Tuesday, May 19, 2009

Podikasti ya Kwanza Jamii

Waweza kujipatia picha ya hali ya maisha ya sehemu fulani za vijijini Tanzania katika podikasti ya Kwanza Jamii, kama ilivyorekodiwa na ndugu Maggid Mjengwa. Isikilize hapa




Monday, May 18, 2009

Watoto na Matatizo ya Mtindio wa Ubongo

Makala hii ya Dada Yasinta aliiandika katika blogu yake ya Ruhuwiko nami niliipenda na naiweka hapa kwa ruhusa yake.
*****************************************************************************
Friday, May 15, 2009
WATOTO NA MATATIZO YA MTINDIO WA UBONGO
Ngoja tuendelee na mada hii lakini samahanini imekuwa kinyume.

Wapo watoto wengi wanaozaliwa wakiwa na matatizo mbali mbali, lakini mojawapo nitatizo la mtindio ya ubongo ambalo leo nimeona nilizungumzia kwa undani zaidi.
Matatizo ya mtindio wa ubongo yanatokana au kusababishwa na kizalia (Genetic), dawa alizotumia mama wakati wa ujauzito, matumizi ya madawa ya kulevya, pombe, hali ya hewa, au hata ajali. Mojawapo ya sababu hizo nilizozitaja zinaweza kusababisha kuzaliwa kwa mtoto mwenye mtindio wa ubongo au mtu kupata mtindio wa ubongo.

Nikianza na tatizo la pombe, ni kwamba pombe ina athari kubwa na mbaya kwa akina mama wajawazito. Lipo tatizo linalofahamika kitaalamu kama Fetal Alcoholic Syndrome (FAS) ambalo huwapata watoto ambao wazazi wao walikuwa wanatumia kiwango kikubwa cha pombe wakati wa ujauzito.

Watoto wanozaliwa na tatizo hili wanakuwa na nyuso ambazo sio za kawaida (FacialDeformities), kwa mfano watoto hawa wanweza kuwa na pua bapa na macho yaliyoingia ndani au kuwa na mtindio wa ubongo (Mental Retardations), matatizo ya kusikia na kutokuwa na uwezo wa kusoma.

Kwa hiyo unywaji wa pombe hata kwa kiwango kidogo katika kipindi cha mwezi mmoja hadi mitatu ya mwanzo kwa mama mjamzito huchangia kwa kiasi kikubwa kuzaliwa kwa watoto wenye matatizo haya.

Watot wote wenye matatizo haya ya mtindio wa ubongo wanaweza pia kujifunza kusoma iwapo watapewa msaada maalum na kuandaliwa mazingira mazuri yatakayowashawishi kujifunza kusoma. Malezi kwa watoto wenye matatizo haya, yanatakiwa yawe tofauti na yale ya watoto wa kawaida.

Watoto hawa wanahitaji kuoneshwa upendo, kusikilizwa na mengineyo ya aina hiyo. Hata hivyo swali la msingi tunalopaswa kujiuliza ni kwamba, tutawatambuaje watoto wenye tatizo hili la mtindio wa ubongo wakingali wadogo?

Ukweli ni kwamba ni vigumu sana kwa wazazi kuwatambua watoto wao wenye tatizo hili, kabla watoto hao hawajatimiza umri wa miaka mitatu au minne. Kwa kawaida inashauriwa kwamba mtoto yeyote ambaye anfanya mambo yake pole pole ukilinganisha na watoto wengine wa umri wake, inapaswa kupelekwa haraka hospitalini kwa daktari bingwa wa watoto ili afanyiwe uchunguzi wa kina.

Hata hivyo dalili zifuatazo zinaashiria kuwa mtoto ana tatizo hili Kwanza haoneshi dalili yoyote ya kulia au anaweza kulia kidogo sana. Pili huchelewa sana kutembea na hata kuongea. Tatu haoneshi kuvutiwa nna mazingira yanayomzunguka, kwa maana kwamba hata kama kuna vitu vya kuchezea hawezi kujishughulisha navyo. Nne ni vigumu sana kufundishika na hata kujifunza kusoma huwa ni kazi ngumu ukilinganisha na watoto wa rika lake.

Tano hawezi kula mwenyewe, kuvaa mwenyewe au kujifunza kutumia choo. Hata hivyo zipo dalili nyingi zinazoweza kujitokeza na mara nyingi zinatambuliwa na madaktari maalum wa watoto.

