Sunday, September 26, 2010

Ujumbe Kuhusu Vitabu

Leo nilienda mji wa Duluth kwa matembezi ya masaa machache nikiwa na mwalimu mwenzangu katika idara yetu. Baada ya kuzunguka na gari sehemu kadhaa za mji huo, niliegesha gari kwenye mtaa uitwao Superior Street, unaoonekana katika picha hizi mbili, tukaanza kutembea katika mtaa huu, kuangalia mazingira.

Hatukwenda mbali, tukaona duka la vitabu na moja kwa moja tukaingia humo.

Humo ndani kulikuwa na vitabu vingi sana na vitu vingine vidogo vidogo vya nyumbani, kama vile sahani, glasi, mishumaa, na maua ya mapambo.

Nilipoingia tu, kwenye meza moja karibu na mlango niliona ujumbe uliowekwa kwenye fremu, kuhusu vitabu. Nilivutiwa sana na ujumbe ulioandikwa na Clarence Day, Jr.

Nilimwuliza mama mhudumu humo dukani kama naweza kupiga picha. Alisema kwa uchangamfu kuwa ni sawa kabisa.

Jioni hii, wakati naandika habari hii kwenye blogu, nimetafuta taarifa nikagundua kuwa Clarence Day, Jr. aliandika ujumbe wake mwaka 1920. Kwa jinsi nilivyoupenda, nimeona niuweke hapa na nijaribu kuutafsiri kwa ki-Swahili. :


VITABU

Ulimwengu wa vitabu ni kitu kilichotukuka kwa namna ya pekee kilicholetwa na binadamu. Hakuna anachounda binadamu ambacho kinadumu hivyo: majengo ya kumbukumbu huanguka, mataifa hutokomea, himaya za ustaarabu hupitwa na wakati na kutoweka duniani; kufuatia zama za giza, mataifa mapya hujenga himaya zingine. Lakini ulimwengu wa vitabu una majuzuu yanayodumu daima, yakiwa na upya na ubichi kama siku yalipoandikwa, na yanaendelea kuelezea mioyoni mwa wanadamu kuhusu yaliyojiri hata mioyoni mwa wanadamu waliokwishafariki karne za zamani.

2 comments:

Neema said...

Safi sana Bwana Mbele na karibu sana Duluth
Kili Culture Team

Mbele said...

Asante kwa ujumbe wako. Nafurahi kujua kuhusu Kili Culture Team. Tuzidi kuwasiliana.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...