Monday, December 2, 2013

Ninayo Pia Blogu ya Ki-Ingereza, Jamani

Wadau wa blogu hii ya hapakwetu, samahani kama sikuweka wazi tangu mwanzo kuwa ninayo pia blogu ya ki-Ingereza. Inaitwa "Mbele" na anwani yake ni hii: http://www.josephmbele.blogspot.com.

Niliamua kuanzisha na kuendesha blogu hii ya ki-Kiingereza ili kuchangia elimu hasa katika masuala ya fasihi ya ki-Ingereza. Mimi ni mwalimu wa somo hili mwenye uzoefu tangu miaka ya mwanzoni ya sabini na kitu. Nilifundisha katika idara ya Literature, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kuanzia mwaka 1976, nikasomea shahada ya udaktari Chuo Kikuu cha Wisconsin-Madison, Marekani, 1980-86, na kuanzia mwaka 1991 nimekuwa nikifundisha katika idara ya ki-Ingereza ya chuo cha St. Olaf hapa Marekani.

Katika blogu hii ya "Mbele" mara kwa mara ninaongelea vitabu, hasa vitabu vya fasihi. Uchambuzi wangu vitabu hivi unasomwa duniani kote. Nimeona kuwa uchambuzi wangu wa riwaya ya The Old Man and the Medal unapitiwa kuliko andiko jingine lolote na watu kutoka duniani kota.

Nina uzoefu na ufahamu mkubwa sana katika masomo hayo, na ndio nikaona niwamegee wanajamii angalau kiasi, kwani blogu si mahala pa kuandika makala ndefu, wala kitabu. Nilivyoanzisha blogu hii ya ki-Ingereza niliwawazia kwa namna ya pekee vijana wa Tanzania.

Nikiongea kwa ujumla kuhusu wa-Tanzania, ni kwamba wale wanaodhani wanajua ki-Ingereza, bado wana safari ndefu. Mimi mwenyewe naendelea kujifunza undani wa ki-Ingereza, ingawa waandishi maarufu hapa Marekani kama vile Mzee Patrick Hemingway na Jim Heynen wanapenda ninavyoandika. Ni jambo baya sana kuridhika na kile unachodhani unajua, na ndio maana nafanya juhudi.

Ninaandika ki-Ingereza sahihi, ipasavyo, na nilitegemea kuwa yoyote anayeisoma blogu ya Mbele kwa makini ataona mfano wa uandishi bora wa ki-Ingereza. Ninafahamu ninachosema, kwani kama nilivyotamka, mimi nafundisha ki-Ingereza katika chuo hapa Marekani. Lakini bado nahangaika kuboresha ujuzi wangu kwa kusoma sana na kuandika sana.

Nimeandika ujumbe huu kwa sababu mbili zinazohusiana. Hutokea mara moja moja mdau akaniuliza blogu yangu nyingine anwani yake ni ipi. Pili, nimegundua kuwa kuitaja tu katika orodha ya blogu niliyoweka hapa kulia, haitoshi. Soma pia makala hii hapa.

Wednesday, November 13, 2013

Kitabu Kinapendwa

Tangu nichapishe vitabu vyangu mtandaoni, ninaweza kufuatilia mauzo kila siku. Nimefungua duka mtandaoni, na nimetoa ushauri kwa waandishi wengine, hasa wa-Tanzania, kuhusu uzuri na ubora wa tekinolojia hii.

Ushauri wangu nimeutoa katika kitabu kiitwacho CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Lakini inaeleweka kuwa ukiwa na wazo ukaliweka kitabuni, usitegemee kama wa-Tanzania wataliona. Huu ni ukweli ambao umesemwa tena na tena. Nami sidhani kama nina la kuongeza. Papo hapo, falsafa yangu ni kuwa ukiwa na jambo la manufaa, waeleze wengine.

Kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences ndicho chenye mauzo kuliko vingine vyote. Kila ninapoona kimenunuliwa, najiuliza ni nani huyu aliyenunua. Pengine inakuwa ni nakala moja, lakini pengine ni nakala za kutosheleza darasa. Nami sijui ni nani kaagiza. Hiki kitendawili kinanifanya niwe na dukuduku, na nafahamu kuwa sitapata jawabu.

Kuna wakati zinapita siku nyingi kidogo bila mtu kukinunua, lakini wakati mwingine hali hubadilika ghafla. Kwa mfano, Oktoba 31, niliona mtu kanunua nakala 51. Laiti ningemfahamu. Ningempelekea barua ya shukrani na pia nakala ya bure kama kifuta jasho. Lakini simjui. Ni kitendawili.

Namshukuru Mungu kwa jinsi alivyoniwezesha kuandika na kuwagusa walimwengu kiasi hicho. Yote ni uwezo wake.


Saturday, November 9, 2013

Nimenunua "Nomad," Kitabu cha Ayaan Hirsi Ali

Miaka kadhaa iliyopita, nilianza kusikia jina la Ayaan Hirsi Ali, mwandishi kutoka Somalia, ambaye alikuwa ameikimbia nchi yake na alikuwa anaishi Uholandi, ambako alifanikiwa hata kuwa mbunge. Ilionekana ni mwandishi mkorofi, kwa maana ya kwamba wengi walikerwa na kukasirishwa alivyokuwa anahoji utamaduni wa wa-Somali na u-Islam, hasa kuhusu masuala ya haki za wanawake.

