Friday, July 20, 2012

Bado Niko Songea

Bado niko Songea. Jana asubuhi sikumsikia muadhin. Nadhani nilizidiwa na usingizi. Lakini baadaye kidogo nilisikia mlio wa kengele za Kanisa Katoliki. Nadhani zilikuwa za kanisa kuu la Jimbo, ambalo liko hapa mjini Songea.

Kama nilivyosema katika ujumbe wangu wa juzi, naona ni jambo jema kukumbushana kwamba kuna Muumba. Haijalishi kwangu kama nakumbushwa na muadhin msikitini au kengele kanisani.Mimi sio mtu wa dini sana, ni muumini wa kawaida sana, isipokuwa naona umuhimu wa kuikumbuka dini na kujitahidi kufuata maadili yake.

Jana mchana nilienda Ruhuwiko, kumtembelea dada yangu. Tulipata fursa ya kuongea masuala ya familia na mengine mengi. Nilitegemea pia kwenda kutembelea chuo kikuu kipya kilichofunguliwa hivi karibuni na Kanisa Katoliki hapa mjini. Ratiba ya jana haikuniwezesha kufanya hivyo. Nategemea nitapata fursa hiyo leo.

Mimi nilisomeshwa na Kanisa Katoliki. Sitasahau msisitizo katika taaluma, nidhamu na maadili ya kazi nilivyofundishwa katika shule zao, ambayo yamenifikisha hapa nilipo. Nitashukuru daima.

Leo, Insh'Allah, nitaendelea na ziara zangu hapa Songea, na pia kukutana na wadau mbali mbali.


1 comment:

Yasinta Ngonyani said...

hakika umesema kweli ni muhimu sana kuzingatia dini. Nimefurahi sana kusoma kuwa umefika hadi Ruhuwiko Karibu sana nyumbani kwetu. Angalao upate hata maji..baba anakipiga kweli kimatengo mtaongea sana. Ukifika hapo chuoni si mbali kufika kwetu..nasubiri mengiiii kutoka Songea/Ruhuwiko...

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...