Jinsi wazazi wanavyoweza kuwasaidia watoto wenye tatizo hili:

Watoto wenye mtindio wa ubongo wanafundishika, iwapo tu watafundishwa kwa makini, utulivu na uvumilivu mkubwa, yaani mtu anayemfundisha mtoto wa aina hii hatakiwi kamwe kuwa na hasira, na pia inashauriwa sana kuwapongeza wanapofanya vizuri japo kidogo.

Mwalimu anatakiwa awe mpole na ufundishaji wake usiwe wa haraka haraka, aoneshe mapenzi kwa mtoto, hapaswi kumkemea hata kama anakaosea .

Watoto wa aina hii inashauriwa wapewe nafasi ya kujenga urafiki na watoto wenzao warika lao. Huko nyuma watoto wenye matatizo ya akili walikuwa wantengwa na watoto wenzao katika madarasa, kwa kuwekwa kwenye madarasa maalum.

Lakini siku hizi inashauriwa wachnganywe na wanfunzi wenzao wasio na matatizo ya akili, japo hata kwa nusu siku. Utaratibu huu hujulikana kitaalamu, kama mainstreaming.Itaendelea.....

Thursday, May 14, 2009

Kipanya na Usomaji Vitabu

Mimi kama mwalimu na mwandishi ninaliongelea sana suala la usomaji wa vitabu. Katika blogu hii, maandishi yangu mengi yanahusu suala hilo. Hapa kuna katuni ya Kipanya, ambayo nimeiona kwa Profesa Matondo. Inatoa mchango wake kwa mtazamo unaofanana na wangu. Nitatoa mfano mmoja.













Tarehe 21 Juni, 2008, niliendesha warsha Arusha, na katika mazungumzo yangu nililalamikia tabia ya waTanzania kutopenda kusoma vitabu. Nilitoa mfano kama huu wa Kipanya, kwamba waTanzania wanaposafiri katika basi, hutawaona wakisoma vitabu. Hapo mwanawarsha mmoja, mama Mwingereza, alitoa hoja kuwa utamaduni wa waTanzania wa kuongea na wenzao ndani ya basi unaonyesha wanavyojali mahusiano ya mtu na mtu, tofauti na wazungu, ambao kwao ni kila mtu na lwake. Alimaanisha kuwa jamii ya wazungu imekosa mshikamano; badala ya kuongea na binadamu mwenzao, wanashikilia kitabu. Hoja hii ilinifungua macho.

Kipanya ana tovuti yake hapa

Friday, May 1, 2009

Mchango wa Wabeba Boksi

Leo, siku kuu ya wafanyakazi duniani, napenda kuwakumbuka wabeba boksi. Hao ni waTanzania wanaoishi ughaibuni, wakifanya kazi za mikono, kama vile kubeba na kupanga mizigo ya bidhaa madukani, kusafisha maofisi, kusafisha vyombo mahotelini, kuwatunza wazee, na kadhalika. Watanzania wanaposema kubeba boksi, wanamaanisha kazi za aina hiyo. Na jina hilo linatokana na huu kweli kuwa wengi wa wahusika wanabeba na kupanga maboksi.

Wabeba boksi wanataniwa sana katika jamii ya kiTanzania. Wabeba boksi wengi nao wanajitania. Watanzania wengi wanaziona kazi za boksi kuwa ni kazi duni. Napenda kubadili mtazamo huo kwa kuelezea umuhimu wa boksi. Natumia hilo neno boksi kwa sababu linatumika pia kumaanisha kazi ya kubeba boksi.

Jambo moja la msingi ni kuwa wabeba boksi wanatumia nguvu zao kujipatia kipato. Wao ni tofauti na wezi au mafisadi, ambao wanakula jasho la wenzao. Kwa msingi huu, mbeba boksi anastahili heshima.

Kila kazi halali ina umuhimu wake katika jamii, iwe ni kilimo, uvuvi, usafishaji vyoo, ualimu, udaktari, au upigaji muziki. Kila kazi ya aina hiyo inastahili heshima. Mpiga boksi anafanya kazi muhimu. Bila yeye, jamii itakwama. Anastahili heshima.

Wabeba boksi, kama vile walivyo waTanzania wengine wanaoishi ughabuni, wanatoa mchango mkubwa katika kipato cha Taifa, kwa hela wanazotuma nyumbani, iwe ni kwa ndugu, jamaa, marafiki, au taasisi. Nimesoma taarifa kuwa mwaka 2008, kwa mfano, watu hao waliliingizia Taifa dola zaidi ya 100 millioni. Wenzetu waKenya wanaoishi nje waliingiza nchini mwao dola zaidi ya 400 millioni. Ni wazi kuwa mbeba boksi, akiwa ni mmoja wa watu hao, ni mtu muhimu kwa uchumi wa Taifa.

