Saturday, February 21, 2009

Nchi Zinazoendelea: Ni Zipi Hizo?

Dhana ya "nchi zinazoendelea" imejengeka vichwani mwa watu, tangu zamani. Pamoja na dhana hiyo, kuna pia dhana ya "nchi zilizoendelea." Je, dhana hizo zina mantiki yoyote?

Binafsi, ingawa zamani nilikuwa na mawazo kama wengine, kwamba kuna nchi zilizoendelea na zile zisizoendelea au zinazoendelea, miaka hii nimegundua kuwa dhana hizi hazina mantiki, na ni ushahidi wa kasumba vichwani mwa watu, au elimu duni.

Kwa mujibu wa dhana hizo, nchi kama Marekani, Uingereza, Sweden, Ujerumani, na Japani zinahesabiwa kuwa zimeendelea. Lakini nchi kama Tanzania, Kenya, na Uganda zinahesabiwa kuwa nchi zinazoendelea.

Kwa nini nasema dhana hizi ni duni? Kwanza, hakuna nchi duniani ambayo imesimama tu. Kila nchi iko katika mchakato na mabadiliko katika uchumi, siasa, utamaduni, na kadhalika. Marekani ya mwaka juzi ni tofauti na Marekani ya leo, na Marekani ya miaka mitano ijayo itakuwa tofauti na hii ya leo. Na ndivyo ilivyo kwa nchi zote. Kama ni tekinolojia, kwa mfano, tekinolojia inabadilika muda wote katika nchi kama Marekani. Kama ni utamaduni, ni hivyo hivyo. Na ndivyo ilivyo kwa nchi zote. Mabadiliko hayaishi, iwe ni katika Tanzania au Uingereza.

Kama huu mchakato na mabadiliko ndio maendeleo, basi kila nchi duniani ni nchi inayoendelea. Ni upuuzi kuziona baadhi ya nchi kama nchi zilizoendelea, wakati nazo ziko katika kubadilika muda wote.

Lakini, jambo la msingi zaidi ni dhana ya maendeleo. Maendeleo ni nini, na nani anayeweka vigezo vya kupima haya maendeleo? Hili ni suali la msingi.

Kwa ujumla, baadhi ya nchi, hasa zile ambazo zilikuwa zimetutawala wakati wa ukoloni, na zile zenye nguvu katika dunia ya leo, ndizo zinazoweka vigezo. Na wengi wamefundishwa kukubali hayo mawazo ya kikoloni na kikoloni mamboleo, bila kufikiri. Kwa vile Ulaya inajitapa kwamba imeendelea, Waafrika na wengine sehemu mbali mbali za dunia nao wanakubali hivyo na kuziona nchi zao kuwa ni nchi zinazoendelea au zisizoendelea. Hii ni kasumba.

Ingekuwa tunavyo vichwa timamu na tunavitumia ipasavyo, tungetafakari mambo sisi wenyewe, na tungetathmini dhana ya maendeleo. Tungejiuliza, maendeleo ni nini? Tungejiuliza iwapo dhana ya maendeleo ya watu wa Ulaya ni sherti tuipokee na kuikubali. Tungechukua jukumu na wajibu wa kujitungia vigezo vyetu na kuvitumia.

Kwa vile hatufanyi hivyo, tumebaki kuwa kasuku. Chochote kinachotoka Ulaya au Marekani tunakiona ni maendeleo. Papo hapo, watu wa Ulaya hawaoni chochote cha kwetu kuwa ni maendeleo. Ni pale tu tunapoiga mambo yao ndipo tunahesabiwa kuwa tunaendelea.

Hata kama jambo halina maana, maadam linatoka Ulaya au Marekani, watu katika nchi zetu wanaliona ni maendeleo. Hata kama ni mambo yasiyoendana na utu, maadam yametoka Ulaya, watu wetu wanayaona ni maendeleo. Kwa mfano, nchi zinazoitwa zimeendelea zimefanikiwa kuharibu mazingira kwa ujenzi wa viwanda na miundombinu mbali mbali, kiasi kwamba hewa katika nchi hizo sio safi, maji sio salama, mahusiano ya jamii ni ya wasi wasi.

