Tuesday, May 4, 2010

Utalijua Jiji

Tangu kuanza kwa miji katika historia, wanadamu wamekuwa na hisia na fikra kuhusu miji na maisha ya mijini. Wametofautisha maisha ya mjini na maisha ya shamba, kama inavyojulikana. Kwa ujumla miji inachukuliwa kuwa sehemu ya maendeleo na usasa, na shamba ni sehemu iliyo nyuma au iliyolala usingizi.

Mitazamo hii imeelezwa vizuri katika semi mbali mbali, hata katika utamaduni wetu. Kwa mfano, kuna usemi kuwa jogoo la shamba haliwiki mjini. Nakumbuka pia wimbo mmoja wa Mbaraka Mwishehe, mwanamuziki maarufu wa Tanzania, ambao una maneno ya kumbeza mtu wa shamba, kwamba "ulipotoka shamba kuingia mjini, mimi nilikuona...."

Siti binti Saad yule mwimbaji maarufu wa zamani wa taarab alibezwa sana na wwashindani wake alipoingia mjini Unguja akitokea shamba alikokuwa mfinyanzI.

Siku hizi Tanzania, mtu ukipata matatizo mjini, unaambiwa "utalijua jiji." Matapeli na wajanja wengine wa mjini wakikuibia, unaambiwa "umeingizwa mjini."

Kutokana na mitazamo na itikadi hizi, kila mtu anayeishi mjini au kuja mjini, hataki kuonekana mshamba. Matokeo yake ni kuwa watu wa mjini wanaweza kuwa na tabia za ajabu ajabu, ili mradi wasionekane washamba. Wanaweza wasiwe na heshima au unyenyekevu, maana kwa utamaduni wa mjini, kuwa na heshima na unyenyekevu inaweza kuonekana kama ni kuzubaa. Kuitwa mtoto wa mjini ni jambo la kujivunia, hata kama tabia zenyewe ni hizo nilizoelezea. Kuitwa mshamba ni dharau.

Dhamira hizi zimeelezwa vizuri katika fasihi za mataifa mbali mbali pia. Kwa mfano, hadithi ya kale ya shujaa Gilgamesh iliyoandikwa miaka yapata elfu sita iliyopita huko Iraq kutokana na masimulizi ya mdomo, inasimulia jinsi mtu aliyeishi maporini na wanyama alivyorubuniwa na watu wa mjini hadi akaletwa mjini, kwa msingi kuwa haimfai mtu kuishi porini na wanyama.

Naye mtunzi maarufu Carl Sandburg wa Marekani, katika shairi lake liitwalo "Chicago," alielezea jinsi vijana wa wakulima walivyokuwa wanaingia jijini Chicago na kuharibika kimaadili. Wazo la mji kuwa ni mahali panapoharibu utu na maadili limeelezwa na waandishi wengi. Pamoja na yote hayo, miji inaendelea kuwa sumaku inayowatuva watu wa vijijini.

5 comments:

Fadhy Mtanga said...

Ahsante kwa somo hili. Kaka Mbele, napenda kusoma hizi hadithi za kale. Waweza kuwa na soft copy zake walau mbili tatu?
Kazi njema.

Mbele said...

Ndugu Mtanga, nakuandalia nakala ya hiki kitabu kiitwacho "The Epic of Gilgamesh" nikuletee nitakapokuja Bongo mwezi ujao mwanzoni. Hakina malipo, kwani nami nilikipata cha bure kutoka kwa wachapishaji.

Fadhy Mtanga said...

natanguliza shukrani zangu za dhati. Nakisubiri kwa shauku kubwa sana.
Ubarikiwe zaidi.

Katu said...

Hata pia vitabu vya riwaya elimu ya awali ya sekondari Tanzania wakti huo tukijaribu kufukua haya mambo enzi za Mwalimu J.K. Nyerere za kusoma shule chache takribani nane hivi kwa idadi zilizokuwa zimesimama dede kama hii hapa ya mchepuo wa kilimo Ifakara....

Bwana Ngoswe kupitia kitabu cha Penzi kitovu cha Uzembe amegusia hilo Profesa Mbele na mhusika mkuu alikuwa ni Chonya..

Nawakilisha kwa sasa

Katu said...

Sahihisho katika kuchangia kwangu niliandika vitabu vya RIWAYA badala yake ni VITABU VYA TAMTHILIYA

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...