Tuesday, September 9, 2014

Viongozi wa Afrifest Foundation

Kama wewe ni mtembeleaji wa blogu yangu hii ya hapakwetu au ile ya ki-Ingereza, utakuwa umesoma taarifa zangu kuhusu Afrifest, taasisi iliyoanzishwa hapa Minnesota, Marekani, na makao yake ni hapa hapa.

Hapa kushoto tunaonekana baadhi ya viongozi tunaoendesha Afrifest. Kulia kabisa ni Nathan White, kutoka Liberia, ambaye nikatibu mtendaji wa Afrifest, na ndiye ambaye alianzisha wazo zima la Afrifest, kama anavyoelezea hapa.

Katikati naonekana mimi, m-Tanzania, ambaye ni mwenyekiti wa bodi ya Afrifest. Nimekuwa mshiriki wa Nathan White tangu mwanzo, pamoja tukapanga na kuendesha tamasha la kwanza la Afrifest, mwaka 2007. Tulipopiga picha hii, afya yangu ilikuwa dhaifu kuliko sasa. Sikumbuki kama maishani mwangu nimewahi kupigwa picha inayonionyesha nikicheka namna hii.

Kusohto kabisa ni Wycliff Chakua, kutoka Kenya. Yeye alijiunga na Afrifest miaka michache iliyopita. Ndiye mweka hazina wa Afrifest.

Tulipiga picha hii tarehe 2 Agosti, wakati wa tamasha la Afrifest lililofanyika Brooklyn Park, Minnesota. Niliandika habari za tamasha hilo mara kadhaa, kwa mfano hapa, hapa, na hapa. Tunao wanabodi wengine ambao hawakuweza kuhudhuria tamasha hili, lakini tuko pamoja katika kushughulikia malengo ya Afrifest ya kuwaunganisha, kuwaelimisha, na kuwaburudisha watu wenye asili ya Afrika popote walipo ulimwenguni, na watu wengine wote wenye mtazamo huo au wanaotaka kufahamu zaidi mambo tunayoyashughulikia.

Kazi zetu katika Afrifest ni za kujitolea. Lakini tunafurahi kuzifanya, na furaha inakuwa kubwa tunapoona jinsi jamii inavyofaidika na shughuli zetu. Utumishi huu kwa jamii unatupa fursa ya kufahamiana vizuri sisi wenyewe na pia kufahamiana na wadau wanaohudhuria matamasha na matukio mengine ya Afrifest. Karibuni kwenye matamasha na matukio haya. Karibuni pia mtutembelee katika Facebook.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...