Cha kushangaza ni kuwa watu wetu nao wanataka tufanye kama wanavyofanya Ulaya au Marekani, na miji yetu iwe kama ya huko Ulaya na Marekani, na viwanda na miundombino iwe kama ilivyo Ulaya na Marekani. Wanatamani nchi zetu ziwe na kila kitu ambacho kiko Ulaya na Marekani, ili tuonekane tumeendelea. Je, hayo ndio maendeleo?

Kwa hali ilivyo, hali ya nchi kadhaa kujiona kuwa zimeendelea, nchi zetu hazitafikia wakati wa kuwa sawa na hizo zingine. Mfumo huu uliopo hautaisha. Watu wa Ulaya na Marekani wataendelea kuyaona mabadiliko ya nchini kwao kuwa ndio maendeleo, na sisi tutakuwa daima watu wa kufuata hayo ya kwao. Kwa mtindo huu, hatutaweza kuwa mbele yao au sambamba nao.

Nchi zote ziko katika hali ya mabadiliko ya kila aina, katika nyanja mbali mbali. Hakuna nchi iliyomaliza mchakato huu na kuwa nchi ambayo imesimama na haibadiliki tena. Pasipo kuwa na vigezo vinavyozingatia haki ya kila watu duniani kuchangia katika kutunga tafsiri na viwango vya maendeleo, si sahihi kuendelea kutumia dhana ya nchi zilizoendelea na nchi zinazoendelea au zisizoendelea. Inatubidi tubadili fikra; tukatae huu mkondo uliopo sasa wa kuitwa au kujiita nchi zinazoendelea. Ni fikra tegemezi, za kikasuku, na kikoloni mamboleo, fikra zinazothibitisha kuwa tunahitaji elimu.

Wednesday, February 4, 2009

Kuwasomea Watoto Vitabu

Enzi za mababu na mabibi zetu, ilikuwa ni kawaida kwa wazee kukaa na watoto jioni na kuwasimulia hadithi. Utamaduni huu ulikuwa sehemu ya maisha. Ilikuwa ni sehemu ya elimu waliyopewa hao watoto. Hapakuwa na shule tulizo nazo leo, wala vitabu, lakini wazee walikuwa walimu bora, waliotumia mbinu mbali mbali, kama hizi hadithi, katika kuwaelimisha watoto.

Siku hizi, kutokana na kuwepo kwa vitabu, tunayo fursa ya kutumia vitabu kuendeleza elimu ya watoto. Kama hatuna uwezo wa kuwasimulia hadithi kwa mtindo wa mababu na mabibi zetu, tunayo fursa ya kuwasomea vitabu. Wenzetu katika nchi kama Marekani wanaendeleza utamaduni huu kwa kuwasomea watoto hadithi za vitabuni. Watoto wa kiMarekani wanategemea mzazi awasomee vitabu. Ni kawaida kwa mzazi kumsomea mtoto kitabu kabla hajalala.

Mashuleni na kwenye maktaba za Marekani, kuna utaratibu wa kuwa na vipindi vya kuwasomea watoto vitabu. Watu wanajitolea kwenda maktabani au mashuleni kufanya kazi hiyo, wawe ni wafanyakazi maofisini, madaktari, wanajeshi au polisi, wanasiasa au viongozi.

Kila mtu atakumbuka, kwa mfano, kwamba siku ile ya Septemba 11, 2001, ambapo mji wa New York ulishambuliwa na magaidi, Rais Bush alikuwa darasani akijumuika na watoto waliokuwa wakisoma. Rais mpya Obama, pamoja na shughuli zake nyingi, anafuata utamaduni huo, kama ilivyoandikwa hapa.

Kuwasomea watoto vitabu kunawajengea mazoea ya kusoma na kuwapanua mawazo. Ni fursa ya kujenga na kuimarisha uhusiano baina ya watoto na watu wazima. Wataalam wa elimu ya watoto wanasema kuwa kumsomea mtoto vitabu tangu anapokuwa mdogo ni njia moja ya kumjengea msingi wa mafanikio maishani.

Watanzania tuko wapi katika suala hili? Je, wazazi wanaendeleza utamaduni wa mababu na mabibi wa kuwasimulia watoto hadithi? Na kwa vile tuko katika utamaduni wa vitabu, tunavyo vitabu majumbani? Tunawasomea watoto wetu?

