Monday, July 2, 2012

Nimetua Tanga

Niko Tanga, ambapo niliwasili juzi tarehe 30, nikitokea Dar es Salaam. Tulisafiri na basi la Tashriff, ambalo nililifurahia sana. Kwanza, kwa kipindi kirefu katika safari, tulikuwa tunaangalia video za hotuba za Mwalimu Nyerere. Jambo hilo lilinifurahisha sana, nikizingatia umuhimu wa mchango wa Mwalimu Nyerere, umuhimu wa kuukumbuka na kuuenzi mchango huo, na pia nikizingatia jinsi umbumbumbu uliochanganyika na majungu unavyozidi kushamiri nchini Tanzania kuhusu Mwalimu Nyerere.

Baada ya hizo hotuba, tuliwekewa miziki. Lakini jambo la kuvutia pia ni jinsi dreva alivyokuwa anaendesha gari kwa ustaarabu na hekima, akiwa anaangalia mwendo vizuri. Kwa kweli, nawajibika kuipa hongera kampuni ya Tashriff kwa yale niliyoyashuhudia.

Nimeshafika Tanga mara kadhaa. Ni mji maarufu katika historia na utamaduni Tanzania. Katika safari zangu hizo, nimepiga picha kadhaa, na niliandika habari za maktaba ya Tanga. Safari hii, kama ningekuwa nimejiandaa vizuri, ningekwenda hadi Machui, kijiji alikozaliwa Shaaban Robert. Ningekwenda kuona kaburi lake.

Ninamwenzi mwandishi huyu. Nimeandika makala juu yake ambayo imechapishwa katika Encylopedia of African Literature, na makala nyingine ambayo nimeichapisha katika kitabu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Pia nimeandika kuhusu kitabu chake kilichochapishwa miaka michache tu iliyopita, kiitwacho Barua za Shaaban Robert. Soma hapa. Mchango aliotoa Shaaban Robert, mwenyeji wa mji huu wa Tanga, katika uandishi Tanzania na duniani kwa ujumla ni mkubwa sana. Ingetakiwa tuwe na maadhimisho yake ya mara kwa mara, tuwe na maandishi na makongamano kuhusu mchango wake, tuwe na kozi mbali mbali mashuleni kutathmini maandishi yake; tuwe na makala magazetini kuhusu kazi zake, na mambo mengine ya aina hiyo. Kampuni za utalii zingekuwa mstari wa mbele katika kuzihifadhi na kuzitumia kumbukumbu hizi. Lakini hilo halitafanikiwa kwa hali tuliyo nayo nchini, ya kutokuwa na utamaduni wa kusoma vitabu.

Haya ndio baadhi ya mawazo niliyo nayo, wakati huu, nikiwa katika mji huu wa Tanga. Kama sitafika kijijini Machui safari hii, nitahakikisha ninafanya hivyo safari nyingine, Insh'Allah.


3 comments:

Yasinta Ngonyani said...

kila la kheri!

Mbele said...

Shukrani. Ni mji mzuri huu. Sijui kama umeshafika hapa?

Yasinta Ngonyani said...

Hapana sijawahi fika ila nasikia tu ni kwamba kuzuri sana na pia wana kiswahili kizuri sana...

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...