Thursday, September 22, 2011

Kwa Mnyakyusa, Mbamba Bay

Katika pitapita zangu kwenye mji mdogo wa Mbamba Bay, kule Ziwa Nyasa, Agosti 2 na 3 mwaka huu, niliona tangazo ukutani, "Kwa Mnyakyusa." Tangazo hili lipo pembeni tu mwa kituo kikuu cha mabasi.


Sikupata wasaa wa kufuatilia tangazo hili na kujua asili yake au kumfahamu mhusika. Kwa vile hapo ni madukani, nilihisi kuwa ni jina la duka liliopo hapa.

Kitu kidogo kama hiki ni changamoto kwa yeyote anayetafakari mambo. Suala la majina ya mahali mbali mbali ni suala linaloweza kutafitiwa, na sehemu mbali mbali duniani wataalam wanafanya utafiti wa namna hii.

Hapa kwetu Tanzania napo tunahitaji utafiti huo, tuweze kujua asili ya majina ya sehemu mbali mbali na hivyo kutunza kumbukumbu zake.

Hii sehemu ya Mbamba Bay, "Kwa Mnyakyusa" inatuonyesha jadi iliyopo Tanzania ya kuzipa sehemu majina yanayotaja kabila. Nina hakika majina ya aina hii ni mengi. Kwa mfano, kuna sehemu kule Kibaha iitwayo "Kwa Mfipa."

Majina mengine ya sehemu mbali mbali yanawataja watu maalum. Kwa mfano, kuna sehemu kule Msasani iitwayo "Kwa Mwalimu." Katika hospitali ya Muhimbili kuna wodi iitwayo Sewa Haji. Wangapi wanajua asili ya jina hili? Kuna sehemu pale Sinza iitwayo "Kwa Remmy." Nasikia kuna sehemu kule Manzese iitwayo "Kwa Mfuga Mbwa." Kama nilivyosema, haya ni masuala ya kutafitiwa.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...