Watu wazima katika Tanzania wanatumia muda mwingi kwenye sehemu zinazoitwa vijiweni. Wangeweza kutumia muda huu kwenda shuleni kusaidiana na walimu kwa namna moja au nyingine, kama wanavyofanya Wamarekani, kwa kujitolea. Wakati walimu wanasahihisha daftari, kwa mfano, wazazi wangeweza kusimamia shughuli za nje ya darasa, kama vile usafi, kilimo, au ufugaji, au wangeweza kusaidia somo moja au jingine.

Kuna watu wazima wengi Tanzania ambao wamesoma vya kutosha, na wangeweza kutoa mchango mkubwa mashuleni, kwa msingi wa kujitolea. Kama wabunge, wafanyabiashara, viongozi wa mitaa, watafiti na wengine wangefanya hivyo, watoto wangefaidika, na Taifa lingepiga hatua nzuri.

Saturday, January 31, 2009

Raha ya Kununua Vitabu

Tangu nilipokuwa kijana mdogo, nilipenda kununua na kusoma vitabu. Niliwahi hata kununua vitabu ambavyo vilikuwa vigumu mno kwangu kuvielewa. Nakumbuka, kwa mfano, kitabu kimoja cha falsafa, kilichoandikwa kiIngereza, ambacho nilinunua ila nilipata taabu sana kukisoma. Pamoja na kuwa somo la kiIngereza nilikuwa nalipenda na kuliweza kuliko masomo yote, kitabu hiki kilinishinda kwa wakati ule wa ujana wangu. Lakini nilifurahi kuwa nacho katika maktaba yangu ndogo.

Nilinunua pia vitabu vya kiSwahili. Kwa mfano, nakumbuka vizuri kitabu cha Shaaban Robert, Maisha Yangu. Vile vile, nakumbuka kitabu cha Yusuf Ulenge, Nguzo ya Maji na Hadithi Nyingine. Wakati ule, sikujua kabisa kuwa Yusuf Ulenge alikuwa mdogo wa Shaaban Robert. Hayo nimekuja kujua mwaka 2008, baada ya kununua na kusoma kitabu kiitwacho Barua za Shaaban Robert 1931-1958, kilichochapishwa na Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa mara ya kwanza mwaka 2002. Nimefurahi sana kufahamu kuwa Yusuf Ulenge alikuwa mdogo wa Shaaban Robert, na barua zilizomo katika kitabu hiki ni hazina kubwa kwa yeyote anayemwenzi Shaaban Robert.

Nilipoingia Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kusoma, mwaka 1973, niliendelea na tabia ya kununua vitabu. Nilinunua vitabu vingi sana, kiasi kwamba, wanafunzi wenzangu wakinitembelea bwenini walikuwa wanashangaa uwingi wa vitabu vyangu. Niliendelea hivyo nilivyokuwa masomoni katika chuo kikuu cha Wisconsin-Madison, 1980-86. Kwa miaka sita niliyokaa pale, nilinunua vitabu vingi sana, na nakisia nilitumia yapata dola 2000 kununulia vitabu. Nilikuwa nimepata ufadhili wa shirika la Fulbright, na haikuwa vigumu kwangu kutumia sehemu ya hela hizo kwa kununulia vitabu. Siku moja, nakumbuka, nilitumia dola 100 kununulia seti nzima ya hadithi za Alfu Lela u Lela zilizotafsiriwa kwa kiIngereza na Sir Richard Burton. Niliporudi Tanzania na shehena hiyo ya vitabu, kuendelea kufundisha katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, watu walinishangaa kwa kununua vitabu badala ya gari.

Utamaduni wa kununua na kusoma vitabu ninauona sana hapa Marekani. Ni kawaida watu kwenda kwenye maduka ya vitabu, kuangalia vitabu na kuvinunua. Wanahudhuria sana tamasha za vitabu. Mara nyingi, watu wanapotaka kumpelekea mtu zawadi, wanamnunulia kitabu, awe ni rafiki, ndugu, mzazi, au mchumba. Zawadi ya kitabu inapendwa. Watu wakienda kupumzika kwenye sehemu za mapumziko, kama vile bustani za mijini, aghalabu wanakuwa na kitabu cha kujisomea.

