Monday, October 24, 2016

Ninarekebisha Kitabu Nilichochapisha Mtandaoni

Mara kwa mara, ninaongelea suala la kuchapisha vitabu mtandaoni, kutokana na uzoefu wangu. Ninatarajia kuwapa wengine uzoefu wangu wa kutumia tekinolojia za uchapishaji mtandaoni, ambazo zinatoa fursa tele kwa yeyote kujikomboa na taabu na vikwazo vya uchapishaji wa jadi.

Faida mojawapo ya uchapishaji wa aina ninayotumia kuchapishia vitabu vyangu ni fursa isiyo na mipaka ya kurekebisha kitabu chako wakati wowote uonapo dosari ndani yake au fursa ya kukiboresha. Hilo linawezekana kwa kuwa mswada wako unakuwa umehifadhiwa kama faili la kielektroniki mtandaoni, hata kama hukuuhifadhi katika kompyuta, disketi, au kifaa kingine.

Mimi ninatumia mtandao wa lulu.com. Hapo, ukishachapisha kitabu, nakala ya mswada inahifadhiwa hapo hapo mtandaoni. Unapotaka kurekebisha kitabu chako, unachofanya ni kuuingiza "(down-loading") mswada katika "flash drive" na kuufanyia marekebisho. Kisha unaurudisha ("up-loading") sehemu ya kuchapishia. Yeyote atakayekinunua baada ya hapo atakuwa ananunua kitabu kilichoboreshwa.

Hatua zote hizi zinafanyika bila mtu yeyote kutambua kinachotokea, bali wewe mhusika tu. Na wakati wote, unaporekebisha mswada, kitabu hakitoweki hapo mtandaoni. Kinakuwa kama kilivyokuwa mwanzo, na yeyote anaweza kukinunua, wakati wewe unaendelea na marekebisho. Unapomaliza marekebisho na kukiingiza tena mtandaoni ("up-loading"), ndipo kitabu kilichoboreshwa kinachukua nafasi ya kile cha awali.

Sasa hivi, niko katika kurekebisha kitabu changu, Notes on Okot p'Bitek's Song of Lawino. Hakuna anayetambua kuwa kinafanyiwa marekebisho, kwani kinaonekana hapo mtandaoni kama kawaida. Nitakapomaliza marekebisho na kukichapisha tena, itakuwa kama vile hakuna lililotokea.

Urahisi huu wa kurekebisha kitabu hauko katika uchapishaji wa jadi, ambapo inabidi kungoja hadi wakati wa kutoa toleo jipya la kitabu. Aghalabu, wachapishaji huwa hawana uwezo wa kifedha wa kutoa toleo jipya. Nakala zikiisha, huwa ndio mwisho wa kuchapishwa kitabu.

Lakini tatizo hili haliko katika uchapishaji wa mtandaoni kama huu ninaotumia. Kitabu hakiwezi kutoweka, yaani kuwa "out of print," labda mtu uamue kukiondoa wewe mwenyewe hapo mtandaoni. Ukibadili mawazo ukataka kukirudisha tena ulimwenguni, ni hiari yako kufanya hivyo, wakati wowote. 

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...