Thursday, August 12, 2010

Kitabu: "Ualimu Katika Shule za Msingi"


Nimemaliza kusoma kitabu kiitwacho “Ualimu Katika Shule za Msingi” kilichoandikwa na Anael Malewo na kuchapishwa na Dar es Salaam University Press. Nilikiona katika duka la vitabu la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam tarehe 27 Julai, 2010, nikakinunua, kwa shilingi 1,500 tu.
Nilivutiwa na kitabu hiki kwa sababu mimi ni mwalimu ambaye napenda kuelewa hali halisi ya shule zetu na mfumo wa elimu, kuanzia shule za msingi hadi vyuo vikuu. Sababu nyingine ni kuwa niliwahi kuandika makala juu ya mwalimu wa shule ya msingi katika gazeti la “Kwanza Jamii,” ambayo inapendwa na wasomaji na imo pia katika kitabu cha CHANGAMOTO.
“Ualimu Katika Shule za Msingi” ni kitabu chenye manufaa sana. Kinatoa mwanga kuhusu wadhifa, wajibu, na maadili ya ualimu, falsafa na mbinu za ufundishaji, wajibu wa serikali, wazazi, na jamii kwa ujumla katika elimu ya shule za msingi. Kitabu hiki kinaelezea pia matatizo ya shule za msingi na kupendekeza ufumbuzi.
Mwandishi anathibitisha anavyothamini elimu na maslahi ya Taifa. Anarejea kwenye miongozo ya Taifa letu, kama vile “Azimio la Arusha.” Kitabu hiki kinasisitiza mambo ambayo mwalimu anapaswa kuyazingatia wakati anawafundisha watoto, kama vile tabia zao na mazingira watokako. Nimekisoma kitabu hiki kwa furaha na ari kubwa, kwa jinsi kinavyoelimisha.
Ni wazi kuwa mwandishi wa kitabu hiki ni mtaalam. Katika jalada la nyuma la kitabu tunasoma kuwa mwandishi wa kitabu hiki “ni mwalimu mwenye uzoefu mkubwa katika ufundishaji na uongozi wa elimu hapa nchini.” Ana uzoefu kama mwalimu mkuu wa shule, afisa elimu wa wilaya, mkuu wa chuo cha ualimu, mwalimu katika shule za kati, na katika chuo cha ualimu cha Marangu.
Kitabu hiki ni hazina kwa kila mtu anayethamini elimu, iwe ni ya shule ya msingi au vyuo vikuu. Ni muhimu kisomwe na kila mtu, kwani kina mambo yanayotuhusu sote.

1 comment:

Yasinta Ngonyani said...

Nafurahi kuona huchoki kuhamasisha juu ya usomaji wa vitabu kwani kama tujuavyo waTanzania ni wavivu sana wa kununua vitabu pia kusoma anakubali kununua ugimbi kuliko kununua kitabu ambacho kitamwelimisha.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...