Wednesday, December 18, 2013

Mama Kutoka Togo Kawahi Kununua Zawadi za Krismasi

Mama mmoja kutoka Togo ambaye ni rafiki ya familia yangu, alitutembelea wiki kama tatu zilizopita. Kati ya mambo mengine, alsema anataka kununua nakala mbili za kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Alisema ni zawadi ya Krismasi kwa marafiki zake waliopo hapa hapa Marekani.

Huyu mama ni kati ya wasomaji wa mwanzo kabisa wa kitabu hiki mara kilipochapishwa, mwanzoni mwa mwaka 2005. Alikipenda sana na kuanzia pale akawa anakipigia debe kwa watu mbali mbali. Hata kuna wakati ndugu yake alikuja kutoka Togo, akamtafutia nakala, ambayo alienda nayo Togo.

Namshukuru mama huyu. Nanatafakari suala hilo. Kuna vitabu vingi sana hapa Marekani ambavyo vinafaa kama zawadi kwa ndugu na marafiki. Lakini mama huyu kachagua kitabu changu. Halafu huyu mama hana kibarua au kipato cha ajabu: anafanya kazi ya kutunza wazee hospitalini.

Lakini, mama huyu, pamoja na ugumu wa kupata hela hapa Marekani, pamoja na ugumu wa matumizi kwa ujumla, kabana hela akaamua kununua vitabu hivi. Halafu, mteja anapokurudia tena, kwa hiari yake, ni jambo la kushukuru, kwamba aliridhika au alifurahishwa na kile alichokipata mwanzo kutoka kwako. Kwa vile mama huyu ni mpiga debe wangu makini, nilimpa punguzo zuri la bei.

Nimeona tabia hii ya kununua vitabu miongoni mwa wa-Afrika wa nchi zingine, ila sio Tanzania. Kwa mtazamo wangu, hao wenzetu wanatoka nchi ambazo zimewaelimisha.

Niliwahi kuandika makala katika blogu hii kuhusu suala la kumpa mtu kitabu kama zawadi ya Krismasi au Idd El Fitr. Mawazo niliyotoa bado ninayo vile vile vile.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...