Saturday, June 18, 2016

Nimepitia Tena Duka la Half Price Books

Leo nilimpeleka profesa mwenzangu Mall of America na halafu St. Paul ambako atakaa siku kadhaa. Wakati wa kurudi, niliamua kupita mjini Apple Valley kwa lengo la kuingia katika duka la vitabu la Half Price Books ambalo nimekuwa nikilitaja katika blogu hii. Ingawa lengo langu lilikuwa kuona vitabu vya aina mbali mbali, hamu yangu zaidi ilikuwa kuona kama kuna vitabu juu ya Ernest Hemingway ambavyo sijaviona kabla.

Niliangalia sehemu vinapowekwa, nikaviona vitabu ambavyo ninavifahamu. Lakini, kuna kimoja ambacho sikuwa ninakifahamu, Paris Without End: The True Story of Hemingway's First Wife. kilichotungwa na Gioia Diliberto. Ninafahamu kiasi habari za huyu mke, ambaye jina lake ni Hadley, na nilimtaja siku chache zilizopita katika blogu hii. Niliwazia kukinunua, lakini badala yake niliamua kununua kitabu cha By-Line cha Ernest Hemingway, ingawa nilishanunua nakala miaka kadhaa iliyopita, bali niliiacha Dar es Salaam mwaka 2013.

By-Line ni mkusanyo wa makala alizochapisha Hemingway katika magazeti na majarida miaka ya 1920-1956. Baadhi ya makala zilizomo zilinigusa kwa namna ya pekee nilipozisoma kwa mara ya kwanza, miaka kadhaa iliyopita. Mifano ni insha iitwayo "The Christmas Gift" na barua ziitwazo "Three Tanganyika Letters." Sikuwa na hela za kutosha, nikanunua hiki kimoja.

Mtu mwingine anaweza kuhoji mantiki ya kununua nakala ya kitabu ambacho tayari ninacho, lakini kwangu hii si ajabu. Nakala iliyoko Dar es Salaam ina jalada jepesi, niliyonunua leo ina jalada gumu. Hiyo kwangu ni sababu tosha. Jambo la zaidi ni kuwa kuna vitabu ambavyo napenda niwe navyo mwenyewe nilipo, hata kama ningeweza kuviazima maktabani. Hii si ajabu, kwani kila binadamu ana mambo yake anayoyapenda na yuko tayari kuyagharamia.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...