Monday, February 25, 2013

Mhadhara Kesho Kuhusu Kitabu Changu

Miezi kadhaa iliyopita, niliandika kuhusu mwaliko niliopewa na maprofesa Scott Fee na Becky Davis wa Mankato, Minnesota, kwenda kuongea na wanafunzi wao ambao walikuwa wanawaandaa kwa safari ya Afrika Kusini. Ombi lilikuwa kwamba nikaongee na wanafunzi hao kuhusu masuala ya tofauti za tamaduni, ambayo nimeyaongelea katika kitabu cha cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences.

Siku zimeenda kasi, maana kesho ndio siku ya mhadhara huo. Badala ya kwenda Mankato, nitatoa mhadhara wangu katika chuo cha South Central kilichopo Faribault. Mhadhara wangu utarushwa kwa televisheni kuwawezesha wanafunzi watakaokuwa Mankato kuufuatilia. Nimepangia nikawape mhadhara wa kuelimisha na kusisimua.

Profesa Becky Davis atakuwepo nami Faribault na ndiye atakayenipokea na kunitambulisha. Profesa Fee atakuwa Mankato, pamoja na wanafunzi, wakinisikiliza.

Kama kawaida, nafurahi kupata fursa ya kuongelea masuala ya tofauti za tamaduni. Kama kawaida, nafurahi kuona kitabu changu kinachangia kuwaandaa wanafunzi na wengine wanaoenda Afrika. Kama ninavyosema daima, namshukuru Mungu kwa kunipa uwezo wa kutoa mchango wa aina hii. Nimetoa mihadhara mingi kuhusu suala hili la tofauti za tamaduni, lakini mhadhara wa kesho nitaukumbuka zaidi, kutokana na kwamba nitakuwa naongea kwa mpigo na wasikilizaji katika vyuo viwili.

2 comments:

PBF Rungwe Pilot Project said...

Nakutakia kila la kheri Profesa katika mhadhara huo muhimu ambao utawapa undani wa hali ya Kiafrika hao wanafunzi

Mbele said...

Asante Mkuu. Ndio sasa hivi nimerudi kutoka Faribault, mwendo wa nusu saa kutoka hapa nilipo. Mhadhara ulikwenda vizuri sana. Mbali ya kwamba baadhi ya wanafunzi nilikuwa nao kwenye chumba cha mhadhara pale Faribault, kwenye skrini nilikuwa nawaona wanafunzi waliokuwa kule kwenye mji mwingine, na mwalimu wao.

Makundi yote mawili yaliweza kuwasiliana vizuri kabisa. Niliulizwa masuali na wanafunzi kutoka pande zote mbili. Hii tekinolojia imenivutia.

Kweli tunaweza kufundisha darasa la wanafunzi waliotapakaa sehemu mbali mbali za dunia, kwa kutumia tekinolojia hii. Hakuna dosari yoyote, ni kama wote mpo katika chumba kimoja.

Napenda tu kusema kuwa wote walifurahia sana mhadhara wangu na majibu na maelezo yaliyotokana na masuali yao. Wanataka niende tena siku nyingine, nami sikuwa mchoyo. Nilikubali.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...