Saturday, December 1, 2012

Mwandishi Hemingway: Vitabu Vipya

Ernest Hemingway ni kati ya waandishi maarufu kabisa duniani. Alizaliwa mwaka 1899 karibu na mji wa Chicago, akafa kwa kujipiga risasi nyumbani kwake kwenye jimbo la Idaho mwaka 1961. Katika maisha yake, aliandika sana, akianzia kama ripota wa gazeti la Kansas City Star. Maandishi yake ni pamoja na riwaya, hadithi fupi, insha, masimulizi ya safari zake, barua magazetini, mashairi, na maelfu ya barua. Tangu wakati wa uhai wake hadi leo, watu wengi sana wamechambua maandishi yake na kuelezea maisha yake.


Vitabu kumhusu Hemingway vinaendelea kuchapishwa. Miezi ya karibuni, vimechapishwa vitabu kama Hemingway and Africa, Hemingway's Boat, na The Letters of Ernest Hemingway: Volume 1,1907-1922.

Kitabu cha The Letters of Ernest Hemingway: Volume 1, 1907-1922 nilikiona kwa mara ya kwanza miezi michache iliyopita katika duka la vitabu la Chuo cha St. Olaf. Ni kitabu muhimu sana kwa jinsi kinavyojumlisha kila barua ya Hemingway inayojulikana kwa kipindi cha miaka iliyotajwa. Ninapangia kujipatia nakala.

Ninayo nakala ya kitabu cha mwanzo cha barua za Hemingway, kiitwacho Ernest Hemingway: Selected Letters: 1917-1961. Lakini hiki cha sasa kinafunika kila kitu. Ni juzuu la kwanza, na inategemewa kwamba kutachapishwa majuzuu mengine, hadi kukamilisha maisha yote ya Hemingway.

Wakati wa maonesho ya vitabu yaliyofanyika wiki chache zilizopita mjini Minneapolis, mzee mmoja alifika kwenye meza yangu, na katika mazungumzo yetu nilimtaja Hemingway. Hapo hapo mzee akaniuliza kama nimeshasoma Hemingway's Boat.

Niligutuka kuona mzee huyu keshasoma kitabu hiki ambacho kimetoka karibuni tu. Lakini papo hapo nikakumbuka kuwa hapa ni Marekani, sio Tanzania. Usomaji wa vitabu hapa ni jambo la kawaida kabisa. Nilimwambia kuwa kitabu hicho nimekiona katika duka la vitabu Chuoni St. Olaf, na kwamba nimekiangalia angalia, ila sijakisoma. Hata hivi, tuliendelea na mazungumzo kuhusu mambo ya aina hiyo.

Kitabu cha Hemingway and Africa nilikiazima kutoka maktaba ya Chuo Kikuu cha Minnesota nikakisoma. Niko njiani kujipatia nakala. Hiki ni kimoja kati ya vitabu muhimu sana vinavyochambua uhusiano wa Hemingway na Afrika. 

Najihesabu kama mmoja wa wapenzi na wafuatiliaji wakubwa wa Hemingway. Nimefanya na naendelea kufanya utafiti juu yake na maandishi yake, hasa uhusiano wake na Afrika. Imekuwa ni furaha kwangu kuwapeleka wanafunzi Tanzania, kwa somo hilo.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...