Ninafahamu tabia za Wamarekani kuhusu suala la kununua vitabu na kujisomea. Hapa siongelei wanafunzi, bali raia wa kawaida, wafanyakazi na kadhalika. Ninakutana nao mara kwa mara ninaposhiriki katika maonyesho ya vitabu, au ninapokwenda kutoa mihadhara. Hapa naleta picha chache za matukio haya.


Hapo naonekana nikiwa na mama mmoja kwenye warsha mjini St. Paul, Minnesota. Anaangalia kwa makini vitabu vyangu. Tabia hii inanivutia na pia ndio tabia inayohitajika, kwani kujielimisha ni wajibu wa kila binadamu. Kusoma vitabu ni njia moja ya kujielimisha.















Hapa juu nimesongwa na wataalam mbali mbali katika sekta ya elimu, ambao walikuwa wanahudhuria mkutano kwenye Chuo Kikuu cha Iowa. Nilikuwa hapo na vitabu vyangu. Kama inavyoonekana, tuko katika shughuli nzito ya masuali na majibu.



Hapa niko na akina mama kwenye warsha niliyosaidia kuendesha, kwenye mji wa Grantsburg, Wisconsin. Wanaonekana wakiwa na furaha kwa kuvipata vitabu. Hii hali ya kufurahi kwa sababu ya kupata kitabu ni nadra nchini Tanzania. Hapo kwenye picha, mama moja anaonekana ameshika hela. Bei ya kitabu kimoja ni dola 14. Lakini anaonekana mwenye furaha. Ninapokuwa Tanzania, nikiwaambia watu kuwa bei ya kitabu changu ni dola 14, wanastuka na wengi wanaishia hapo. Wako wanaoomba wapunguziwe bei, na wako wanaoomba wapewe bure. Sio kila anayeomba kupunguziwa bei au kupewa kitabu cha bure ana tatizo la hela. Watanzania wengi wana hela sana. Hela wanazonunulia bia, kwa mfano, ni nyingi sana, kila wiki. Msimamo wangu ni kuwa hao wenye kuthamini bia kuliko vitabu wanao uhuru wa kuendelea na msimamo wao huo. Tunapishana mawazo, kwani mimi naamini kuwa mawazo yaliyomo katika vitabu vyangu yana thamani kuliko bia. Halafu, najiuliza, inakuwaje watu hao wasiombe kupunguziwa bei ya bia, ambayo inapanda muda wote?

Hapo ni pale kwenye mkutano Chuo Kikuu cha Iowa. Niko katika mjadala na mtaalam wa masuala ya elimu baada ya yeye kununua kitabu.


Picha hii inanivutia labda kuliko zote na ni hazina ya pekee kwangu. Huyu mama ni wa kutoka Nigeria. Hapa tulikuwa kwenye mkutano katika mji wa Minneapolis. Alifika na mwanae kwenye meza yangu na tuliongea kuhusu shughuli zangu za ufundishaji, utafiti, na uandishi. Kilichonivutia zaidi ni kitendo chake cha kuja na binti yake. Kumlea mtoto katika hali hii ya kupenda vitabu ni jambo la kupigiwa mfano. Je, ni wazazi wangapi katika nchi yetu wanafanya hivyo? Lazima tujitafiti, na tujizatiti ipasavyo katika kukuza taifa la kesho.

Saturday, January 24, 2009

Chakula Bora

Niliwahi kuandika makala, Kuku kwa Mrija. Leo nimeona nilete makala juu ya vyakula anavyokula Rais Mpya wa Marekani, Barack Obama, makala ambayo inasisitiza umuhimu wa kuangalia tunakula nini, na inaonyesha kuwa kiongozi anaweza kutoa mfano kwa wananchi. Kama nilivyosema katika ile makala ya Kuku kwa Mrija, kuna tabia mbaya inayojengeka miongoni mwa Watanzania, ya kushabikia vyakula ambavyo au havina faida kiafya au vina madhara kiafya. Lakini kutokana na kasumba, watu wanaona wanajipatia hadhi ya juu kwa kutumia vyakula hivi.

