Friday, June 29, 2012

Kugombana na Madaktari ni Uchuro

Mgomo wa madaktari umeanza tena, siku chache zilizopita. Inasikitisha kuona kuwa tumefikia hali hiyo. Ukiniuliza nani namhesabu kama mwajibikaji mkuu aliyesababisha tatio hili, nitakuambia kuwa ni serikali ya CCM. Huo umekuwa msimamo wangu tangu pale ulipotokea mgomo wa mwanzo wa madaktari wiki kadha zilizopita. Nilieleza msimamo huo hapa.

Siku chache zilizopita, nilimsikiliza mwenyekiti wa madaktari wanaogoma, Dr.Stephen Ulimboka, akiongelea jinsi uhaba wa vitendea kazi ulivyo. Alitaja mfano wa kifaa cha "CT-scan" ambacho kimeharibika Muhimbili yapata miezi mingi iliyopita.

Kama nilivyosema katika makala yangu ya mwanzo, sera za serikali ya CCM zinasabisha upotevu mkubwa wa mali ya Tanzania, kama vile madini. Serikali yenyewe imekiri kuwa mikataba ya madini ya siku zilizopita ilikuwa ni ya hasara kwa Taifa. Lakini je, serikali imeshamwajibisha yeyote aliyehusika katika kusaini mikataba hiyo?

Je, ni kweli kuwa nchi hii haiwezi kununua hicho kifaa cha "CT-scan"? Kutokana na sera mbovu za CCM, makampuni kama Barrick yanafaidika sana na dhahabu yetu wakati sisi, ukifananisha na mapato wanayopata wao, sana sana tunaambulia mapato duni sawa na njugu kiganjani, na tunaambulia uharibifu wa mazingira na afya za watu wanaoishi maeneo ya migodini,

Kitu kimoja kinachokera katika mgogoro huu baina ya serikali na madaktari ni jinsi madai ya madaktari yanavyopotoshwa. Wako ambao wanaongea kama vile wanachodai madaktari ni posho na maslahi yao tu. Ukweli ni kuwa madaktari wana madai ya msingi ya kuwatetea wananchi. Kuna uchakachuaji wa makusudi unaofanywa kuhusu jambo hilo, ili ionekane kuwa madaktari hawajali maishai ya wananchi.

Ni kweli kuwa mgomo huu unaathiri maisha ya wa-Tanzania. Hili si jambo jema. Lakini serikali haina haki ya kuwashutumu madaktari kwa hoja hii ya kutojali maisha ya wa-Tanzania, wakati serikali hiii hiii inawakumbatia hao wanaoitwa wawekezaji ambao wengi wao wanahujumu maisha na afya za wa-Tanzania, achilia mbali kuharibu mazingira maeneo ya migodini. Serikali ingekuwa haifanyi hayo, ingekuwa na haki ya kuwaandama madaktari kwa hoja hii ya kuathiri maisha ya wa-Tanzania.

Katika mgogoro baina ya serikali na madaktari, kuna pia suala la serikali kutumia mwanya wa sheria na uamuzi wa mahakama. Serikali haifanyi haki inapokwepa kuwajibika kwa yale yanayodaiwa na madaktari, madai ambayo ni ya kweli, na yako katika uwezo wa serikali na nchi yetu hii ambayo ina utajiri mkubwa. Kama suala ni sheria na maamuzi ya mahakama, sote tunakubali kuwa sheria ichukue mkondo wake.

Lakini kinachokera ni kuwa serikali inatumia mwanya huu kufunika kile ambacho sisi wengine tunakiona ni uzembe na kutowajibika kwa serikali yenyewe. Madai ya madaktari ni ya msingi, na yako katika uwezo wa serikali hii. Kwa serikali kutowajibika hapo na kukimbilia mahakamani kuwabana madaktari kwa kipengele cha sheria tu, sio jambo la haki na haliiweki serikali katika sura nzuri, kwa mtazamo wangu.

Kama nilivyosema katika makala yangu ya mwanzo, kugombana na madaktari si jambo jema. Nilikumbushia usemi wa wahenga kuwa tusidharau wakunga na uzazi ungalipo. Napenda kuongezea kwa dhati kabisa kuwa kugombana na madaktari si dalili njema bali ni uchuro.

2 comments:

tz biashara said...

Wapunguze mishahara na posho kwa mawaziri na wabunge ili wafidie kwa madokta kama uchumi hauruhusu ili kubana matumizi.La sivo siku zinavokwenda mbele Tahrir inaweza ikazaliwa Bongo kwasababu Zanzibar wameamua wafanye kivyao tusiwalaumu ila ni kuchoshwa na maisha yasiyo na uhakika.

Anonymous said...

Professa Umeongea Ukweli nimeisoma hii kwa makini mwanzo nilikuwa kama upeo wa wengine kwanini Ma-Daktari wagome? Madaktari wengi hujitolea kwa moyo bila watu kujuwa na pia ni kweli vifaa vya kufanyia kazi ni kidogo nchini kwetu Tanzania, Wa-Tanzania lazima waunge mkono Madaktari sema wasigome tu kwa wale wagonjwa Mahututi tu, Madaktari ni muda wapewe haki zao Na Tanzania waanze kuweka vitega uchumi vya ajira Mikoani na Visiwani sasa Dar-es-salaam inajaa na magonjwa yatajaa watu wanavyozidi kuwa wengi. Inshallah tutashikamana yale ya elimu na Akhera tufanye mambo kwa vitendo na kuongea sauti za juu bila kuogopa, Wa-Tanzania Serikali inaweka kipa umbele sana Matangazo ya Bia(Ulevi) kuliko elimu na Ushirikina umejaa bado sana sijui kwanini? Tabia ya Vijana wenzangu inazidi kuharibika Inshallah Mwenyezi atatujaalia tutafunguka. Profesa mie naomba endelea kutupa Elimu kwenye hii Blog kuliko Maswali ya kizushi ya blog zengine sisemi kwa unafiki nasema ukweli wewe na mjengwa Blog zenu mnaandika kwa umakini mnafikiria mbele na kufungua vichwa vya watu. Vijana kama sie wenye umri kwenye 20-35 tunahitaji hizi blog MZ.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...