Wednesday, October 25, 2017

Ninangojea Mwaliko Kuelezea Tamaduni

Nimeona tangazo la chuo kimoja cha hapa Minnesota kwamba wanajiandaa kuwapeleka wanafunzi kwenye nchi moja ya Afrika. Ni programu ambayo wamekuwa nayo kwa miaka kadhaa. Kila mara, wamekuwa wakitumia kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences katika maandalizi hayo, ili kufahamu mambo ya msingi ya tofauti za tamaduni. Wamekuwa wakinialika kuongea nao kabla ya safari.

Nilivyoona tangazo nilijisemea kuwa hawa watu lazima watatafuta kitabu changu tena, na watanitafuta tena, kutokana na nilivyoona siku zilizopita. Nimejifunza tangu zamani kuwa unapotoa huduma kwa mteja, toa huduma bora kiasi cha kumfanya mteja asiwe na sababu ya kutafuta huduma kwingine.

Kwa upande wangu, nilijenga uhusiano huu na wateja kwa awamu. Mwanzoni, nilikuwa ninatoa ushauri tu, hasa katika program za kupeleka wanafunzi Afrika, zinazoendeshwa na vyuo mbali mbali vya Marekani. Baadaye, nilichapisha kitabu, Africans and Americans: Embracing Cultural Differences,  na hicho kikawa kinawavutia wateja wapya. Si kwamba kitabu hiki kina kila kitu. Vile vile, wanaonialika hawanialiki nikawasomee hiki kitabu. Wanakuwa wameshakisoma, ila wanakuwa na shauku ya kujua zaidi kutoka kwangu mwandishi. Kitabu ni kama chambo na kianzio cha mazungumzo.

Ninaandaa kitabu kingine cha kuendeleza yaliyomo katika Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Kitakuwa na mwelekeo ule ule na mtindo ule ule, ila kitaibua mambo mapya. Tayari nimeshakipa jina, Chickens in the Bus, ambacho ni kichwa cha sura mojawapo katika kitabu hiki.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...