Makala ninayoleta hapa imeandikwa kwa kiIngereza, na ingawa blogu yangu hii inatumia kiSwahili, nimeona nivunje utaratibu huu kutokana na umuhimu wa suala la chakula. Ninategemea kuwa wale ambao hawajui kiIngereza labda wataweza kupata msaada wa kutafsiriwa makala hii. Watanzania na wengine wote tunaweza kujifunza mengi kutokana na makala hii inayomhusu Rais Obama. Soma hapa.

Monday, January 19, 2009

Waafrika Wanamwenzi Obama?

Kesho, tarehe 20 January, 2009, Barack Obama anaapishwa kama rais wa 44 wa Marekani. Dunia nzima iko katika heka heka za furaha na matumaini yasiyo kifani kutokana na ushindi wa Obama katika kampeni za urais wa Marekani.

Waafrika nao wamejawa na furaha, na wanajivunia, wakizingatia kuwa baba yake Obama ni Mwafrika mwenzao, kutoka Kenya. Waafrika wanaamini kuwa Rais Obama atajenga uhusiano bora na Afrika, kwani Afrika ni kwake.

Lakini je, Waafrika wanaomshangilia Obama wanamfahamu Obama au wanashangilia tu kwa vile kwa asili yake ni Mwafrika? Ukweli ni kuwa, Waafrika wengi hawana fikra wala mtazamo kama wa Obama kwa mambo mengi. Kwa mfano, Obama amekuwa mstari wa mbele kwa shughuli za kujitolea kwa ajili ya jamii yake na binadamu kwa ujumla, amekuwa mtetezi wa wanyonge, na ameonyesha mfano mzuri wa kujibidisha katika elimu na kuwa binadamu bora.

Ajabu ni kuwa hata Waafrika ambao ni wazembe, wanaoendekeza rushwa na ufisadi, wasiothamini elimu, wasiothamini suala la kujitolea, wote wanamshangilia Obama. Kuna nini katika vichwa na mioyo ya watu hao?

Obama amezingatia sana suala la heshima kwa wanadamu wote bila kujali tofauti za rangi, dini, taifa, na kadhalika. Anaamini kuwa kila mtu anastahili fursa ya kufanya yale ambayo yanaendana na uwezo wake. Ana imani kubwa kuhusu uwezo wa binadamu, na kila binadamu.

Waafrika wengi ni wabaguzi, kwa misingi ya kabila, dini, na kadhalika. Hawatambui usawa wa binadamu, bali wanamthamini mtu wa kabila lao, kijiji chao, ukoo wao, dini yao, na kadhalika. Wakati Obama amechaguliwa na Wamarekani wa rangi na dini mbali mbali, na wakati Obama anawahamasisha Wamarekani kujiona kama kitu kimoja, bila kujali tofauti zao, wawe ni weusi, weupe, wanawake, wanaume, wa dini mbali mbali, na kadhalika, Waafrika wengi hawako tayari hata kumpigia kura mtu wa kabila lisilo lao.

Inashangaza kwamba Waafrika hao ambao wanapigana na kuchukiana kutokana na tofauti za lugha, utamaduni, kabila, na kadhalika, wanashangilia ushindi wa Obama na wanaamini kuwa Obama ni mtu wao. Inashangaza kuwa nao wanaamini wanamwenzi Obama, badala ya kutambua kuwa namna ya kweli ya kumwenzi Obama ni kufuata nyayo zake. Ni sahihi kabisa kuuliza: hao Waafrika wanamwenzi Obama kweli au wanajikanyaga?

Saturday, January 17, 2009

Watanzania na Mkutano wa Sullivan

Mwanzoni mwa mwezi Juni, 2008, mji wa Arusha ulipata fursa ya kuwakaribisha wageni wengi kwenye mkutano mkuu wa nane wa Sullivan. Nilikuwa katika mkoa wa Arusha pamoja na Wanafunzi kutoka Chuo cha Colorado, ambao nilikuwa nawafundisha kuhusu maandishi na safari za Ernest Hemingway maeneo hayo. Kwa hivi, sikupata fursa ya kuhudhuria mkutano wa Sullivan.

