Saturday, October 17, 2015

Kitabu Kinapouzwa Amazon

Nina jadi ya kuandika kuhusu vitabu katika blogu hii. Ninaandika kuhusu vitabu ninayonunua na ninavyosoma, uandishi, uchapishaji, na uuzaji wa vitabu. Ninaandika ili kujiwekea kumbukumbu na pia kwa ajili ya wengine wanaotaka kujua mambo hayo, iwe ni wasomaji na wadau wa vitabu, waandishi, au wanaotarajia kuwa waandishi. Leo napenda kuongelea kidogo juu ya vitabu vinavyouzwa katika tovuti ya Amazon.

Nimewahi kuandika kuhusu mada hii. Lakini nimeona si vibaya kuirudia, ili kuelezea kama yale niliyoyasema mwanzo yamebaki vile vile au kama kuna lolote jipya. Ninaongea kutokana hali halisi ya vitabu vyangu Amazon.

Kwanza kabisa, mambo ya msingi niliyosema mwanzo yamebaki vile vile. Vitabu vyangu viliingia Amazon bila mimi kuvipeleka kule. Vinauzwa kule kuliko sehemu nilipovichapisha au kwenye duka langu la mtandaoni. Ninajionea mwenyewe kuwa Amazon ni mtawala wa himaya ya uuzaji wa  vitabu mtandaoni.

Kila niendako, kwenye matamasha ya vitabu au katika kukutana na watu popote, likijitokeza suala la upatikanaji wa vitabu vyangu, watu wanaovitaka wanaulizia kama vinapatikana Amazon. Imefikia mahali sasa sioni hata umuhimu wa kuwatajia sehemu nyingine. Amazon imejengeka vichwani mwa watu sawa na nyumba ya ibada ilivyojengeka kichwani mwa muumini wa dini: mu-Islamu na msikiti, au m-Kristu na kanisa.

Mimi mwenyewe sina tofauti na hao watu. Ninapotaka kununua kitabu mtandaoni, ninakwenda moja kwa moja Amazon. Ninavutiwa na urahisi wa kuviagiza na kuletewa, na uhuru wa kuchagua bei unayotaka kulipia, kwani kitabu hicho hicho kinauzwa kwa bei mbali mbali.

Hiyo ndio hali halisi ya ununuaji wangu wa vitabu mtandaoni. Tofauti ni pale ninapotaka kununua vitabu vyangu. Hapo siendi Amazon, bali kwenye duka langu. Ninavipata kwa bei pungufu. Punguzo la bei linaongezeka kufuatana na uwingi wa vitabu ninavyonunua. Ninapenda kununua vingi, kwa sababu ninapenda pia kutoa nakala za bure kwa taasisi, vikundi, au watu binafsi wanaojishughulisha kama mimi mwenyewe katika kujenga mahusiano mema baina ya jamii mbali mbali.

Kama nilivyosema katika ujumbe wangu wa mwanzo na kurudia hapa juu, Amazon inauza vitabu kwa bei pungufu. Kwa upande mmoja, hii ni hasara kwa mwandishi. Ni hali halisi ya mfumo wa biashara, na hakuna sheria inayokiukwa. Kwa upande mwingine, hii ni baraka kwa mteja. Kama methali isemavyo, Kuvuja kwa pakacha, nafuu ya mchukuzi.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...