Tuesday, November 22, 2011

Nimekutana na Wadau wa New Hampshire

Leo nimebahatika kukutana na wadau wawili, mtu na mkewe, kutoka New Hampshire, ambako ni waumini wa Kanisa la Holy Trinity. Wamekuja hapa Minnesota kwa masuala ya shirika la Bega kwa Bega, ambalo linashughulikia ushirikiano na maendeleo katika mkoa wa Iringa.

Wadau hao, Mama Dot na Mzee Kurt, wanajiandaa kwenda Iringa, ambako wameshaenda mara kadhaa. Katika ujumbe wao wa mwanzo kwangu, walisema kuwa Profesa Joe Lugalla, ambaye wako wote New Hampshire, aliwahamasisha tukutane. Profesa Lugalla, kama mimi, anawasaidia wa-Marekani wanaokwenda Tanzania kwa kuwapa ushauri unaohitajika. Kwa msingi huo, amekuwa mdau mkubwa wa kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences" na amekipigia debe kwa watu hao tangu kilipokuwa mswada tu, mkusanyiko wa dondoo mbali mbali, usio na sura ya kitabu.

Wadau hao wawili nami tumeongea kwa karibu saa mbili. Maongezi yetu yalihusu shughuli wanazofanya Iringa katika mpango wa Bega kwa Bega, na hasa maandalizi wanayofanya ya kupeleka kikundi cha wa-Marekani Iringa katikati ya mwaka ujao. Mama Dot amewahi kufundisha Chuo Kikuu Cha Tumaini, na tuliongelea pia habari za chuo kile, ambacho nami nimekifahamu tangu mwanzo na ninafahamiana na baadhi ya viongozi na walimu wake. Tuliongelea sana tofauti za tamaduni baina ya wa-Marekani na wa-Afrika, kama nilivyozieleza katika kitabu changu, ambacho wamekisoma vizuri. Walikuja na nakala yao, na wakaniomba niisaini. Nami nilifanya hivyo.

Tumefurahi kukutana, na tumekumbushana kuhusu watu kadhaa wa Tanzania na Marekani ambao sote tunawafahamu, kuanzia walioko Chuo Kikuu cha Tumaini hadi walioko New Hampshire. Ni kweli, milima haikutani bali wanadamu hukutana.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...