Hata hivi, nilipata fursa tele ya kuongea na Watanzania kuhusu mkutano huo. Lengo la taasisi ya Sullivan ni kuchangia maendeleo ya Afrika, kwa kujenga uhusiano wa kibiashara, kijamii, na kadhalika baina ya Afrika na hasa Marekani na Ulaya. Mwanzilishi wa taasisi alikuwa Mmarekani Mweusi, Rev. Leon Sullivan, na kwa sababu hiyo, taasisi hii imekuwa na mvuto mkubwa miongoni mwa Wamarekani Weusi. Hao wanaikaribisha kwa mikono miwili fursa ya kuwekeza barani Afrika na kuungana na Waafrika katika kutekeleza ajenda ya maendeleo.

Basi, kwenye mkutano wa Arusha, Wamerekani Weusi walikuja wengi sana, wakiwemo watu maarufu katika nyanja mbali mbali, wanasiasa, wafanya biashara, na wanataaluma. Mategemeo ya mkutano yalikuwa mengi, kama vile kutoa fursa ya wawekezaji kuleta mitaji, kujenga ushirikiano baina ya wafanya biashara wa Tanzania na hao wageni, na kujenga ushikiriano katika nyanja mbali mbali.

Katika mazungumzo yangu na Watanzania, nilikuwa nawauliza kama wao wamejiandaa vipi kwa yote hayo. Niliwauliza, Je, wanavyowania kushirikiana na Wamarekani, wamefanya juhudi yoyote kuwafahamu hao Wamarekani? Wanamfahamu Mmarekani Mweusi? Hapo nilimaanisha ufahamu wa tabia, hisia, imani, maadili, namna ya kufikiri, namna ya kuongea, na kadhalika. Je, Mtanzania anafahamu hayo? Au anadhani kuwa ni jambo rahisi tu kukutana na Wamerekani na kushughulika nao?

Maongezi yalikuwa mazuri, na nilipata fursa ya kuwaeleza umuhimu wa kujiandaa. Niliwapa mifano hai kuhusu tabia na hisia za Wamarekani Weusi. Mfano moja niliutoa kwa kutumia tabia za Watanzania wanapokuwa na wazungu. Watanzania, kama walivyo Waafrika wengine, wana tabia ya kumtetemekea mzungu. Katika mahoteli ya utalii, kwa mfano, wahudumu wa kiTanzania wanawahangaikia sana wazungu, na hawaoni tatizo kumwacha mteja Mwafrika akiwa bila huduma au kumwacha akingoja huduma hiyo hiyo, hata kama aliwahi.

Niliwaeleza kuwa endapo Wamarekani Weusi watakuja na kuona tabia hii, hawatafurahishwa; watakata tamaa, na huu unaweza ukawa ndio mwisho wa hili wazo la kujenga ushirikiano. Tatizo ni kwamba Watanzania kwa ujumla hawaelewi undani wa hali ya Marekani na mahusiano baina ya Wamarekani Weusi na weupe. Hawaelewi hisia na fikra za Wamarekani. Niliwaasa Watanzania waache kuishi katika ulimwengu wa giza na ndoto, bali waanze kujielimisha.

Mfano mwingine niliotoa ni namna ya kuongea. Wamarekani wanaongea kwa namna ambayo inaweza kuonekana ni maudhi kwa Mtanzania, wakati wao kwao ni sahihi. Na wao wanaweza kuudhiwa na namna Watanzania wanavyoongea, wakati kwa upande wa Tanzania ni sahihi. Na kuna mambo mengine mengi yanayotofautiana baina ya tamaduni hizi mbili.

Kwa hivi, niliwaambia Watanzania kuwa suala la kujielimisha kuhusu hao Wamarekani ni la msingi. Sikusita kuwaeleza kuwa mimi ni mtafiti na naandika sana kuhusu masuala hayo. Niliwaeleza kuwa waanze kulichukulia suala la kujisomea na kujielimisha kuwa ni suala muhimu, hata katika biashara. Kununua kitabu kwa ajili hiyo ni sawa na kununua kifaa kingine chochote kinachoboresha biashara. Kwa lugha rahisi, kitabu ni zana na mtaji muhimu.

Nitaendelea kufanya mazungumzo ya aina hii, kwa namna yoyote. Kwa bahati nzuri, nimeshaanza sasa utaratibu wa kuendesha semina, ninapokuwa Tanzania. Nilifanya hivyo mwaka jana, kama inavyoonekana hapa, na ndivyo itakavyokuwa siku zijazo, panapo majaliwa.