Nilisoma kuhusu kitabu chake Infidel, ambacho kilisemekana kiliwakasirisha wa-Islam wengi. Nilikuwa na dukuduku ya kusoma maandishi yake, lakini, kutokana na majukumu mengi, sikufuatilia.

Hata hivi, nimezingatia ukweli kuwa, kuliko kutegemea ya kuambiwa, muhimu mtu kujisomea mwenyewe. Leo nimenunua kitabu cha Ayaan Hirsi Ali kiitwacho Nomad. Ingawa ninasoma vitu vingi kila siku, nitakipa kitabu hiki kipaumbele. Wakati huo huo, nitanunua vitabu vyake vingine. Insh'Allah, nitapata wasaa wa kuelezea nawazo yake.

Tuesday, October 29, 2013

Nimepata Wageni Leo

Leo nimepata bahati ya kutembelewa na wageni wawili. Mmoja ni Mchungaji John Mhekwa kutoka Tungamalenga, Iringa. Mwingine ni Profesa Paula Swiggum wa chuo cha Gustavus Adolphus, St. Peter, Minnesota.

Mchungaji Mhekwa hatukuwa tunafahamiana, lakini Profesa Swiggum tumefahamiana kwa miaka kadhaa, kwani katika programu yake ya kupeleka wanafunzi Tanzania, alinialika kuongea nao kuhusu masuala ya tofauti za tamaduni, kama maandalizi ya safari.

Wanafunzi walikuwa wanasoma kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Huo ulikuwa ni uamuzi wake. Mazungumzo yangu na hao wanafunzi yalihusu mambo niliyoandika katika kitabu hiki. Baada ya Profesa Swiggum kustaafu, profesa aliyemrithi, katika kuendesha programu hiyo, Barbara Zust, aliendelea na utaratibu huo.

Kifupi ni kwamba Profesa Swiggum tumeanza zamani kiasi kushirikiana katika nyanja hizo. Leo ilikuwa fursa ya pekee ya kufahamiana na huyu mgeni mwingine, Mchungaji Mhekwa. Nimemwambia kuwa Tungamalenga nilipita, mwezi Agosti mwaka 2011, nikiwa na wanafunzi tukiwa tunaelekea hifadhi ya Ruaha.

Sunday, October 13, 2013

Tamasha la Vitabu Twin Cities, Oktoba 12, Lilifana

Tamasha la vitabu, Twin Cities Book Festival, lililofanyika mjini St. Paul, Minnesota, jana, tarehe 12, lilienda vizuri. Niliondoka mapema asubuhi, yapata saa mbili, nikafika kwenye maaonesho saa tatu. Sikuwa nimechelewa, kwani wakati naandaa vitabu vyangu kwenye meza yangu, wengine nao walikuwa wakiandaaa, ingawa wengi walishapanga vitabu vyangu siku iliyotangulia
Meza niliyopata, baada ya kulipia dola 80, ilikuwa namba 12. Nilikuwa nimejisajili kwa jina la Africonexion, ambayo kampuni yangu ndogo inayohusika na uchapishaji na uuzaji wa vitabu vyangu, na pia kuratibu mihadhara yangu ya kuchangia maelewano baina ya watu wa tamaduni mbali mbali. Tangu nilipoisajili kampuni hii, shughuli zake zimekuwa zikifanyika zaidi hapa Marekani, lakini hatimaye, hasa nitakaporejea Tanzania baada ya kustaafu hapa Marekani, nataka kuijenga kampuni hii Tanzania, Africa Mashariki, na sehemu zingine.







 




Kama kawaida, watu walianza kuingia ukumbini tangu milango ilipofunguliwa. Ukiwaangalia wanavyojishughulisha kuangalia vitabu kwenye meza mbali mbali, unaona kabisa kuwa hao ni watu wanaothamini elimu. Kwa vigezo vyangu, hao ni watu walioelimika.











Inavutia kuona jinsi watu wanavyoacha shughuli zao nyingine ili kuja kwenye tamasha la vitabu. Ingekuwa ni Tanzania, watu hawangehudhuria. Hilo nimeshuhudia tena na tena, na nami, na wengine wengi, tumeandika sana kuhusu suala hilo. Kadiri miaka inavyopita, Tanzania inazidi kuwa taifa la wajinga. Hakuna sababu ya kubembelezana; ukweli lazima usemwe.









Ushahidi wa kuelimika ni kuwa na kiu isiyoisha ya kujifunza mambo. Ni dukuduku ya kutaka kujua, ambayo kwa ki-Ingereza huitwa "intellectual curiosity." Mtu asiye na "intellectual curiosity" hajaelimika, kwa sababu kuridhika na kile ambacho unadhani unajua, ambacho kwa kweli ni kidogo, ni ujinga. Ni wajibu wangu kama mwalimu kupambana na tabia za aina hiyo, bila kumwonea aibu mtu yeyote.








