Sunday, April 14, 2013

Tamko la CHADEMA Kuhusu Njama za Kukichafua

TAMKO LA CHADEMA KUHUSU NJAMA ZA KUKICHAFUA ZINAZOFANYWA NA GENGE LA VIONGOZI WAKUU WA CCM NA VYOMBO VYA DOLA, LIMETOLEWA JIJINI DAR ES SALAAM LEO, MACHI 14, 2013 NA MJUMBE WA KAMATI KUU NA MWANASHERIA WA CHAMA, MH. MABERE NYAUCHO MARANDO

Ndugu waandishi wa habari;

LEO tumewaita hapa ili kuwaomba mtufikishie ujumbe kwa Watanzania, kwamba nikiwa mwanasheria na mtu ambaye nimepata ujuzi wa kazi za ushushu, nimefanya uchunguzi matukio haya ya utekaji na utesaji na kugundua mambo mengi mno.

Uchunguzi huu nimeufanya kabla na baada ya kukamatwa kwa Mkurugenzi wetu wa Ulinzi na Usalama, Willifred Muganyizi Lwakatare, ambaye hivi sasa anashitakiwa mahakamani kwa tuhuma za kupanga ugaidi.

Nimefanya hivyo kwa kuangalia maslahi mapana ya taifa langu na chama changu. Katika uchunguzi wangu huo, nimegundua mambo mengi ikiwamo kuwapo kwa genge la watu ndani ya serikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM), wanaopanga mipango hii ya kishetani na kisha kuwasingizia watu wengine.

Angalieni mfano huu: Unaoitwa na polisi na Mwigulu Nchemba, “mkanda wa Lwakatare” unadaiwa uliwasilishwa jeshi la polisi Desemba mwaka jana. Lakini jeshi hilo halikumkamata yoyote wala kumhoji, hadi pale Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri, Absalom Kibanda, alipovamiwa na kuumizwa.

Aidha, Nchemba amedai kumiliki video ile Desemba mwaka jana, lakini rekodi hiyo iliwekwa kwenye mitandao ya kijamii (YouTube na Jamii Forum) baada ya kutekwa kwa Kibanda. Hapa mtu makini anaweza kujiuliza, hiki kimelenga nini?

Kwamba genge hili la kina Nchemba na wenzake, walipanga kumteka Kibanda, wakatimiza lengo lao hilo, baadaye wakaingia kwenye plani B ya kutaka kuihusisha Chadema. Wakamtumia Ludovick Joseph Rwezahula ambaye ni mshitakiwa wa pili katika kesi ya Lwakatare, kufanikisha mkakati wao huu wa kishetani.

Ndugu waandishi wa habari;

Huu ni mchezo mchafu na wahatari mno ambao kwa vyovyote vile, haupaswi kuvumiliwa. Kuanzia sasa nimeamua kwa dhati kabisa, kukomesha mchezo huu ambao unahatarisha uhai wa taifa letu.

Kwa kuanzia, kesho Jumatatu, nitaongoza jopo la mawakili sita wa Chadema kumtetea Bw. Lwakatare. Wenzangu wengine katika kesi hii, ni Profesa Abdallah Safari, Tundu Lissu, Edson Mbogoro, Peter Kibatara na Nyaronyo Kicheere. Huko mbele tutaongeza mawakili wengine, akiwamo mmoja anayewekwa na familia ya Lwakatare.

Ndugu waandishi wa habari;

Mnaweza kujiuliza, kwa nini Chadema kimechukua uamuzi huu wa kuweka kundi kubwa la wanasheria katika kesi hii ya Lwakatare? Jibu ni kwamba tumegundua kuwa kesi hii imefunguliwa kwa lengo maalum la kuidhoofisha Chadema na kuinusuru CCM ambayo inakabiliwa na dhahama ya kushindwa katika uchaguzi mkuu ujao kutokana na kushamiri kwa makundi.

Hivyo wameamfungulia kesi Lwakatare, kwa lengo la kutaka kuaminisha umma kuwa Chadema ni chama cha magaidi, kinapanga ugaidi na hivyo kichukiwe. Hilo ndilo lengo lao. Basi!

Ndugu waandishi wa habari;

Pili, nitakwenda mahakamani kuwasilisha ombi maalum la kuomba amri ya mahakama kuagiza makampuni ya simu za mkononi kuwasilisha mahakamani statement za simu za watu kumi (10) ili kusaidia mahakama kutenda haki na jamii kujua ukweli wa mambo haya.

