Sunday, October 28, 2012

Taarifa kwa Umma Kuhusu Hatma ya MwanaHalisi

Leo 28 Oktoba 2012

Mtandao wa Watetezi wa Haki za Bidamu (THRD-Coalition), wadau wanaounda mtandao huu na mwanachama mwanzilishi wa Mtandao likiwa ni shirika lenye majukumu ya ya kutetea uhuru wa habari kusini mwa Afrika (MISA-Tan) tunaendelea kwa pamoja kuonyesha kusikitishwa kwetu kwa kufungiwa kwa gazeti la Mwanahalisi.

Kwa mara kadhaa sasa tunawakutanisha tena lengo likiwa ni kuendelea kuishawishi serikali ilifungulie gazeti la Mwanahalisi. Kwa vile hoja yetu ya kutaka kuliona gazeti la Mwanahalisi likiwa mitaani haijatimia basi na sisi kwa upande wetu kazi yetu bado haijatimia.

Tunatambua umuhimu wa kuheshimu sheria za nchi, lakini kwa upande mwingine tunaona kwamba ipo haja ya sisi watetezi wa haki za binadamu kupitia kwenye vyombo vya habari na pia kwenye mashirika mengine yanayounda mtandao huu kuishawishi serikali kuachana na sheria gandamizi ambazo ni za kidikteta kama sheria hii ya magazeti ya mwaka 1976 ambayo hukiuka misingi ya haki za binadamu na utawala bora. Pia kwamba maendeleo ya kiteknolojia na kisiasa hapa nchini yanaiweka rehani sheria hiyo gandamizi.

Tumebaini kuwa kufungiwa kwa gazeti la Mwanahalisi siyo tu kwamba kunawaathiri kwa kiwango kikubwa wasomaji wake ndani na nje ya nchi bali pia kunaathiri uhuru wa kutafuta, kupata na kueneza habari, kunawaathiri waajiriwa wa gazeti hilo na familia zao na pia kunaiweka katika hati hati hata kampuni nzima ya Halihalisi ambayo ndiyo mchapishaji wa gazeti hilo.

Tunaendelea kusisitiza kuwa sababu walizotumia viongozi wa wizara ya habari kulifungia gazeti la mwanahalisi sio za kweli kwani kilichoandikwa na Mwanahalisi ni ukweli mtupu ambao hivi karibuni umethibitishwa na tamko la Dr Steven Ulimboka.

Pia, hivi karibuni Dkt Stephen Ulimboka, kupitia kwa wakili wake Mheshimiwa Nyaronyo Kicheere aliweka wazi kwamba Afisa wa Usalama wa Taifa Ramadhan Ighondu alihusika katika kutekwa kwake kwa kuwa mazingira yote kabla na baada ya tukio yanaonyesha wazi kuwa Ramadhani Ighondu ni mdau katika tukio hili.

Kinachoshangaza zaidi ni kwamba baadala ya serikali kutoa tamko kwamba sasa imepata uhakika kwamba afisa wake alikiuka kanuni za ajira yake na ingeaza rasmi kuwasaka washirika wa afisa hiyu jambo hilo halijatokea mpaka sasa huku gazeti hili lililosidia kubainisha ushahidi likifungiwa. Zaidi, tulitegemea serikali ingemkana afisa huyo kwamba siyo mwajiriwa wake katika idara hiyo, kama hivyo ndivyo ilivyo, au vinginevyo tungeitarajia serikali itangaze kwamba inachukua hatua za kisheria dhidi ya afisa huyo ambaye ametajwa kuhusika katika makosa ya jinai kinyume cha utaratibu wa mwajiri wake. Pia tungetemea Jeshi la polisi lingetumia fursa hii kumkamata mshukiwa huyu wa Usalama wa Taifa na kulisadia Jeshi la Polisi kuwapata wale waliotekeleza udhalimu huu dhidi ya Dr Steven Ulimboka. Kwa namna yoyote vitendo vya aina hiyo vinaiabisha serikali na haviwezi kuwa sehemu ya utawala bora ambao serikali yetu imekuwa ikitangaza kwamba inauzingatia.

Mpaka sasa kumekuwapo na matamko mbali mbali kutoka kwa wadau, viongozi wa kiroho, mabalozi na hata Baraza la Habari Tanzania (MCT) likiwa peke yake na hata kwa kushirikiana na wadau wengine wakilaani kufungiwa kwa gazeti hili lakini serikali imeendelea kuwa kaidi katika hili.

Tunachosisitiza
1. Kwa Serikali
Tunaendelea kuwasihi viongozi wa nchi waone sasa umuhimu wa kukutana na viongozi wa Hali Halisi na kujadili namna ya kulifungulia gazeti hili kwani tayari Dr Steven Ulimboka ameshaweka wazi kilichoandikwa na Mwanahalisi ni cha kweli kabisa. Serikali itambue kuwa suala hili sio dogo katika anga za kidemokrasia na haki za binadamu kwani ubabe wa baadhi ya viongozi serikalini leo unaweza iweka nchi pabaya siku za usoni.

2. Vyombo vya Habari
Vyombo vya habari pamoja na taasisi mbalimbali katika tasnia ya habari tuweke tofauti zetu pembeni na kuungana kwa pamoja katika hili na kuhakisha kuwa ukandamizaji wa uhuru wa habari kama huu wa wazi wazi haupati nafasi katika enzi hizi za uwazi na ukweli. Vyombo na taasisi mbalimbali za habari bado mna nafasi na uwezo mkubwa katika kuhakisha gazeti la Mwanahalisi halipotei katika tasnia ya habari hapa nchini.

3. Jumuiya ya Kimataifa
Kwa kuwa mmekuwa wadau wakubwa wa maendeleo na utekelezaji wa haki za binadamu hapa nchini, tukiwa tunaendelea kuuthamini mchango wenu, tunawasihi muendelee kuishawishi serikali kwa njia za kidiplomasia kuhusu suala la kuheshimu kazi za watetezi haki za binadamu na uhuru wa habari. Nafasi zenu za kidiplomasia na uhusiano mkubwa mlionao na nchi ya Tanzania inaweza pia kutumika kushawishi viongozi wa Tanzania walifungulie gazeti la Mwanahalisi.

Kutokana na hali ilivyo ya uvunjifu wa haki za watetezi wa haki za binadamu ikiwamo haki ya kutoa habari, MISA-Tan, mwanachama wa THRD-Coalition anaehusika na uhuru wa habari inaandaa mkutano wa siku moja utakaowakutanisha wadau mbalimbali katika tasnia ya habari ili kujadili hatma ya gazeti la Mwanahalisi na uhuru wa habari nchini.

Mwisho Tunawasihi wanaharakati, watanzania wote wasichoke wala wasirudi nyuma katika azma hii ya kutetea haki, uhuru na ulinzi kwa haki na watetezi wake.

CHANZO: KATUNEWS BLOG

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...