Monday, May 30, 2011

Kanisa laingilia kati mauaji ya North Mara

Kanisa laingilia kati mauaji ya North Mara

By George Marato

30th May 2011

CHANZO: NIPASHE

Wiki chache baada ya Jeshi la Polisi Kanda Maalum Tarime na Rorya, kutuhumiwa kuwaua kwa risasi raia watano na kujeruhi wengine kadhaa wakidaiwa kutaka kuvamia mgodi wa North Mara, Kanisa la Anglikana Doyosisi ya Tarime limeitaka serikali kuacha kuingiza siasa katika kutafutia ufumbuzi wa mgogoro huo.

Kanisa hilo limesema mgogoro huo wa muda mrefu kati ya wawekezaji na wananchi wanaozunguka mgodi huo unaomilikiwa na kampuni ya African Barrick Gold, umechangiwa na serikali kushindwa kuchukua hatua za haraka za kuwapatia haki ya msingi wananchi wa eneo hilo.

Akizungumza katika mahojiano maalum na NIPASHE nyumbani kwake juzi mjini Tarime, Askofu wa Anglikana Dayosisi ya Tarime, Dk Mwita Akiri, alisema lazima serikali ibebe lawama kuhusu mgogoro huo na roho za watu zinazopotea kila wakati kwa kushindwa kuchukua hatua za kuwatengea eneo mbadala la uchimbaji wananchi hao.

“Ndio tunakubali sera ya uwekezaji ya serikali na ndio imefanya kuwapo kwa hawa wenzetu wageni katika eneo la Nyamongo na ni faida kwa taifa kwa kupata kodi lakini tunajiuliza serikali inatambua wazi wananchi wa pale miaka yote mashamba yao ni uchimbaji sasa ilitegemea imewanyang’anya maeneo na kuwapa wageni na baada ya hapo nini kifuate kama si kuruhusu uvamizi huo,”alisema na kuongeza.

“Huwezi kumaliza tatizo kwa kuongeza ulinzi wa askari polisi na kufanya matumizi makubwa ya nguvu za dola katika eneo hilo cha msingi hapa serikali imechelewa tu kuchukua hatua za kumaliza mgogoro huu..utaleta majeshi yote lakini ipo siku utakuja kujuta kwani ni hatari kuimba amani wakati vijana hawana ajira na watu wana njaa,”alisema askofu huyo.

Kiongozi huyo wa dini aliwashutumu baadhi ya viongozi wa serikali kwa kutokuwa wa kweli kwa mamlaka wanazowakilisha kuhusu hali ilivyo katika eneo hilo, badala yake wamekuwa wakitoa taarifa za kupika na za uongo ili kuwapendezesha wawekezaji kwa maslahi binafsi.

“Rais akija hapa Tarime anaelezwa mazuri tu ya mwekezaji na jinsi anavyolipa kodi serikalini lakini haambiwi ukweli shida wanazopata wananchi wa eneo hilo na baada ya hapo wanamchukua kiongozi wa nchi bila kumpeleka kwa wananchi wanamwingiza mgodini kisha anaondoka je hapa unatarajia nini,”alihoji kingozi huyo.

Alisema hatua iliyofikia sasa ni lazima serikali ikatambua wazi mgogoro huo ni janga la kitaifa na si la Tarime pekee na endapo itashindwa kuchukua hatua za haraka kumaliza suala hilo kuna hatari eneo hilo likakosa amani, kuongezeka kwa chuki hasa kutokana na ongezeko la watu wanaozidi kupoteza maisha kwa kupigwa risasi.

Kwa mujibu wa Kamanda wa polisi kanda hiyo maalum Constantine Masawe, waliouawa kwa kupigwa risasi na polisi hivi karibuni kuwa ni Chacha Mwita(25)Chacha Ngoka(25)Chawali Bhoke(26)Mwikwabe Marwa(35) na Emanuel Magige(27) ambapo mmoja kati yao mkazi wa wilaya ya Serengeti na wengine wakazi wa wilaya ya Tarime.

+++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++
Mimi mwenye blogu hii napenda kuongezea kuwa kwa taarifa zaidi kuhusu kampuni ya Barrick na mambo yake sehemu mbali mbali za dunia, fuatilia hapa.
+++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...