Tuesday, July 12, 2011

Nimebeba Maboksi ya Kwenda Njombe (NJOUCO)

Jana na leo nimehenya sana na kazi ya kubeba maboksi. Kwanza niliyafungasha ofisini kwangu, halafu nikayapakia katika gari. Kisha nikaendesha gari maili hamsini na kidogo hadi mjini Coon Rapids, ambako nilihenya tena kuyapakua na kuyaingiza katika stoo kubwa. Hapa nilipo nimechoka na nasikiliza maumivu mwilini.

Hayo maboksi ni shehena ya majarida ambayo nayapeleka chuo kikuu kipya cha Njombe, NJOUCO. Ni majarida ya "New England Journal of Medicine" (NEJM), na "Journal of the American Medical Association" (JAMA), kwa kipindi cha kuanzia miaka nane iliyopita hadi miezi michache iliyopita.

Hata mimi ambaye siko katika taaluma ya udaktari nafahamu kuwa NEJM na JAMA ni majarida maarufu. Majarida hayo nimepewa na mzee moja daktari mstaafu ambaye alipata habari kuwa huwa napeleka vitabu Tanzania. Ninamshukuru sana mzee huyu.

Niliwahi kuongelea habari ya hiki Chuo cha Njombe katika blogu hii. Nilipomweleza Mchungaji Dr. Kimilike ambaye ni mratibu wa NJOUCO kuwa ninayo majarida hayo, aliniunganisha na Global Health Ministries, ambao wanashughulikia miradi ya aina hii sehemu mbali mbali za dunia, hasa upande wa afya. Shukrani tele kwa msaada wao wa kusafirisha majarida hayo. Jumla nimefungasha na kupeleka maboksi 12.

Kinachofurahisha ni kuwa baada ya miezi kadhaa, shehena hii ya majarida itatua NJOUCO. Ni hazina kubwa kwa wanafunzi, walimu, madaktari, na watafiti katika masuala ya afya na matibabu.

Napenda kumalizia kwa kusisitiza kuwa hiki ni chuo kipya, ambacho mahitaji yake ni mengi. Hali hii inakuwa ni changamoto kwetu kushiriki katika kuleta mafanikio yanayotarajiwa.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...