa mbali na walimwengu. Mifano ni The Odyssey ya Homer, Robinson Crusoe ya Daniel Defoe, na mashairi kadhaa ya Derek Walcott, kama vile "The Castaway." Hata baadhi ya wanafalsafa wa mkondo wa "existentialism" wameongelea uwepo wetu hapa duniani kwa kuufananisha na upweke wa watu waliotupwa na kusahauliwa. Ni dhamira ambayo imekuwa na mashiko ya pekee katika fikra na hisia za wanadamu.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...