Tuesday, January 5, 2016

Yule Binti Bukola Ametua Ikulu ya Marekani Leo

Siku kadhaa zilizopita, niliandika kuhusu binti Bukola Oriola katika blogu hii. Huyu ni binti kutoka Nigeria ambaye alipatikana na mkasa wa kutumikishwa na kunyanyaswa huku Marekani kwa miaka miwili na mtu ambaye alikuwa ni mume wake, ambaye naye alikuwa m-Nigeria.

Hatimaye, kwa bahati nzuri, aliokolewa, na katika ujumbe wangu nilitoa taarifa ya kuteuliwa kwake kama mjumbe katika tume ya serikali ya Marekani ya kutoa ushauri kuhusu majanga haya ya watu kusafirishwa kwa ghilba, kutumikishwa na kunyanyaswa.

Leo, Bukola na wanatume wenzake wamekutana kwa mara ya kwanza katika Ikulu ya Marekani, kama inavyoonekana pichani, wakiwa na Mheshimiwa John Kerry, "Secretary of State," wa tano kutoka kulia. Bukola anaonekana amevaa kilemba chekundu. Nimeona nilete taarifa hii hapa kuonyesha hatua hii ya safari ya Bukola. Vile vile, nataka kusema kwamba tatizo tunaloongelea hapa ni la dunia nzima. Tusijiziuke, hata wa-Tanzania wanakumbana nalo. Ni tatizo lisilojali jinsia, umri, dini, au rangi ya mtu.

Wako ambao wanarubuniwa kwenda nchi za nje kwa ahadi au mategemeo ya mafanikio lakini wanaishia kuwa mateka na kunyanyasika kama watumwa. Sio lazima kwenda nje ya nchi. Wengine hurubuniwa kutoka vijijini au sehemu nyingine nchini na kupelekwa sehemu tofauti humo humo nchini, hasa mijini, ambako wanatumikishwa na kunyanyaswa. Yote hayo ni matatizo yanayotambuliwa kama "human trafficking" kwa ki-Ingereza.

Napenda kumalizia kwa kusema kwamba, kwa kufuatana na ukaribu wangu na huyu binti Bukola, na kwa kufahamu alivyo na uchungu na tatizo hili, na ari ya kuwasaidia wanaoteseka nalo, na ufahamu wake wa fursa zilizopo za kuwasaidia waathirika, napenda kusema, hasa kwa wa-Tanzania walioko hapa Marekani, lakini kwa wengine pia, kuwa yeyote mwenye kuhitaji msaada, nitaweza kumwunganisha na Bukola hima, ili tatizo lake lianze kushughulikiwa. Mambo hayo ni nyeti, na usiri unazingatiwa vilivyo.

Hapa kushoto anaonekana Bukola katika "selfie" na Bwana John Kerry.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...