Thursday, March 17, 2016

Ninafurahia Kuendesha Blogu

Ingawa kuendesha blogu kuna magumu, ninatambua faida zake. Faida kubwa kabisa kwa upande wangu ni uhuru wa kujieleza. Hakuna yeyote anayenizuia kuandika chochote nitakacho, kwa namna nitakayo.

Ninaifurahia hali hii nikizingatia jinsi vyombo vya habari vinavyotawala uhuru wa watu. Wahariri na wamiliki wa vyombo hivyo wana uwezo wa kulikubali au kulikataa andiko wanaloletewa. Waandishi wanakosa uhuru nilio nao kama mmiliki wa blogu. Ninaamini kuwa baadhi ya mambo ninayoandika katika blogu yangu hayangechapishwa kwingineko. Mfano ni mada za dini.

Mimi ni mtetezi wa uhuru wa watu kujieleza. Nikianzisha mada hapa katika blogu, ninamkaribisha yeyote kuchangia. Ninafurahi kuona hoja zikipambanishwa. Ninafurahi kuwapa watu fursa ambayo ni finyu au inakosekana mahali pengine.

Msimamo huo nimekuwa nao tangu zamani. Siafiki kupigwa marufuku vitabu, magazeti, au njia zingine za watu kujieleza na kusambaza mawazo na mitazamo. Kuunga mkono upigaji marufuku wa maandishi au aina zingine za watu kujieleza ni kujichimbia kaburi. Kama unatetea vitendo hivyo, usilalamike endapo maandishi yako au yale unayoyathamini yatapigwa marufuku. Usilalamike ukihujumiwa haki na uhuru wako wa kujieleza.

Kumiliki na kuendesha blogu kumeniunganisha na wasomaji sehemu mbali mbali za dunia. Ninaangalia takwimu na kujionea idadi ya watu wanaotembelea blogu na mahali waliko. Baadhi yao wananiandikia ujumbe binafsi. Kwa mfano, mwanahabari wa kituo cha televisheni maarufu Tanzania aliniandikia kwamba anafuatilia blogu yangu na inamsaidia katika kuandaa vipindi. Ni faida nyingine na motisha ya kuendesha blogu.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...