Watu ambao nitaomba mahakama itoe amri ya kuletwa taarifa zao simu

na meseji (sms) ni Naibu Mkurugenzi wa Usalama wa Taifa nchini (TISS), Jack Zoka, anayetumia simu Na. 255756809535, Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mwigulu Lameck Nchemba, anayetumia simu tano zikiwamo 0754 008888, 0757 946223, 0714 008888 na 0787 513446 na Ludovick Joseph Rwezahula, ambaye simu zake ni,0715 927100 na 0753 927 100.

Mwingine ambaye mawasiliano yake yanahitajika, ni Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Emmanuel Nchimbi, anayetumia simu Na. 0754 003388, Mhariri Mtendaji wa magazeti ya Mwananchi, Dennis Msaky anayetumia simu mbili, 0655 331010 na 0764 331010 na Bw. Sinbad Mwagha, ambaye ni afisa wa idara ya usalama wa taifa, anayetumia simu 0754 006355.

Wengine, ni Bw. Shaali Ali, afisa mwinge wa usalama wa taifa anayetumia simu Na. 0716990099, Saumu K. Malungu, mwenye kutumia simu 0719 541 434 na 0789 614 629, simu mbili zinazotumiwa na mtuhumiwa mkuu wa utekaji wa Dk. Steven Ulimboka, Bw. Ramadhani Abeid Igondo ikiwamo 0713 760 473, simu za Bw. Ridhiwani Kikwete ambazo ni 0754 566299, 0784 566 299, simu ya Dr. Steven Ulimboka, ambayo ni 0713 0713 731 610, pamoja na simu zote tatu za Willifred Lwakatare, ambazo ni 0786 774697, 0713 237869 na 0758 417169.

Ndugu waandishi wa habari;

Mtu mwingine muhimu nitakayeomba mahakama itoe amri ya kutolewa kwa taarifa zake, ni mwandishi wa habari na mpigapicha wa magazeti ya serikali, Muhidini Issa Michuzi. Mwandani huyu wa Ikulu, ndiye aliyeandika ujumbe kwa njia ya emeili kuipongeza ofisi binafsi ya rais (OBR) na usalama wa taifa kwa kupata video ya Lwakatare.

Pongezi za Michuzi kwa TISS ndizo zinanisukuma kuiomba mahakama kuagiza kupatikana taarifa zake. Michuzi anaipongeza TISS kwa kuibua njama za wahalifu, lakini mimi ninajua TISS ikipata njama za aina hiyo haraka inapeleka ushahidi polisi, lakini huu wa Lwakatare ulipelekwa Youtube, badala ya kwenye vyombo vya sheria.

Maneno ya Michuzi kwamba ni TISS imeibua hiyo video yanathibitisha ushiriki wa TISS kwenye mchezo huo mchafu, na kwamba Chadema kinajua kuwa Michuzi alishirikiana na watu wa usalama wa taifa katika kazi hiyo chafu. Software za video (editing) walizotumia zilitoka kwake. Fedha ya kuandaa hiyo video zilitoka usalama na Ikulu. Tunajua kuwa wale vijana wa Ada Estate na yule jamaa anayempelekea kigogo wa Jamii Forum, walilalamika sana kwa mmoja wa wamiliki wa JF.

Ndugu waandishi wa habari;

Chadema kinajua kuwa mmoja wa watuhumiwa hawa, Mwigulu Nchemba anafanya mipango na baadhi ya wafanyakazi wa kampuni ya Vodacom ili kumsaidia kufuta taarifa zake. Nachukua nafasi hii, kuionya kampuni hiyo kuacha kucheza mchezo huo kwa kuwa ni kinyume cha sheria za mamlaka ya mawasiliano (TCRA).

Tunahitaji mawasiliano haya kwa kuwa Mwigulu – zinaonyesha mtuhumiwa huyo akifanya mawasiliano mfululizo na Ludovick, yakiwamo yale ya tarehe 4 Machi 2013. Hii ilikuwa siku moja kabla ya Kibanda kutekwa.

Ndugu waandishi wa habari;

Hawa niliowataja ni watu muhimu sana katika upangaji wa mkakati wa utengenezaji wa video ya Lwakatare na vitendo vya kihalifu vya utekwaji wa Kibanda na tukio la kutekwa na kisha kutupwa msutuni kwa mwenyekiti wa Jumuiya ya madaktari nchini, Dr. Steven Ulimboka.

Kwa mfano, simu ya Mwigullu Nchemba, namba 0714 008888, 0756 008888 na 0757 946223, zimefanya mawasiliano mara kadhaa na Ludovick Joseph, Saumu K. Malungu, Jack Zoka, Ali Shaali na Ramadhani Ighondo. Mawasiliano hayo yalifanyika katika kipindi ambacho mgomo wa madaktari ulishamiri; baadaye yakarudi tena kati ya 26 Desemba mwaka jana na 15 Machi mwaka huu.

