Saturday, March 30, 2013

Wa-Marekani Watua kwa Mama Lishe, Usa River

Mwezi Januari mwaka huu, nilipokuwa Tanzania nikifundisha kozi ya Hemingway, niliandaa fursa mbali mbali za kuwawezesha wanafunzi, ambao ni wa-Marekani, kushiriki katika utamaduni wa wa-Tanzania, ili kujifunza. Tulikuwa tumefikia Colobus Mountain Lodge, iliyomo pembeni mwa Arusha National Park. Siku moja, mara tu baada ya wanafunzi hao kuwasili nchini niliwapeleka kwenye mji mdogo wa Usa River, ili wakazunguke na kujionea. Niliamua kuwasafirisha katika dala dala, tukiwa tumebanana. Usafiri ule ulikuwa kitu kipya kabisa kwao, lakini niliona ni muhimu kwao, wajifunze. Tulifika Usa River, tukazunguka mitaa kadhaa, na kisha tukasogea tena pembeni mwa barabara kuu. Hapo wanafunzi walimwona mama lishe akiwa kazini, wakapanga foleni kujipatia chipsi mayai.



Kwao hili lilikuwa jambo jipya, ila walifurahia hicho chakula. Niliridhika sana kwamba wanafunzi walipata fursa hiyo ya kujionea na kufaidi huduma ya mama lishe, kwani ni sehemu muhimu katika utamaduni wa Tanzania ya leo.











Wanafunzi walikuwa wengi zaidi ya hao wanaoonekana pichani. Mama lishe alifanya kazi kubwa ya kuwahudumia. Wala hiyo haikuwa mara yao ya mwisho kuja hapa. Walifika tena, na kama tungekaa siku nyingi eneo hili la Usa River, wangefika tena na tena.

Kwa vile wengi wanaosoma blogu hii ni wa-Tanzania, naomba tukumbushane tu kuwa mbali ya elimu inayotokana na safari za aina hii, kwa wageni na wenyeji, na mbali na fedha nyingi inayoingia katika hazina ya nchi, shughuli hizi za kuwapeleka wanafunzi Tanzania ni zinachangia kipato cha watu wa kawaida, kama vile mama lishe, dobi, mwenye nyumba ya kulala wageni, na muuza ndizi sokoni. Safari hii, hata vinyozi nao walijipatia biashara.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...