Monday, January 16, 2017

Erica Huggins Ahutubia Chuoni St. Olaf

Leo mwanaharakati Erica Huggins amehutubia chuoni St. Olaf. Alialikwa kuhutubia kama sehemu ya maadhimisho ya siku ya Martin Luther King Jr. Erica Huggins alikuwa mwanaharakati maarufu katika Black Panther Party, na ameendelea kuwa mwelimishaji wa jamii, kama inavyoelezwa katika tovuti yake.

Ameelezea historia yake katika Black Panther Party, jinsi mume wake alivyouawa na idara ya upelelezi ya FBI, na jinsi yeye mwenyewe alivyofungwa kwa miaka miwili. Humo kifungoni alitumia muda wake kujichunguza nafsi na akili yake na masuala ya maisha na ulimwengu kwa umakini na utulivu mkubwa. Anaendelea na jadi hiyo, ambayo huitwa "meditation," kila siku.

Amesema kuwa mifumo yote ya kihasama na ukandamizaji, fikra zote za kihasama na kikandamizaji ni mambo yaliyoundwa na wanadamu. Kwa hivyo, wanadamu wana uwezo wa kuleta mabadiliko kwa kuunda mifumo na fikra zenye kujenga maelewano, upendo, na maendeleo ya binadamu. Alisema kuwa tunapaswa kuviheshimu viumbe vyote, sio binadamu tu. Hapo nilimkumbuka Shaaban Robert, ambaye naye alihimiza moyo wa kuvijali viumbe vyote.

Nimeguswa sana na hotuba yake, nikalazimika kutafakari hali ya Tanzania na ulimwengu, jinsi tunavyotumia nguvu nyingi katika kujenga uhasama, kushambuliana, na kubezana. Erica Huggins amebainisha kuwa tunaweza kuleta mapinduzi katika nafsi zetu, katika jamii zetu, na ulimwenguni.  

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...