Sunday, January 11, 2009

Matawi ya CCM Nje ya Nchi

Kwa miezi mingi sasa, kumekuwa na habari za kuanzishwa matawi ya CCM nje ya Tanzania. Naamini kila Mtanzania anaweza kuwa na maoni yake kuhusu jambo hili, na mimi ninayo pia, ingawa mimi ni Mtanzania ambaye si mwanachama wa chama chochote cha siasa.

Niliishi nje ya Tanzania kwa mara ya kwanza miaka ya 1980-86, nikiwa masomoni Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, Marekani. Nilipofika hapo, nilipokelewa vizuri na Watanzania waliokuwa wanasoma hapo. Walinipa kila msaada na ushauri niliohitaji ili kuzoea maisha yale mapya.

Jumuia hii ya Watanzania, ingawa haikuwa kubwa, ilikuwa kama familia huku ugenini. Wakati wa shida na raha tulijumuika. Na mara kwa mara tulikuwa tunakutana kwa maongezi na kustarehe pamoja. Kama mtu alishindwa kuja kwenye mikutano hii, ilikuwa ni sababu ya labda kuzidiwa na shughuli au kuwa safarini. Lakini hatukuwa na mtu aliyekuwa hatakiwi au aliyejiona hatakiwi au hahusiki katika mikutano hiyo.

Ningependelea Watanzania wanoishi nje waendeleze jadi hiyo. Mazingira ya huku nje ni tofauti na yale ya Tanzania. Mtu aliyeko Tanzania hana tatizo la upweke. Kuna ndugu, jamaa, marafiki na majirani muda wote. Mtanzania aliyeko Tanzania hana tatizo la kujikuta katika utamaduni mgeni na athari zake. Yuko kwake.

Watanzania walioko nje wanakutana na utamaduni usio wao, na hali hii ina athari za aina aina kwa kila mtu, na inaweza kuwa na madhara kisaikolojia. Watanzania wanaoishi nje ya nchi wanahitaji kuwa karibu na Watanzania wenzao bila ubaguzi wa aina yoyote. Kuanzisha matawi ya CCM au chama kingine chochote cha siasa huku nje ni kuathiri hali ambayo tayari ni ngumu.

Nakumbuka tulivyoishi Wisconsin, halafu najiuliza: Je, ingekuwa ndio leo, tuko Wisconsin, halafu baadhi yetu waanzishe tawi la CCM, hali ya jumuia yetu ingekuwaje? Je, kama baadhi nao wangeanzisha tawi la chama kingine, au matawi ya vyama vingine, hali ya jumuia yetu huku ugenini ingekuwaje?

Vyama vya siasa Tanzania, kuanzia CCM, vimekuwa mstari wa mbele katika kuhujumu amani na mshikamano nchini, hasa wakati wa uchaguzi. Mifano iko wazi, kama vile yaliyotokea Zanzibar mwaka 2001, kama ilivyoelezwa hapa, Tarime mwaka 2008, na sehemu mbali mbali nyingine. Vurugu za Visiwani ziliendana na mauaji, uvunjwaji wa haki za binadamu, na uharibifu wa mali uliosababisha watu kukimbilia sehemu kama Kenya na hata Somalia, kama inavyoelezwa hapa na hapa. Ni ajabu sana, kwamba Watanzania wakimbilie Somalia. Haya yote ni matokeo ya ukosefu wa uongozi bora, uongozi wa busara na haki. Kama CCM, ambayo ilishika hatamu za uongozi nchini, ingekuwa na uongozi bora, wa busara na haki, matatizo au hayangekuwepo au yangetatuliwa bila ubabe na vurugu kama zile.

Wasi wasi wangu ni kuwa, yanapoanzishwa matawi ya CCM nje ya nchi, fujo zinazoletwa na vyama vya siasa huko Tanzania zitahamia pia nje. Utengano unaoimarika Tanzania, kutokana na siasa za vyama, nahisi utatokea pia huko nje. Na kama nilivyosema, afadhali Tanzania kuna fursa nyingi za mtu kujumuika na wengine, na hakuna upweke na matatizo ya kisaikolojia yanayohusiana na kuishi katika utamaduni wa kigeni.