Je, lipi bora zaidi: kukaa vijiweni nchini bila ajira, au kubeba boksi? Hili ni suali la kutafakariwa.

Kuna wabeba boksi ambao, baada ya kukusanya hela, wanaanzisha miradi nyumbani wakiwa bado ughaibuni, na wengine wanarudi nyumbani na kuanzisha hiyo miradi. Kwa njia hiyo, wanatoa ajira kwa wananchi wenzao.

Mpiga boksi, kwa kukaa ughaibuni, anajifunza mengi. Anarudi nchini akiwa na upana wa mawazo kuhusu dunia na uzoefu wa nidhamu ya kazi, vitu ambavyo vinaweza kutoa changamoto kwa wananchi wengine.

Kwa ufupi, boksi lina umuhimu na heshima yake.

Sunday, April 26, 2009

Migogoro ya Kitamaduni Sehemu ya Kazi

Kadiri dunia inavyozidi kuwa kijiji, kwa maana kwamba umbali kutoka sehemu moja hadi nyingine unazidi kupoteza umuhimu, na mawasiliano baina ya watu yanazidi kuwa rahisi, na kukutana uso kwa uso inazidi kuwa rahisi, tutakuwa na kazi kubwa ya kujizatiti kukabiliana na tofauti za tamaduni duniani.

Watu wa kila utamaduni wana namna yao ya kufikiri, kuelewa, kufanya mambo, kuongea, na kadhalika. Wao kwa wao wanaelewana. Lakini dunia ya leo si ya watu kukaa na wenzao wanaoelewana tu, bali ni ya kukabiliana na watu wa tamaduni tofauti. Haijalishi kama uko Dar es Salaam, Tokyo, au Los Angeles. Mchanganyiko wa watu wa tamaduni mbali mbali unazidi kuziathiri sehemu zote za dunia.

Hapa Marekani, nimeona juhudi inayofanyika ya kujizatiti na hali hiyo. Sehemu za kazi, kwa mfano, kutokana na kuwa na wafanyakazi kutoka sehemu mbali mbali za dunia, wahusika wanaanza kuelewa umuhimu wa kujielimisha na kuelimishana kuhusu tofauti za tamaduni, ili kuzuia migogoro na kuboresha mahusiano kazini.

Mimi mwenyewe, kutokana na utafiti na uandishi wangu kuhusu masuala hayo, nimekuwa napata fursa za kwenda sehemu mbali mbali kuchangia mawazo na uzoefu wangu. Kwa mfano, tarehe 14 Februari, 2008, nilialikwa kwenye mji wa Minneapolis na kampuni ya RBC Wealth Management kutoa ushauri na uzoefu mbele ya timu ya uongozi wa kampuni hiyo.

Kampuni hii, kama kampuni zingine nyingi, ina mchanganyiko wa wafanyakazi kutoka sehemu mbali mbali duniani, wakiwemo waAfrika. Mazungumzo yangu yalihusu umuhimu wa kujifunza kuhusu tamaduni mbali mbali na mbinu za kukabiliana na hali hiyo, ili tuwe na maelewano na ufanisi mahali pa kazi na duniani kwa ujumla.

Pamoja na mazungumzo hayo, kampuni iliagiza nakala za kutosha za kitabu changu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, kwa watendaji waliohudhuria. Nilitambua kuwa kampuni hii inayo jadi ya kutafuta elimu kwa njia ya vitabu. Walinionyesha vitabu ambavyo walikuwa tayari wanavyo na wanavitumia, kwa lengo hilo hilo la kuelewa namna ya kushughulikia masuala yatokanayo na tofauti baina ya wafanyakazi. Kitabu kimoja walichonionyesha ni A Peacock in the Land of Penguins.

Hili ni fundisho kwetu waTanzania. Ni muhimu tuamke. Kama vile ilivyo Marekani na sehemu zingine duniani, waTanzania wanavyo vyuo, makampuni, na taasisi mbali mbali ambamo watu wa tamaduni mbali mbali wanashughulika. Kwa mfano, katika vyuo hivi na taasisi kuna watu wa kujitolea wanaotoka Marekani, Ulaya na sehemu zingine. Je, waTanzania wanaoendesha taasisi hizi wameshawahi kuwazia suala la elimu kwa wafanyakazi wote kuhusu tofauti za tamaduni? Mahusiano baina ya waTanzania na wageni katika sehemu hizo za kazi yakoje?

