Sunday, November 8, 2009

Vitabu Bila Karatasi

Kitu kimoja ambacho kinampambanua mwanadamu na viumbe wengine ni tekinolojia. Chimbuko la binadamu lilifungamana na uwezo wake wa kutengeneza na kutumia zana mbali mbali, kuanzia zana za miti na mawe, hadi chuma na leo zana zinazoendeshwa na umeme au nguvu za nyuklia. Katika maendeleo haya ya tekinolojia, binadamu amegundua na kuweza kutumia nishati mbali mbali, kama vile maji, upepo na jua.

Uandishi na uchapishaji vimefungamana na maendeleo ya tekinolojia. Tangu binadamu wa kwanza alivyoandika michoro kwenye miamba au kuta za mapango, kwenye ngozi za wanyama, vibao vya udongo, au karatasi, yote hayo ni matunda ya tekinolojia. Leo kuna mashine na mitambo ya aina aina ya kuchapisha magazeti na vitabu.

Maendeleo ya tekinolojia ya uchapishaji yametufikisha mahali ambapo uchapishaji sasa unaweza kufanyika bila karatasi. Vitabu vinaandikwa na kusomwa bila kutumia karatasi, bali kwa mtindo wa digitali. Kwa mtindo huu wa digitali, mtu anaandika kitabu chake kwa kutumia kompyuta, na anakihifadhi mtandaoni. Mwenye kutaka kukisoma kitabu hiki anatumia kifaa maalum kiitwacho "e-reader" au "e-book reader." Kuna vifaa vingine pia. Mtu huyu anaingiza kitabu kutoka mtandaoni katika kifaa chake na kukisoma kwenye skrini ya kifaa hicho. Anaweza kuhifadhi vitabu vingi katika kifaa hicho.

Hatua hii ni muhimu, kwani kati ya faida zake nyingi ni kuwa inachangia kuhifadhi miti na misitu ambayo ilikuwa inaharibiwa ili kutengeneza karatasi. Tekinolojia hii ya digitali ni baraka kwa waandishi na wasomaji. Waandishi hawalazimiki tena kuwategemea wachapishaji. Wasomaji hawalazimiki kwenda kwenye duka la vitabu, au kuagiza kitabu na kukingoja kisafirishwe. Wanakipata papo kwa papo mtandaoni. Baadhi ya vitabu vangu, sasa vinapatikana kwa mtindo huo, kama inavyoonekana hapo upande wa kulia.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...