Ni vema Watanzania wanaoishi nje waweke nguvu katika kuboresha mshikamano na utaifa. Watoto wa waTanzania na vijana wa kiTanzania wanaoishi nje wanahitaji kuelimishwa kuijua Tanzania, kujua historia, siasa, utamaduni na maisha ya Tanzania, na kulipenda Taifa lao. Katika mazingira ya huku nje, jukumu hili ni gumu sana. Hata waTanzania ambao ni watu wazima wanaoishi nchi za nje wana shida katika kudumisha uelewa wa nchi yao, kutokana na kuwa mbali. Wengi hawana fursa ya kwenda Tanzania mara kwa mara, na mengi yanawapitia mbali. Wangeweka kipaumbele katika kuifahamu Tanzania, ili waweze kuwafundisha pia watoto wao. Katika mazingira haya, kushughulika na matawi ya CCM ni kupoteza mwelekeo unaopasika.

Watoto, vijana, na watu wazima wanaoishi Tanzania hawana tatizo hilo, kwani wako katika mazingira muafaka ya kuifahamu nchi yao. Wanakomaa katika uTanzania, na hata wakiamua kujiunga na chama cha siasa, hakuna tatizo. Lakini je, ni sawa kwa vijana wa kiTanzania wanaoishi nje kujibidisha na CCM wakati suala la utaifa linayumba katika mazingira ya ugenini? Je, ni sahihi watoto wa kiTanzania wanaokulia nje, ambako tunashindwa kuwapa elimu kamili ya siasa ya kiTanzania, waanze maisha yao kwa kuona mfarakano baina ya waTanzania, badala ya kukuzwa katika fikra zinazoendana na ukweli kuwa Tanzania ni nchi inayozingatia sana utaifa?

Kuna wakati ziitokea taarifa za mpango wa kuanzisha tawi la CCM sehemu fulani hapa Marekani. Wazo hili lilizua hisia kali za upinzani. Sijui kama tawi hilo lilianzishwa, ila ilikuwa wazi kabisa kuwa wazo la kuanzisha tawi hilo hapa Marekani lingeleta mtafaruku miongoni mwa Watanzania. Taarifa mbali mbali zimeonyesha pia kuwa hata sehemu za Ulaya, kuanzishwa kwa matawi ya CCM kumeleta hisia kali ambazo hazichangii mshikamano miongoni mwa Watanzania.

Hali hii ingetosha kuwafanya viongozi wa CCM Tanzania kutambua kuwa kuanzishwa matawi ya CCM huku nje kunaweza kuathiri mshikamano wa Watanzania na kuleta picha mbaya kuhusu Tanzania. Watanzania walioko nje wanapaswa kuwa na umoja na mshikamano kwa kila hali ili waweze kuwa mabalozi wazuri wa nchi yetu, waweze kuwa mfano kwa Waafrika wengine tunaokutana nao huku nje, ambao wengi wao wanabaguana kwa msingi wa ukabila. Sisi Watanzania tulipokuwa Wisconsin, tukikutana pamoja na kuongea Kiswahili, baadhi ya Waafrika walikuwa wanatuuliza kama sisi ni kabila moja. Hawakuwa na namna nyingine ya kufahamu au kuelezea kitendo cha watu kuwa na mshikamano wa namna hii, nje ya dhana ya ukabila. Hayo ndio mazuri ya Tanzania na uTanzania, ambayo naamini yanatishiwa na vitendo vya kuanzishwa matawi ya CCM huku nje.

Hayo ndio mambo yanayonisumbua akilini ninaposoma taarifa za kufunguliwa kwa matawi ya CCM huku nje. Matawi ya CCM au chama kingine chochote yakifunguliwa nchini, mimi sioni tatizo. Ni sehemu ya haki na uhuru wa kila Mtanzania. Lakini picha inakuwa tofauti tunapozungumzia hali halisi ya jumuia za Watanzania wanaoishi nchi za nje. Nilitegemea viongozi wa CCM wangefanya uchambuzi wa kina wa suala hilo, lakini sijaona dalili zozote za kunipa matumaini.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...