Kuna vile vile makampuni na taasisi za kigeni Tanzania, zenye wafanyakazi wananchi na wageni. Wahusika wana mkakati wowote wa kutoa elimu kuhusu tofauti za tamaduni?

Ukweli ni kuwa, mara kwa mara tunasikia taarifa za migogoro katika sehemu za kazi nchini Tanzania. Ninapoziangalia taarifa hizi, naona kuwa baadhi ya migogoro hii chanzo chake ni tofauti za tamaduni, au inachochewa na hizo tofauti za tamaduni. Tabia au kauli ya mgeni inaweza kuwaudhi waTanzania, ambao wanaichukulia kwa msingi wa utamaduni wa kiTanzania, na papo hapo, tabia au kauli ya mTanzania inaweza kumwudhi mgeni, kwa vile naye anaichukulia kwa misingi ya utamaduni wake. Shutuma zinatokea pande zote mbili. Nimeona, kwa mfano, waTanzania daima wanatoa malalamiko kuhusu ubaguzi. Sina hakika kama muda wote suala ni ubaguzi, bali nahisi kuwa wakati mwingine ni tofauti za tamaduni. Na wageni nao wanayo malalamiko mengi kuhusu waTanzania, ambayo msingi wake ni kutoelewa tofauti za tamaduni. Bila kuelimishana, magomvi hayo yataendelea na ufanisi sehemu za kazi utakuwa wa matatizo.

Je, waTanzania tunajizatiti vipi na masuala hayo ya dunia ya leo ambayo inazidi kuwa kijiji? Ninapenda sana kutafakari masuala hayo na kutoa mchango kwa kadiri niwezavyo. Nimeanza kuendesha semina nchini Tanzania. Ninajiandaa kufanya semina hizo mwaka huu pia. Kwa taarifa zaidi, yeyote anaweza kuwasiliana nami, kwa anwani hii: info@africonexion.com

Saturday, April 25, 2009

Mmarekani na Mswahili

Kwa miaka mingi nimekuwa katika utafiti wa tofauti baina ya utamaduni wa Mmarekani na ule wa Mswahili (yaani Mwafrika). Huwa najiuliza masuali mengi, kuhusu matatizo yanayoweza kutokea pale Mmarekani anapokutana na Mswahili. Nafahamu fika, na wengine wanafahamu pia, kuwa matatizo yanaweza kuwa mengi, kero, maudhi na kutoelewana. Lakini sikuwahi kuona kitabu kinachotoa mwanga kuhusu masuala hayo, kwa namna ya kuniridhisha.

Kwa vile kitabu cha aina hiyo niliyowazia hakikuwepo, niliamua kukiandika mimi mwenyewe. Niliona kuwa hakuna maana kukaa tu na kulalamika. Tatizo haliondoki kwa malalamiko, bali kwa vitendo.

Kitabu nilichoandika kinaitwa Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Napenda kuwashukuru wasomaji waliotoa maoni yao kuhusu kitabu hiki kwenye kumbi mbali mbali. Mmoja wa hao ni Dada Sophie ambaye ameandika maoni yake kwenye blogu mbali mbali.

Miaka ya karibuni, nimefahamiana na kikundi cha vijana wa Mto wa Mbu, Tanzania, wanaojishulisha na utalii. Hao vijana wananitia moyo kwa jinsi wanavyotambua umuhimu wa elimu, katika kufanikisha shughuli na miradi mbali mbali, na katika maisha kwa ujumla. Unaweza kusoma baadhi ya maelezo yao hapa na unaweza kusoma maelezo yangu hapa.

Sote tungefaidika iwapo wengine wangejitokeza na kuandika mawazo yao. Tunahitaji maandishi kuhusu tamaduni mbali mbali. Mimi niliandika kuhusu Wamarekani na Waswahili kwa vile hao ndio ninaowafahamu. Naendelea kuandika, hasa makala fupi fupi magazetini na katika majarida, kuhusu masuala hayo hayo. Panapo majaliwa, nitatoa kitabu kingine. Lengo ni kumsaidia Mmarekani na Mswahili kuepuka migongano isiyo ya lazima.

Kwa yeyote atakayependa, kitabu hiki na vingine vinapatikana Dar es Salaam, simu namba 0754 888 647 au 0717 413 073.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...