Wednesday, June 8, 2016

Nimempigia Simu Mzee Patrick Hemingway

Leo, saa 12.52 jioni, nimempigia simu Mzee Patrick Hemingway, kumwarifu kuwa nimeshawasiliana na wahusika wa maktaba ya J.F. Kennedy kuhusu safari yangu ya kwenda kufanya utafiti. Nimemwambia kuwa nimepata majibu kutoka kwa wahusika sehemu zote mbili za hifadhi ya Hemingway.  Wote wameniletea maelezo ya taratibu za kufuata nitakapofika katika maktaba ile.

Nimemwambia kuwa nimefurahishwa na ukaribisho wao, na nimemshukuru kwa kunitia moyo katika azma yangu ya kwenda kwenye maktaba ile. Nimemwambia kuwa nimesoma taarifa ya yaliyomo katika maktaba ile, nikizingatia yanayohusiana na utafiti wangu, ambao ni juu ya Hemingway na Afrika.

Nimemkumbusha alivyoniambia kuhusu simba aliyehifadhiwa katika maktaba ya J.F. Kennedy, na kuwa ninangojea kwa hamu kumwona simba huyu ambaye amesimuliwa na Hemingway katika Under Kilimanjaro kama "Mary's lion." Mzee Patrick ameniambia kuwa simba huyu aliye maoneshoni si yule wa Mary, bali aliuawa na Clara Spiegel, na kwamba Sara Spiegel anaonekana katika picha mojawapo iliyomo katika kitabu cha Mary Hemingway, How It Was, picha ambamo naye yumo. Nimemwambia kuwa ninacho kitabu hiki, ila nimejifunza jambo jipya, kwani nilidhani ni simba wa Mary.

Nilivyomwambia kuwa ninapangia kuangalia zaidi miswada na nyaraka zinazohusiana na maandishi ya Ernest Hemingway kama Green Hills of Africa, Under Kilimanjaro, "Snows of Kilimanjaro," na "The Short Happy Life of Francis Macomber," Mzee Patrick alikumbushia chimbuko la hadithi hiyo, akamtaja John Patterson, na kisha akaongelea simba wa Tsavo ambao wamehifadhiwa Chicago katika Field Museum of Natural History.

Aliendelea kunielezea kuwa kuna mtaa mjini Tel Aviv ambao unaitwa Patterson, kwa heshima yake, kwani alikuwa ameshiriki vita kwenye eneo la mashariki mwa Mediteranean na kujipatia heshima katika nchi ya Israel. Mzee Patrick ameniambia pia kuwa Patterson alikuja kuishi California. Hayo ni mambo ambayo sikuwa ninayajua, lakini sasa ninayafuatilia. Inashangaza jinsi Mzee Patrick Hemingway alivyo na kumbukumbu, ingawa umri wake sasa ni miaka 88.

Tuligusia pia namna Ernest Hemingway alivyoanza kuvutiwa na Afrika. Mzee Patrick alianza kwa kusema kuwa Hemingway alisoma riwaya juu ya Afrika wakati alipokuwa kijana Paris. Hapo nilitaja jina la kitabu na mwandishi, yaani Batouala na mwandishi, yaani Rene Maran, tukaongelea mapitio ya Hemingway ya kitabu hiki, yaliyochapishwa mwaka 1922, na jinsi mtindo wa uandishi wa Maran ulivyochangia uandishi wa Ernest Hemingway mwenyewe.

Tulimaliza mazungumzo akinitakia safari njema, akaahidi kuwapigia simu wahusika wa maktaba ya J.F. Kennedy kuhusu ujio wangu, akasema pia niwasiliane naye kumweleza kuhusu ziara yangu. Mazungumzo yetu yalikuwa ya dakika kumi na mbili tu. Kama ilivyo kawaida yangu, nimeona niandike kumbukumbu hizi.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...