Miongoni mwa mawasiliano ambayo tunaona yanahusika na ujambazi huu, ni yale ya 28 Desemba, siku ambayo mkanda wa Lwakatare umerekodiwa; tarehe 4 hadi 6 Machi 2013, siku moja kabla ya Kibanda kutekwa na yale ya usiku wa manane (saa 8:17) wa 13 Machi 2013, ambako mchana uliofuata Lwakatare alikamatwa.

Huyu Mwagha ndiye aliyekuwa anatumika kuwasiliana na Saumu Malungu, ambaye tulimtaja kuwa ndiye aliyekuwa amepewa kazi na Mwigulu na usalama wa taifa, kurubuni vijana wetu kwa fedha ili kutoa ushahidi wa uongo juu ya video ya Lwakatare.

Vilevile, mawasiliano ya Mwiguluna Mwagha, katika kipindi hicho nayo tunayahitaji. Kwa sababu, huyu Mwagha anayetumia simu 0754006355, mbali na kuwasiliana na Mwigulu, ndiye aliyekuwa anawasiliana na mmoja wa waliomteka Ulimboka; na ndiye aliyewasiliana na Saumu kati ya 20Januari na Machi 6 mwaka huu.

Ndugu waandishi wa habari;

Ludovick alifanya mawasiliano ya mwisho na Joyece Agustine, ambaye anatumia simu Na. 0717 559210, mawasiliano ambayo yalifanyika saa 5:13 usiku. Hiyo ndiyo ilikuwa simu yake ya mwisho usiku huo; katika siku hiyo Ludovick aliwasilisna na Joyce mara tisa kuanzia saa 12: 54 asubuhi.

Kwa mujibu wa taarifa za kwenye mtandao wa Jamii Forum, ambako video ya Lwakatare ilitumwa, Ludovick alikamatwa Machi 15 mwaka huu. Hata hivyo, rekodi katika simu yake Na. 0715 927100 inaoyesha 17 Machi Ludovick alifanya mawasiliano na Joyce Augustino. Mawasiliano hayo yalifanyika saa 8: 9 usiku, wakati inadaiwa na polisi alishakamatwa.

Naye mhariri wa Mwananchi, Bw. Msaky ambaye anatajwa kutaka kutekwa na Ludovick na Lwakatare, amekuwa na mawasiliano kadhaa na Ludovick – mtu anayepanga kumteka. Ludovick na Msaky walifanya mawasiliano mfululizo kati 27 Desema 2012, siku moja kabla ya video ya Lwakatare haijarekodiwa na 7 Machi siku moja baada ya Kibanda kutekwa.

Msacky alitumia simu zake hizo mbili (0764 331010 na 0655 331010) kuwasiliana na Ludovick, huku Ludovick akitumia 0753927100. Mawasiliano ya 31 Desemba yalifanyika Ludovick akiwa Tegeta, jijini Dar es Salaam. Mawakala hawa wawili wa usalama wa taifa (Ludovick na Msaky), walikutana 31 Desemba 2012, katika hoteli ya Tamal, Mwenge jijini Dar es Salaam.

Ndugu waandishi wa habari;

Baada ya kupitia taarifa hizi za mawasiliano ya simu za Mwigulu Nchemba, Ludovick Joseph, Ramadhani Ighondo na Saumu Malungu tumegundua yafuatayo: Kwamba, Ramadhani Ighondo, amefanya mawasiliano mara nyingi na Mwigulu, Mwagha na Zoka; naye Mwagha amefanya mawasiliano na Mwigulu na Saumu; naye Saumu amefanya mawasiliano na Mwagha, Mwiguluna Shaali Ali, ambaye ni afisa usalama wa taifa.

Tumegundua vilevile, kuwapo mawasiliano kadhaa kati ya Ludovick na Msaky; Ludovick na Mwigulu; Msaky na Nchimbi; Msaki na Mwagha, Samu na Mwagha na Ramadhani Ighondo Abeid, anayetuhumiwa kumteka Dk. Ulimboka na Mwanga na Mwigullu.

Tumegundua pia kuwapo mawasiliano kati ya Ulimboka na Ramadhani; Zoka na Ighondo na Ridhiwani na Ighondo. Mawasiliano haya yalifanywa mfululizo usiku wa Juni 2012 siku ambayo Dk. Ulimboka alitekwa.

Tumepata kufahamu pia kwamba baadhi ya watu waliotajwa na gazeti la MwanaHALISI kuwa waliwasiliana na Ighondo usiku wa Juni 26, mwaka 2012, wamefanya mawasiliano pia na Mwigulu, Mwagha na Shaali Ali.