Kama kawaida, ushiriki wangu katika tamasha la Twin Cities Book Festival ulikuwa na mafanikio mazuri. Nilionana na kuzungumza na watu wengi waliofika kwenye meza yangu. Niliuza vitabu kadhaa. Niliitangaza kampuni ya Africonexion kwa kuwagawia watu chapisho la ukurasa moja ambalo linaelezea shughuli zake, na pia niliwapa kadi ya biashara ya Africonexion.

Binti yangu Zawadi alifika baadaye kunisaidia kwenye meza yangu, nami nikapata fursa ya kutembelea meza za wachapishaji na waandishi wengine. Nilielimika sana kwa kuongea na watu mbali mbali, kujionea shughuli za uchapishaji na maelfu ya vitabu vilivyokuwepo kwenye maonesho. Nilipata fursa ya kuwaelimisha wengine, kama mwalimu, mwandishi na mshauri katika masuala ya tofauti za tamaduni na athari zake.

Tuesday, October 8, 2013

Vijana Washikwa Mtwara Wakiwa Katika Mafunzo ya Al Shabaab na Al Qaida

1 
Stori ambayo ilishika namba 1 kwenye habari 10 za AMPLIFAYA ya Clouds FM October 7 2013 ni hii ya Polisi Mtwara kukamata vijana 11 ambao walikua wakifanya mazoezi ya kijeshi waliyokua wakijifunza kutoka kwenye cd za magaidi zilizokua na mafunzo kutoka kwa makundi ya Al Shabaab na Al Qaeda.
Taarifa zaidi unaweza kuzisoma hapo chini kwenye hiyo taarifa iliyotolewa na jeshi la polisi.
2 3

4 5 6


CHANZO: dj sek

0 comments:


Post a Comment

Tamasha Kubwa la Vitabu, Twin Cities, Oktoba 12

Lile tamasha maarufu kabisa la vitabu ambalo limefanyika mjini Minneapolis kwa miaka mingi, mara moja kwa mwaka, limekaribia kabisa. Kuanzia mwaka jana, tamasha limehamia mjii St. Paul, kwenye viwanja vya State Fairgrounds.

Hakuna tamasha kubwa zaidi ya hili katika eneo hili la Minnesota na majimbo ya jirani. Wanahudhuria watu yapata 7,000, wapenzi wa vitabu. Wanakuwepo waandishi, wachapishaji, wahariri, wachora picha za vitabuni, wahakiki, wauzaji wa vitabu na majarida. Wanahudhuria wazee, watu wazima, vijana, na watoto.

Nimeshiriki tamasha hili kwa miaka mingi, kama mwandishi wa vitabu na mwelimishaji katika chuo kikuu na jamii. Kila mara nimepata fursa ya kuongea na wasomaji wa maandishi yangu na watu ambao sijawahi kuwafahamu kabla. Wanakuja na maoni, taarifa, na uzoefu mbali mbali. Tunabadilishana mawazo. Inakuwa ni kama shule muhimu sana. Tamasha linapoisha, jioni, najiona nimeelimika sana.

Namshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuandika vitabu na maandishi mengine. Namshukuru kwa namna ya pekee kwa kuniwezesha kuandika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho najua kimesomwa na bado kinasomwa na maelfu ya watu hapa Marekani, ambao huguswa na mawazo na ushauri niliotoa katika kitabu hiki.

Kwenye kila tamasha, ambamo kunakuweko vitabu maelfu kwa maelfu, unawajibika kushangaa wadau wanafikiaje uamuzi wa kununua kitabu fulani au vitabu fulani. Nina bahati kuwa kitabu changu, ingawa kimekuwepo sokoni kwa miaka mingi kiasi, hakijachujuka bali kinawavutia wateja. Ninachoweza kusema ni kimoja, kwamba yote ni mipango ya Mungu.

Baadhi ya watu ninaokutana nao ni waandishi chipukizi. Huniulizia namna ya kuchapisha kitabu. Nami huwahamasisha kufuatilia hali ya uchapishaji wa leo, unaotumia tekinolojia tofauti na zile tulizozizoea. Kwa taarifa, na kwa manufaa ya watu wanaoongea ki-Swahili, nimetoa maelezo na uzoefu wangu kuhusu uchapishaji huo na mikakati mingine inayohusika, katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii.

Nimeshajiandaa vizuri kwa tamasha la tarehe 12. Nakala za vitabu vyangu ninazo, pamoja na matangazo na machapisho mengine. Nangojea kwa hamu kukutana na kuongea na watu wengi. Kwa namna ya pekee, nangojea kuongea na watoto. Insh'Allah, nitaandika ripoti ya tamasha, kama ilivyo jadi yangu. Kwenye tamasha hili, nimejisajili kwa jina la kampuni yangu ndogo iitwayo Africonexion: Cultural Consultants, ambayo nimekuwa nikijitahidi kuitambulisha Tanzania. Unaweza kuona jina hilo katika orodha ya wauza vitabu, ambayo hi hii hapa.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...