Saturday, December 16, 2017

Vitabu Kama Zawadi ya Krismasi

Niliwahi kuandika makala katika blogu hii kuhusu vitabu kama zawadi ya sikukuu. Kwa wenzetu huku ughaibuni, hili ni jambo la kawaida. Watu wanafurahi kununua vitabu na kuwapelekea ndugu na marafiki wakati wa sikukuu. Watu hufurahi kupata zawadi ya vitabu.

Leo nimeviangalia baadhi ya vitabu nilivyonunua mwezi huu nikajiwa na mawazo kwamba vitabu hivi ni kama zawadi ya Krismasi ambayo nimejinunulia mwenyewe. Watu wengi wanajitayarisha kwa sikukuu kwa kujinunulia mavazi na siku ambayo ndio sikukuu wanajizawadia kwa vyakula maalum na vinywaji. Wanywaji wa bia wananunua bia.

Katika kufikiria hivyo, nimejiaminisha kwamba sijakosea katika kujiaminisha kuwa vitabu nilivyonunua katika katika kipindi hiki cha kuelekea Krismasi ni zawadi yangu. Tofauti na bia, vitabu hivi nitavifurahia kwa miaka yote ya maisha yangu, na vitabaki hata baada ya mimi kuondoka duniani.

Pichani hapa kushoto kuna vitabu vinne. Cha kwanza ni Behold the Dreamers, cha Imbolo Mbue. Huyu ni dada kutoka Kamerun. Nilikuwa nimesikia jina lake kijuu juu, lakini sikuzingatia. Nilipoona kitabu chake hicho katika duka la vitabu la hapa chuoni St. Olaf niliamua kukinunua. Nilivyoangalia ndani nimeona kimepata sifa nyingi sana kutoka kwa wahakiki. Bila shaka nitakiweka katika kozi yangu mojawapo.

Kitabu cha pili ni Shot All to Hell: Jesse James, the Northfield Raid, and the Wild West's Greatest Escape kilichotungwa na Mark Gardner. Hiki ni kimoja kati ya vitabu vingi vilivyowahi kuchapishwa juu ya jambazi Jesse James na washirika wake. Nilishafanya utafiti juu ya Jesse James, kuanzia mwaka 1992 hapa Northfield, ambapo jambazi huyu na genge lake walivamia benki na kujaribu kuiba pesa, lakini wenyeji waliwashtukia na kuzimisha uharamia huo na majambazi wakakimbia. Kitabu hiki nilikinunua kwa sababu kinahusu utafiti wangu na pia kwa kuwa kinahusu mji ambamo ninaishi.

Kitabu cha tatu nilichonunua ni The Essentials of Psychoanalysis, ambacho ni mkusanyo wa insha kadhaa maarufu za Sigmund Freud, ambao umetayarishwa na Anna Freud. Aliyetafsiri insha hizo ni James Strachey. Ninavyo vitabu vyenye insha za Freud, lakini niliona ni vizuri kuwa na insha hizi katika kitabu kimoja.

Kitabu cha nne ni Nana cha Emile Zola. Nilifahamu jina la mwandishi Zola tangu zamani sana, labda wakati ninasoma chuo kikuu cha Dar es Salaam. Nilikuja kumfahamu kama mfano wa waandishi waliofuata mkondo wa "critical realism." Nilifahamu jina la kitabu chake kingine, Germinal. Mimi mwenyewe, ninapofundisha fasihi, mara kwa mara nimekuwa nikimtaja Zola. Nitajitahidi nipate wasaa wa kusoma hizi riwaya za Zola, ingawa ninajua itakuwa baada ya Krismasi

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...