Sunday, June 24, 2018

Maongezi ya Kina Leo na Msomaji Wangu

Leo nimekuwa na maongezi ya kina na msomaji wangu, mchungaji ambaye nilishamtaja katika blogu hii. Tulikutana mjini Hastings, Minnesota, tukaongeaa kwa saa mbili na robo. Tulikuwa tumeahidiana kwamba nikasaini nakala ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho mchungaji alikuwa anampelekea mtu fulani wa karibu.

Tuliongea sana kuhusu shughuli zetu za kuelimisha na kuhamasisha jamii ya watu weusi juu ya masuala ya kujitambua. Mchungaji ameendelea kunifahamisha kuwa kitabu changu kinamsaidia kujitambua kama mtu mwenye asili ya Afrika, ingawa ana pia asili ya ki-Cherokee na ki-Faransa. Anataka kitabu hiki kitumike kuwaelimisha vijana wa-Marekani Weusi, waweze kujitambua na kujivunia walivyo na silika za u-Afrika, ili wasiwe wanabezwa na wazungu.

Nami naelewa vizuri tatizo lilivyo kwa hao vijana. Wanashinikizwa kubadili mwenendo, lugha, na mambo yao mengine, ili wafuate ya wazungu. Mashuleni wanashinikizwa, kudhibitiwa, na kuadhibiwa kwa mienendo yao ambayo mamlaka zinaitafsiri kama utovu wa nidhamu.

Jukumu lililopo, ili pawe na suluhu, ni kwa walimu na viongozi wa shule kufanya juhudi ya kujielimisha kuhusu utamaduni wa wa-Marekani Weusi ambao misingi yake kwa kiasi fulani, au kwa kiasi kikubwa, ni u-Afrika. Wa-Afrika walivyoletwa utumwani huku Marekani, walikuja na tamaduni zao, ambazo zimerithishwa tangu kizazi hadi kizazi, ingawaje zimekuwa zikiathirika na mabadiliko na mazingira kutoka kizazi hadi kizazi.

Hata hivyo, baadhi ya misingi na vipengele vya u-Afrika vimeendelea kuwepo. Kwa mfano, wa-Afrika tuna namna yetu ya kuongea, kama nilivyoelezea katika kitabu changu, hasa kurasa 32-39 na 44-45. Na nimeelezea kitabuni kwamba ninapokutana na wa-Marekani Weusi, ninatambua vipengele hivi vya u-Afrika katika tabia na mienendo yao.

Ninashukuru kufahamiana na mchungaji huyu ambaye ana tafakari za kina kuhusu masuala na ana ukarimu moyoni mwake wa kunielezea anavyojisikia na anavyowazia kuhusu ujumbe wowote uliomo katika kitabu changu. 

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...