Thursday, November 17, 2011

Nimekutana na Mdau Mjini Apple Valley

Leo nimekutana na mdau Dr. Mary Sheedy Kurcinka, mhadhiri na mwandishi maarufu wa masuala ya malezi ya watoto wachanga. Nilishamtaja siku chache zilizopita hapa. Tuliongea kwa saa moja na nusu mjini Apple Valley.

Mama huyu alishatembelea Nigeria na Ghana wakati wa ujana wake, akaandika kuhusu malezi ya watoto wachanga katika jamii ya wa-Yoruba. Sasa anapangia kwenda Tanzania, mwanzoni mwa mwaka ujao.

Mazungumzo yetu ya leo yalihusu suala hilo analofanyia utafiti. Aliponiandikia ujumbe wa kwanza, wiki kadhaa zilizopita, alisema alisikia habari zangu kutoka kwa muumini wa Shepherd of the Valley Lutheran Church.

Leo kaja na nakala ya kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho alikinunua hivi karibuni. Amesema amekisoma na amekipenda sana. Kimemkumbusha aliyoyaona alipoishi Nigeria na Ghana. Kama ilivyo kawaida kwa wa-Marekani, aliniomba nisaini nakala yake, nami nikafanya hivyo.

Katika kuongea naye, nimepata motisha ya kufuatilia suala la malezi ya watoto wachanga, kwa kuzingatia saikolojia ya hao watoto wachanga, na changamoto zinazowakabili wazazi wao katika tamaduni mbali mbali. Leo tumejaribu kuongelea suala hilo tukizingatia tamaduni za wa-Marekani na wa-Afrika. Leo ulikuwa mwanzo, na tunategemea kuendelea kubadilishana mawazo.

Kwa vile sote wawili ni waandishi, tumepata fursa ya kuongelea masuala ya uandishi pia, kubadilishana uzoefu. Katika maongezi hayo, nilipata fursa ya kumweleza changamoto zilizonifanya nikaandika kitabu changu hiki, na pia nilivyojifunza kutokana na jinsi mwandishi Ernest Hemingway anavyofafanua dhana ya ukweli katika uandishi.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...