Sunday, November 15, 2015

Jana Nilikwenda Kusimulia Hadithi

Jana jioni nilikwenda Maple Grove, Minnesota, kwenye sherehe ya watu wa Liberia ya kumbukumbu ya kuzaliwa mtoto. Nilikuwa nimealikwa kusimulia hadithi, kama nilivyoandika katika blogu hii.

Nilifika saa moja jioni, kama nilivyotegemewa, nikakuta sherehe zimeshamiri. Watoto walikuwa katika michezo, na watu wazima walikuwa katika mazungumzo.  Baada ya kukaribishwa kuongea, nilijitambulisha kifupi, nikashukuru kwa mwaliko. Nilifurahi kumwona binti mdogo ambaye alikuwa amehudhuria niliposimulia hadithi katika tamsha la Afrifest. Yeye na mama yake, ambaye alikuwa mwenyeji wangu hiyo jana, ndio watu pekee nilowafahamu.

Nilijiandaa kusimulia hadithi kutoka Afrika Magharibi. Nilisimulia hadithi moja kuhusu urafiki baina ya Chura na Buibui ("Frog and Spider") na ya pili juu ya mhusika aitwaye Pesa ("Money").

Baada ya kusimulia hadithi ya Chura na Buibui, nilitumia muda kuwauliza watoto mawazo yao kuhusu hadithi hiyo. Hawakusita kujieleza. Sikushangaa, kwani katika uzoefu wangu wa kuwasimulia watoto hadithi hapa Marekani, nimeona kuwa wanapenda kuelezea maoni yao kuhusu tabia za wahusika, maudhui, na kadhalika.

Vile vile, kabla ya kusimulia hadithi ya pili, nilisema kuwa iwapo watoto wanapenda kuendelea na michezo yao wafanye hivyo, na wale ambao wanapenda kusikiliza hadithi nyingine, wabaki. Nilisema hivyo kwa kuona kuwa watoto wengine walikuwa wadogo mno, ambao hupenda kubadili shughuli mara kwa mara. Sio rahisi kuwakalisha wakakusikiliza kwa zaidi ya dakika 20.

Nilisimulia hadithi ya pili, ambayo ni ndefu zaidi kidogo kuliko ile ya kwanza. Ilifaa kabisa kwa watoto wenye umri mkubwa zaidi na kwa watu wazima.

Baada ya hapo, nilisema kuwa ninashughulika na kurekodi na kutafsiri hadithi za jadi, nikawaonyesha kitabu cha Matengo Folktales. Mtu mmoja aliuliza iwapo kinauzwa, nami nikamkubalia. Kwa bahati nzuri nilikuwa na nakala za ziada, na watu walizinunua. Sina shaka kwamba watazifurahia hadithi hizo pamoja na uchambuzi wangu.

Safari ya jana nitaikumbuka miaka ijayo. Unaweza kusoma taarifa nyingine niliyoandika katika blogu ya ki-Ingereza.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...