Friday, November 25, 2011

Mahojiano na Profesa Joseph Mbele

Nimefanya mahojiano mara nyingi na watu mbali mbali, wakiwemo wa-Tanzania, kuhusu shughuli zangu katika jamii, kama vile maandishi na mihadhara. Hapa naleta mahojiano yaliyofanyika Septemba 2006, ili wale ambao hawajawahi kusikia sauti yangu au namna yangu ya kujieleza katika mazungumzo ya papo kwa papo, wapate fursa hiyo.

(Chanzo: Butiama.podomatic)







5 comments:

Anonymous said...

nimekusikia profesa wangu mahojiano mazuri na unaongea kiswahili fasaha sio wengine akishakaa huko anaongea kwa maringo asante sana

Mbele said...

Anonymous, shukrani kwa ujumbe wako. Suala unalogusia, la lugha, ni muhimu sana. Nami miaka mingi iliyopita nilijitafakari nikaamua kufanya juhudi kuboresha ufahamu wangu wa ki-Swahili.

Nashukuru kwa kauli yako kuhusu matumizi yangu ya ki-Swahili kwenye hayo mahojiano. Napenda kusema kuwa nimeendelea kufanya juhudi. Kila ninapokuwa Tanzania, ninanunua vitabu vya waandishi maarufu kama vile Shaaban Robert, Haji Gora Haji, na wengine na ninavisoma ili kuboresha ufahamu wangu wa ki-Swahili.

Vile vile, ninaandika kwa ki-Swahili. Hadi wakati huu, nimeshachapisha kitabu kiitwacho CHANGAMOTO: Insha za Jamii.

Nitaendelea na juhudi hizi, kwani elimu haina mwisho. Lugha ni utambulisho na msingi wa utu na upekee wa kila jamii na taifa. Kuifahamu na kuitumia vizuri lugha yetu ni ishara ya kujitambua na kujiheshimu.

Nikirudi kwenye usemi wako kuhusu hao wanaoongea kwa maringo, napenda kuongezea kuwa wengi pia wanajifanya hawajui ki-Swahili, na wengi wetu tunachanganya maneno ya ki-Swahili na ki-Ingereza. Ukweli ni kuwa tunajidharau tunapofanya hivyo.

Hata kwenye haya mahojiano yangu, pamoja na juhudi zangu zote za kukitumia ki-Swahili vizuri, kuna sehemu ambapo nimekwama. Nataka kuondoa kabisa dosari hizo. Nikifikia hatua ya kutumia ki-Swahili vizuri kabisa, bila kuingiza maneno ya ki-Ingereza, ambayo ni kuficha mapungufu katika ufahamu wa ki-Swahili, nitatembea kifua juu na kujivuna. Nitasema sasa kweli nimeelimika. Tatizo letu wasomi wengi ni kuwa tumesoma ila hatujaelimika.

Simon Kitururu said...

Naengelea kugundua kwanini kuna watu hawaamini Profesa J anafunza KIINGEREZA katika levo NGULI!

Profesa JAY uko kwenye fani na unaweza FANI yani (Nagusia kiswahili kwenye hili)

Mbele said...

Ni kweli, hii ya m-Matengo kuwafundisha wa-Marekani ki-Ingereza kwenye chuo kikuu tayari ni gumzo huko vijiweni, hasa baa :-)

Kali zaidi itakuwa pale nikifanikiwa kukijua ki-Swahili kiasi cha kufundisha chuo kikuu kama Dar. Hapo nitakuwa nimekomesha ubishi :-)

John Mwaipopo said...

nimeyasikiliza mahojiano hakika ni mazuri. nimesikiliza mwanzo-mwisho. niliyasikiliza nikisahihisha mitihani hivyo yalikuwa kiburudisho na elimu tosha. nadhani sasa nikitafute kitabu hiki nikienda dar es salaam.

ila prof pamoja na kuzamia ughaibuni miaka yote hiyo kale kalafudhi ka-kimatengo bado kapo. hongera kwa kukatunza

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...