Ndugu waandishi wa habari;

Mwagha ni afisa usalama wa taifa anayefanyakazi makao makuu ya idara hiyo. Ndiye yule anayetumika kuendesha michezo ya kuhonga wanasiasa wa CCM na upinzani.Ni Mwagha anayepanga wabunge na kuwapanga waongee nini kwa maslahi ya CCM. Ushenzi wote anaoongea Mwighulu bungeni, hupewa na Mwagha kwa maelekezo ya Jack Zoka.

Naye Shaali ndiye aliyekutana na afisa wetu wa usalama, Ahmed Sabula na mwenzake, Machi 29 mwaka huu katika hoteli ya See Cliff jijini Dar es Salaam. Katika mkutano huo kati ya Sabula, kijana wetu wa usalama na afisa usalama wa serikali Bw. Shaali alitaka Sabula akubali kutumika kwa kutoa taarifa za vikao vya chama, kuwasilisha kwake nyaraka za kamati kuu na kueleza mipango ya chama katika kesi ya Lwakatare.

Kwenye mpango huu, afisa huyo wa usalama wa taifa ambaye ninamfahamu vizuri, alimuahidi Sabula kiasi cha Sh. milioni 30 na kwamba fedha hizo angelipwa wiki iliyopita. Aliahidiwa pia kwamba kila nyaraka atakayopeleka atalipwa ujira.

Aidha, Sabula aliahidiwa kulipwa shilingi 500,000 (laki tano) kila mwezi; afisa wetu huyu ameripoti tukio hilo kwa viongozi wake wa chama. Yule mwenzake aliandaliwa kuwa shahidi wa kesi ya Lwakatare; aliambiwa akikubali dili hiyo atalipwa kila mwezi Sh. 500, lakini akaombwa kuwa mvumilivu kwa kuwa atalazimika kupotea kwa miezi kama mitano hadi sita.

Ndugu waandishi wa habari;

Kitendo cha Mwigulu kuwasiliana Ramadhani Ighondo, Mwigulu kuwasiliana na Ludovick, Saumu kuwasiliana na Mwigulu, Ighondo kuwasiliana na Ulimboka, Zoka kuwasiliana na Ighondo, tena katika muda uleule ambao Ighondo amewasiliana na Ulimboka na Saumu kuwasiliana na Mwagha, ni uthibitisho tosha kwamba usalama wa taifa wako nyuma ya mipango hii ya michafu ya kupanga utekaji na kisha kutaka kukichafua Chadema.

Aidha, kitendo cha Ludovick kuwasiliana Msaky; Ighondo kuwasiliana na Mwagha, Ridhiwani Kikwete kuwasiliana na Ighondo, tena kila baada ya Ighondo kuwasiliana na Ulimboka na Jack Zoka, ni uthibitisho mwingine kuwa genge hili la wahalifu linashirkiana na baadhi ya watu kutaka kuangamiza taifa.

Ni uthibitisho tosha kwamba hawa ndiyo wanaowahonga wanachama wa Chadema na watu wengine ili watoe ushahidi feki dhidi ya Lwakatare, na kwamba ni usalama wa taifa walioandaa ile video uchwara inayopigiwa chapuo na Mwigulu.

Ndugu waandishi wa habari;

Chama Cha Mapinduzi kinajua kwa hali ya sasa hakiwezi kushinda uchaguzi wa mwaka 2015 huku Chadema ikiwa katika hali nzuri ya kisiasa tunayoiona sasa. Wanajua kabisa CCM imegawanyika, kundi lolote litakalopita ndani ya CCM, litahujumu kundi jingine. Ni kama ilivyotokea uchaguzi mdogo wa Arumeru Mashariki.

Ndiyo maana wanapanga kila mbinu kutaka kuiangamiza Chadema. Nasi tunasema katu hatutakubali kuona Chadema kinakufa. Tutapambana usiku na mchana. Juna na mvua. Hadi tushinde hila hizi.Tunawaambia wanachama wetu na wale wanaotuunga mkono, Chadema ni chama kikubwa. Kina mtandao kila mahali, kuanzia Ikulu hadi polisi; na hivyo hakitakufa au kuzorota kwa mambo ya kupikwa.

Ni imani yangu kwamba amri ya mahakama itawafichua wote hawa ni kuirudisha Tanzania katika amani yake. Ni lazima tufikike mahala watu hawa wafahamike mbele ya umma, tunataka wafahamu kuwa maisha ya mwanadamu yana thamani kuliko siasa chafu na ufisadi wanaouendeleza.

Nawashukuru kwa kunisikiliza.

Mabere Marando,

Dar es Salaam

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...