Thursday, December 18, 2014

Kitabu Sasa Kinapatikana Katika "Kindle"

Baada ya kujaribu jaribu, jana nimefanikiwa kukichapisha kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differeces katika "Kindle." Yeyote, sehemu mbali mbali za dunia, mwenye kifaa cha kuingizia na kusomea vitabu pepe anaweza kukipata mtandaoni, kwenye duka la Amazon Kindle.

Kwa miezi mingi nilikuwa nawazia kukiweka kitabu hicho katika Kindle, lakini sikujituma vya kutosha na kufanya kazi hiyo. Wiki hii, nilipania kuitekeleza, na nimefanikiwa. Katika kuhangaika kwangu, nimejifunza mambo ya ziada kuhusu tekinolojia hii, ambayo nilianza kujifunza kwa vitendo wakati nilipochapisha kitabu hiki hiki katika lulu.com.

Kuna sababu zilizonifanya niingie huko Kindle. Kwanza, ninafahamu kuwa kadiri tekinolojia inavyosonga mbele na kuenea, shughuli nyingi zinahamia mtandaoni, kuanzia elimu, biashara na mawasiliano ya aina mbali mbali. Nami najaribu kwenda na wakati.

Vile vile, ninalikumbuka tukio lililonitokea siku moja katika tamasha la vitabu la Twin Cities, mjini St. Paul, Minnesota. Kati ya watu waliofika kwenye meza yangu, alikuwepo bwana mmoja ambaye aliniuliza kama hiki kitabu cha Africans and Americans; Embracing Cultural Differences kinapatikana katika "Kindle." Nilipomwambia hakipatikani, alijibu kuwa yeye ni mtu anayesafiri mara kwa mara kwa ndege, na hataki udhia wa kubeba mzigo wa vitabu safarini. Anatumia vitabu pepe.

Kauli yake hii ilinigusa na kunifanya nijisikie vibaya. Tangu siku ile, kauli ile imekuwa changamoto kwangu, ikinikumbusha umuhimu wa kuwatimizia mahitaji wateja wa aina yake. Sasa, kwa kukichapisha kitabu katika Kindle, ninajisikia kama nimetua mzigo uliokuwa unanielemea moyoni.

Hata hivyo, Kindle sio mahali pekee mtandaoni ambapo huchapishwa vitabu pepe. Kwa mfano, kama nilivyogusia hapa juu, kitabu hiki hiki cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences nilikichapisha kwanza kule lulu.com. Kuna sehemu zingine pia, ambako mwandishi anaweza kuchapisha kitabu chake na wateja wakakipata huko. Kadiri siku zinavyopita, fursa zinaendelea kuongezeka.

Kwa kumalizia, napenda kusema kuwa mara kadhaa nimewahi kuelezea suala hili la kuchapisha vitabu mtandaoni. Mfano ni makala hii hapa na hii hapa. Vile vile, katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii, nimeelezea suala hilo (kurasa 27-29), ili kuwagawia wengine yale ninayoyajua na ninayoendelea kujifunza. Ni jambo la kutia moyo kuwa kuna wa-Tanzania wenzangu ambao wanayasikiliza mawazo yangu, kama inavyodhihirika katika makala ya Ibrahim Yamola hii hapa.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...