Saturday, January 9, 2010

Arusha na Kansas City: Miji Rafiki

Kama ilivyo kwa miji mingi hapa Marekani na duniani kwa ujumla, mji wa Kansas una utaratibu wa kujenga urafiki na miji mingine duniani. Arusha ni mji moja ambao tayari una urafiki huo na mji wa Kansas, kama inavyoonekana kwenye tovuti hii.

Nilifahamu habari ya uhusiano huu baina ya mji wa Kansas na Arusha tangu miaka kadhaa iliyopita, kwa kusoma taarifa mtandaoni. Kuna taarifa nyingi, lakini iliyonivutia zaidi ni ile ya harakati za Pete O'Neal, mwenyeji wa mji wa Kansas, ambaye aliikimbia nchi yake akahamia Arusha. Shughuli zake hapo Arusha ni pamoja na kuwa kiungo baina ya wa-Marekani na wa-Tanzania, kama inavyoelezwa hapa. Habari za mwanaharakati huyu zinaelezwa vizuri katika filamu iitwayo A Panther in Africa.

Katika kufuatilia habari hizi, nilianza kupata wazo la kuwasiliana na watu wa mji wa Kansas wanaoshughulika na mpango huu wa urafiki baina yao na Arusha. Nilishatembelea mji wa Kansas, kwa utafiti kuhusu mwandishi Ernest Hemingway, lakini si kuwa kufuatilia uhusiano baina ya mji huu na Arusha.

Mwaka huu, nilialikwa Kansas. Fursa hii ilitokana na Dr. Mbaari Kinya, mwanasayansi Mkenya, ambaye tulionana kwenye mkutano katika Chuo cha Principia, Illinois, ambapo nilikuwa mtoa mada mwalikwa. Dr. Kinya anaendesha taasisi inayoshughulikia nishati, mazingira, tekinolojia na maendeleo ya wanawake. Taarifa zake hizi hapa. Nilipoelezwa kuwa Dr. Kinya anaishi mjini Kansas, nilimweleza kwamba nafuatilia masuala ya uhusiano baina ya mji wa Kansas na Arusha, naye alisema anafahamiana na mratibu wa mpango huu. Aliporejea Kansas, alimpa taarifa zangu Eslun Tucker, na huo ukawa mwanzo wa mawasiliano baina ya Eslun nami. Kwa bahati nzuri, Eslun ni rafiki ya baadhi ya wa-Kenya waishio Kansas. Nao waliniulizia iwapo ningeweza kuhudhuria kumbukumbu ya Jamhuri ya Kenya, tarehe 12 Desemba. Elsun Tucker ni mama mmoja mwenye mawazo mapana kuhusu ulimwengu. Tofauti na wengi wetu ambao ni wa-Afrika au wenye asili ya ki-Afrika na tumejikita upande wetu tu, yeye ana uzoefu wa watu weusi wa kuanzia Marekani, hadi Caribbean, Afrika Mashariki na Afrika Magharibi.
Nilienda Kansas terehe 12 Desemba, kukutana na wahusika wa mpango huu wa urafiki baina ya Kansas na Arusha na pia kushiriki sherehe za kuazimisha kumbukumbu ya Jamhuri ya Kenya.
Katika kikao chetu alihudhuria pia Harvey Marken. Huyu ni mwalimu na mshiriki katika mpango wa ushirikiano baina ya Kansas na Arusha. Harvey Marken alitembelea Tanzania mara moja, ziara ambayo ilimgusa akaamua kujishughulisha na maendeleo ya shule ya Shangarao.

Alikuwepo pia Deo Rutabana, mwenyekiti wa jumuia ya wa-Tanzania wa mjini Kansas. Yeye ni mdau wa shughuli za maendeleo Tanzania. Nilivutiwa na ajenda za timu hii ya Kansas na ari yao ya kujenga na kuboresha mahusiano baina ya watu wa Marekani na Tanzania na Afrika kwa ujumla
Kati ya shughuli wanazofanya ni kuwawezesha watu kutoka miji hiyo miwili kutembeleana. Safari hizi zinahusisha watu wazima, vijana na watoto wa shule pia. Lengo moja kubwa ni kukuza maelewano baina ya watu wa Tanzania na Marekani.
Watu walioanzisha wazo hili la kujenga uhusiano baina ya mji wa Kansas na Arusha huenda walikuwa na ajenda fulani maalum, kwa mujibu wa taratibu za mipango ya aina hii. Lakini ukweli ni kuwa mbegu iliyooteshwa imekua na kueneza matunda sehemu nyingi. Imezaa mipango mingi yenye wahusika wa sehemu mbali mbali, Marekani na Tanzania. Mtandao huu utaendelea kupanuka.
Lengo langu kubwa ni kutafakari namna mahusiano ya aina yoyote baina ya watu wa tamaduni mbali mbali yanavyoathiriwa na tofauti za tamaduni.
Ni wazi kuwa, katika suala kama hili la uhusiano baina ya Arusha na Kansas, masuala ya tofauti baina ya utamaduni wa m-Tanzania na ule wa m-Marekani yatajitokeza. Ni lazima yashughulikiwe, sambamba na masuala mengine yote.
Katika mazungumzo ya aina hii tuliyofanya, mambo mengi yalijitokeza, mawazo na ushauri. Ni namna nzuri ya kuboresha mipango ilikwisha anza, na pia kuandaa mipango mingine.


Kamati ya Kansas inafahamu umuhimu wa kushughulikia suala la utamaduni. Kwa mfano, imeandaa kijitabu cha kufundishia ki-Swahili. Kuna wazo pia la kuandaa kijitabu kuhusu mapishi na vyakula. Zote hizi ni juhudi za kuuleta utamaduni wa ki-Tanzania katika mawazo na maisha ya watu wa Marekani. Ni muhimu vile vile wa-Tanzania nao tufanye juhudi kuwaelewa wa-Marekani, ili tunapokuwa pamoja tusiwe tunakutana kama wageni daima. Tunayo fursa ya kupunguza ugeni na kujenga maelewano ya karibu zaidi.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...