Friday, June 22, 2018

Nimehudhuria Mhadhara Kuhusu Frantz Fanon

Jioni hii nilikuwa St. Paul kuhudhuria mhadhara juu ya Frantz Fanon uliotolewa na Dr. Moustapha Diop. Mhadhara uliandaliwa na Nu Skool, jumuia ya wa-Marekani Weusi ambayo nimewahi kuiongelea katika blogu hii.

Niliona ni lazima nikahudhurie mhadhara huu, ambao mada yake ilikuwa "Becoming Fanon: A Portrait of the Decolonized" kwa kuzingatia umuhimu wa fikra za Fanon katika harakati za ukombozi sehemu mbali mbali za dunia, hasa ukombozi wa fikra.

Nilikutana  na fikra za Fanon kwa mara ya kwanza nilipokuwa mwanafunzi chuo kikuu cha Dar es Salaam, katika idara ya Literature, miaka ya 1973-76. Aliyetufundisha ni mwalimu Grant Kamenju, na vitabu vya Fanon alivyotumia ni The Wretched of the Earth na Black Skin White Masks. Katika kufundisha fasihi ya Afrika, ninaona umuhimu wa kurejea katika fikra za Fanon mara kwa mara. Sielewi utakosaje kurejea kwenye fikra za Fanon.

Katika mhadhara wake, Dr. Diop alielezea kifupi maisha ya Fanon, akajikita zaidi katika kufafanua jinsi baina ya mwaka 1956 hadi 1961 Fanon alivyobadilika na kuwa Fanon tunayemjua kama mwanamapinduzi. Fanon alikuja kuwa mwanaharakati hadi akafukuzwa nchini Algeria. Alikwenda Tunisia, ndipo alipoendesha harakati, ikiwemo kuwapiga msasa wapiganaji wazalendo wa Algeria kabla hawajaingia nchini mwao kupambana na jeshi la wakoloni.

Jambo jingine ambalo nimejifunza katika mhadhara huu ni kuwa The Wretched of the Earth hakukiandika, kutokana na hali ya afya yake, bali alimwelezea mke wake kwa mdomo, naye akaandika. Ilichukua miezi kadhaa. Dr. Diop alitoa muhtasari wa mambo muhimu aliyotufundisha Fanon na akawataja watu walioendeleza fikra  za Fanon Afrika na Marekani, wakiwemo Kwame Nkrumah na Steve Biko.

1 comment:

Unknown said...

Fanon sijapata kumsoma ila nitajaribu Kumsona ili kupata alichokiandika.

Kubwa kwangu ni kuhusu mkewe alivyomsaidia kuyaandika mawazo ya huyo Frantz.

Ni hilo tu kwa sasa.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...