Showing posts with label The Power of Positive Thinking. Show all posts
Showing posts with label The Power of Positive Thinking. Show all posts

Friday, May 16, 2014

Vitabu Vya Kutuendeleza Kimaisha

Katika ujumbe wangu wa jana, kuhusu nia yangu ya kuandika kitabu kingine kufuatia kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, nilisisitiza umuhimu wa kujiamini. Hilo ni fundisho linalotolewa katika vitabu vingi, labda niseme vyote, vinavyojadili suala la maendeleo ya mtu binafsi, kumweka katika hali ya kufanikiwa.

Pamoja na kujiamini, mtu unapaswa kuangalia uwezo wako na kuutumia, badala ya kukaa na kulalamika kuwa huna hiki au kile, au kuwasikiliza watu wanaojaribu kukukwamisha au kukukatisha tamaa. Hakuna sababu ya kuwa na watu kama hao, bali ambatana na watu wanaosonga mbele na wana mtazamo wa kusonga mmbele.

Jana hiyo, nilitaja kitabu kimojawapo ambacho ni maarufu, kiitwacho The Power of Positive Thinking. Sijui ni wa-Tanzania wangapi wanakifahamu kitabu hiki, wamekisoma, au wanakisoma. Kama wapo, watakuwa ni wachache sana, kama vile kijana Meshack Maganga wa Iringa, ambaye habari zake naziona kwenye mitandao kama Facebook.

 Kwanza, kuna suala la lugha. Wa-Tanzania wamepuuzia ki-Ingereza, kwa visingizio mbalimbali. Kwa hivi, ni lazima elimu iliyomo katika vitabu hivi inawapitia mbali; wanabaki gizani, wakiwa na fikra na mitazamo ya kuwakwamisha. Pili, kwa ujumla, wa-Tanzania hawana utamaduni wa kununua na kusoma vitabu. Hilo ni janga la Taifa.

Kwa miaka kadhaa nilikuwa nimekisikia kitabu cha The Power of Positive Thinking. Nimesoma baadhi ya vitabu vya aina hiyo, lakini sio hicho. Hivi karibuni, nilipolazwa kwa wiki sita katika hospitali ya Abbott Northwestern ya mjini Minneapolis, nilikwenda na nakala yangu ya kitabu hiki, nikawa najikongoja kukisoma kidogo kidogo, kutokana na hali ya kuumwa na kuwa kitandani siku zote.

Baada ya kuja kupumzika nyumbani, ingawa naendelea na matibabu, nimemaliza kukisoma kitabu hiki. Kina mafundisho mengi na ushauri wa thamani. Jambo moja ambalo limenikaa sawa sawa akilini ni kuwa fikra na mtazamo ulio nao, ndio msingi wa kufanikiwa au kutofanikiwa. Ukiwa na fikra za kutojiamini, au fikra kwamba hiki au kile huwezi, basi hutaweza. Utabaki hivi hivi ulivyo.

Fikra na mtazamo ndizo zinakuongoza au kukukwamisha maishani. Kama huna mafanikio, ni wewe mwenyewe unasababisha hali hiyo. Tukirudi Tanzania, tunaona matatizo makubwa. Wengi hawajiamini; hawaelewi kuwa kufanikiwa au kutofanikiwa ni juu yao, badala yake wanakuja na visingizio au wanatafuta wachawi.. Utawaona wanaenda kwa waganga wa kienyeji, kwa mfano. Au utawasikia wakitafuta wa kumlaumu, kama vile wa-Islamu wengi wa Tanzania wanavyoaminishwa kwamba tatizo ni "Mfumo Kristo."

Basi, napenda kusisitiza kuwa ni muhimu tujibidishe kusoma vitabu mbali mbali vinavyotufungua macho na akili ili tuwe watu wa kujiamini, kutambua uwezo wetu na neema tulizojaliwa; tuzitumie juhudi yote ili tufanikiwe. Ndio maana katika ujumbe wangu wa jana, nilielezea kwa kujiamini azma yangu ya kuandika kitabu kingine kufuatia kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Nilitamka bila kusita kuwa hiki kitakuwa kitabu bora kabisa, kuliko hiki kingine, ingawa ni maarufu miongoni mwa wasomaji.

Thursday, May 15, 2014

Kitabu Kingine Kufuatia "Africans and Americans: Embracing Cultural Differences"

Ni yapata miaka tisa sasa tangu nichapishe kijitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences
Kadiri siku zinavyopita, wazo la kuandika kitabu kingine cha aina ile linazidi kuimarika akilini mwangu.

Tangu pale nilipochapisha Africans and Americans, nilifahamu kuwa sijaongelea masuala yote ambayo ningependa au ningeweza kuongelea. Sikupenda kuandika kitabu kikubwa; ilinibidi nifanye uchaguzi wa mada na kuandika kitabu kidogo.

Wazo la kuandika kitabu hiki cha pili nimekuwa nalo kwa miaka mingi. Kuna wasomaji wa Africans and Americans ambao, tangu mwanzo, walinishauri niandike kingine, ili kuongelea masuala ambayo sikuwa nimeyaongelea. Nami niliafiki wazo hilo.

Vile vile, kwa miaka yapata saba hivi nimeandika sura ambazo zitakuwemo katika hiki kitabu kipya. Ingawa Africans and Americans kimejipatia sifa tele miongoni mwa wasomaji, nilipania kuwa kitabu hiki kinachofuata kiwe bora  zaidi.

Uwezo wa kuandika kitabu bora zaidi ninao.Mungu akinijalia uzima, nitakamilisha kazi hiyo. Sio kazi ya wiki chache, au miezi michache. Nahisi itachukua miaka, ingawa, kama nilivyosema, sura kadhaa nilishaandika. Nataka kutumia uwezo wangu wa lugha kwa ufanisi kuliko ambavyo nimefanya kabla. Kitabu hiki kitakuwa kimeandikwa kwa ki-Ingereza kizuri sana, mfano wa kuigwa. Uwezo wa kuandika hivyo ninao, bora tu niwe na muda wa kutosha. Kama Ernest Hemingway alivyotufundisha, uandishi bora ni kazi ngumu inayohitaji muda sana.

Halafu, sina haraka, tofauti na mazingira ambamo niliandika Africans and Americans. Niliandika kitabu kile kwa kusukumwa na maprofesa tuliokuwa katika bodi ya uongozi wa Associated Colleges of the Midwest, ambao ni jumuia ya vyuo kumi na nne maeneo haya ya katikatika ya Marekani (USA. Kwa kutambua changamoto za kuwaelimisha wanafunzi wanaoenda kusoma Afrika kuhusu tofauti za utamaduni, na kwa kutambua kuwa hapakuwa na kitabu cha mwongozo cha kufaa kwa shughuli hiyo, waliniomba na kunishinikiza niandike. Nami nilifanya hivyo, ili kuhitimisha andiko hilo kwa muda mfupi, lianze kutumika.

Ninaongea hivi kwa sababu nataka kuwashauri wengine umuhimu wa kujiamini. Vitabu mbali mbali ambavyo nimekuwa nikisoma kuhusu maendeleo na mafanikio binafsi vinasisisitza umuhimu wa kujiamini, sio kuangalia zaidi vipingamizi, na matatizo, bali uwezo na fursa. Kitabu kimojawapo ambacho ningeshauri kila mtu asome ni The Power of Positive Thinking, kilichoandikwa na Norman Vincent Peale (New York: Simon and Schuster, 2011) kikachapishwa  mara ya kwanza mwaka 1952.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...