Saturday, August 1, 2009

Nilivyoenda Zanzibar na Pemba Kuwaongelea Wamarekani

Tarehe 16 Machi, 2005, nilipata barua pepe kutoka Ubalozi wa Marekani Tanzania. Ujumbe ulikuwa ni ombi kama nitakapokuwa Tanzania nitaweza kutoa mihadhara kwa waTanzania kuhusu utamaduni na jamii ya Wamarekani. Ujumbe ulifafanua kuwa itakuwa ni juu yangu kuamua nini cha kuongelea: mazuri, mabaya, hata mabaya kabisa. Nilikubali ombi hilo. Nilipofika Tanzania, niliwasiliana na Ubalozi, na maandalizi yalifanyika, kuniwezesha kwenda Zanzibar na Pemba, tarehe 15 na 16 Agosti, 2005.

Matangazo yalitayarishwa na kubandikwa sehemu mbali mbali Zanzibar na Pemba. Nilisindikizwa kwenye ziara hii na Bwana David Colvin, ofisa utamaduni katika Ubalozi wa Marekani. Yeye ndiye aliyekuwa ananitambulisha kwa wenyeji wangu, kwani alikuwa amewazoea. Mhadhara wa kwanza ulifanyika katika Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar.


















Walikuja watu wengi. Kwa bahati nzuri baadhi nilikuwa nawafahamu, tangu walipokuwa wanafunzi wangu katika chuo kikuu cha Dar es Salaam. Walikuwepo pia wanafunzi kutoka Ulaya, waliokuwa wanasoma kiSwahili hapo Chuoni. Mhadhara wangu ulitokana na yale niliyoandika katika Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Ilikuwa fursa nzuri ya kuwaleza waTanzania mambo kadhaa yanayoweza kuleta matatizo ya kutoelewana baina ya waTanzania na waMarekani. Baada ya mhadhara, kilifuata kipindi cha masuali. Jambo mojawapo lililoleta msisimko ni jinsi dhana ya tabia njema au heshima ilivyo katika jamii ya kiMarekani, na jamii ya kiTanzania.













Nililala Zanzibar na siku ya pili nikaenda Pemba. Nilipokelewa uwanja wa ndege na bwana mmoja ambaye alinikumbusha kuwa alikuwa mwanafunzi wangu Chuo Kikuu cha Dar es Salaama miaka iliyopita. Tulienda hadi mjini Chake Chake, na hapo nilipokelewa kwa ngoma ya Msewe.
Nilifurahi sana kuiona Pemba. Ilikuwa ni mara yangu ya kwanza. Mhadhara wangu ulifanyika katika jumba la makumbusho, ambalo Ubalozi wa Marekani umegharamia ukarabati wake. Ukarabati huu umewezesha kuhifadhiwa kwa vitu vingi vya thamani katika historia na utamaduni wa Pemba. Ni hazina kubwa kwa vizazi vijavyo.













Mhadhara wangu ulikuwa sawa na ule wa Zanzibar. Watu walijaa ukumbini, na wengi walilazimika kusikiliza wakiwa nje ya ukumbi.
Wakati wa masuali, wengi waliulizia kwa huzuni kuhusu sera za Marekani kwa nchi za kiIslam. Walitaka ninaporudi Marekani nielezee hisia na masikitiko yao kuhusu sera hizo huko Iraq, Afghanistan, Palestina, na kwingineko. Niliwahakikishia kuwa Wamarekani wenyewe hawana kauli moja kuhusu sera hizo. Wananchi wengi wanazipinga. Niliwaelezea kuwa hata wakati niliposoma Marekani, miaka ya Rais Reagan, niliona Wamarekani wengi wa kawaida walivyokuwa wanapinga sera za serikali ya Reagan huko Nicaragua na sehemu zingine.













Hii ni kati ya ziara ambazo sitazisahau. Pamoja na yote niliyoweza kuongea kuhusu waMarekani, nilifurahi kupata bahati ya kuiona Pemba kwa mara ya kwanza maishani. Nawajibika kutoa shukrani kwa Ubalozi wa Marekani Tanzania kwa kunipa fursa hii ya kuiona sehemu ya nchi yangu. Namshukuru sana Bwana David Colvin kwa kunipa picha nyingi, zikiwemo nilizotumia hapa.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...