Friday, June 3, 2011

Maonesho Minnesota Mwezi Juni

Mwezi huu Juni nimealikuwa kushiriki katika maonesho sehemu mbili tofauti hapa Minnesota. Tarehe 11 nitakuwa Brooklyn Park, kushiriki maonesho ya African Health Action. Wahusika walinialika kwa msingi kuwa wameshaniona kwenye maonesho mengine hapa Minnesota.

Tarehe 16 Juni nimealikwa kushiriki maonesho ya waandishi wa-Marekani Weusi hapa Minnesota. Nilialikwa na mmiliki wa Black Parent Group, waandaaji washiriki wa onesho hilo, ambao wanafahamu kuhusu shughuli zangu, hasa kitabu cha Africans and Americans. Nimetangaza onesho hilo hapa.

Ingawa mimi si m-Marekani, huwa ni kawaida kwa hao wenzetu wa-Marekani Weusi kutujumlisha namna hiyo, kwa vile wanavyoangalia sana rangi ya mtu. Usishangae ukiona wa-Marekani Weusi wanapoandika orodha ya wa-Marekani Weusi maarufu, ukakuta majina ya watu kama Mzee Mandela.

Hao wa-Marekani weusi huwa wanafanya hivyo kwa nia njema na pia kutojua hisia zetu sisi wa-Swahili. Kwa upande wangu, nikizingatia hali halisi ya mahali ninapofundisha, ambacho ni chuo cha wazungu, ni nadra kupata fursa ya kuwa na wa-Marekani weusi. Kwa hivi, naona ni bora kushiriki mialiko yao na kujumuika nao vizuri, kuliko kuanza kuleta zogo ambalo hasara yake inaweza kuwa kubwa kuliko faida. Naamini ni busara kusema kuwa maongezi ya kujipambanua mimi ni nani yatakuja baadaye, baada ya kuzoeana.

Sehemu zote mbili nitakwenda kuonesha vitabu vyangu na kuongea na wadau kuhusu uandishi, uchapishaji, na masuala ya tamaduni katika ulimwengu wa utandawazi wa leo. Wadau mlioko Minnesota mnakaribishwa.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...