Saturday, November 12, 2011

Vitabu Nilivyonunua Leo Apple Valley

Jioni ya leo nilipita kwenye duka la Half Price Books, mjini Apple Valley. Nilikuwa natoka Minneapolis.

Nilipoingia ndani, niliwakuta watu wengi humo, wanazunguka huko na huko wakiangalia vitabu. Kwenye sehemu ya kulipia, kulikuwa na foleni. Hii ni jioni ya Jumamosi, wikiendi, na wa-Marekani wamejazana katika duka la vitabu. Je, jambo hili linawezekana nchini mwetu?

Baada ya kuangalia vitabu vingi, nilichagua viwili. Kimoja ni The Hottentot Venus kilichotungwa na Rachel Holmes, na kingine ni The Time and the Place and Other Stories kilichotungwa na Naguib Mahfouz.

Hottentot Venus, ni habari ambayo nimeifahamu kwa miaka mingi. Ni jina alilopewa Saartje Baartman, mama mw-Afrika kutoka Afrika Kusini ambaye alipelekwa Ulaya kama kivutio, hasa kwa vile alikuwa na makalio makubwa sana, kutokana na desturi za kwao za kukuza makalio. Huko Ulaya alinyanyasika sana, kwani walimweka kwenye uzio kama mnyama, akitembezwa kwenye miji mbali mbali kwa maonyesho, na kukutana na adha za kila aina. Alifariki mwaka 1815.

Ni habari ya kusikitisha sana. Maiti yake iliwekwa katika jumba la makumbusho kwa miaka mingi, na hata ubongo na sehemu zake za siri zikiwa zimenyofolewa na kuwekwa kama kivutio cha aina yake. Hatimaye, serikali ya Mzee Mandela iliweka shinikizo kuwa masalia ya Saartje Baartman yarudishwe Afrika Kusini kwa mazishi sahihi. Mazishi hayo yalifanyika mwaka 2002.

Huo ni ufupi wa habari nilizozifahamu kwa miaka kadhaa. Lakini sasa nimenunua hiki kitabu, nitazifuatilia kwa undani zaidi.

Naguib Mahfouz ni kati ya waandishi maarufu waliopata kuishi. Alikuwa mtu wa Misri. Aliandika riwaya nyingi na hadithi fupi. Mwaka 1988 alipata tuzo ya Nobel kwa uandishi wake. Nimesoma na kufundisha baadhi ya vitabu vyake, kama vile Midaq Alley. Hiki kitabu nilichonunua leo ni kati ya vile ambavyo sikuwa navyo.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...