Wednesday, October 26, 2011

Mwandishi Nuruddin Farah Katutembelea

Jana jioni, mwandishi maarufu Nuruddin Farah, mzaliwa wa Somalia, alikuja chuoni Carleton, hapa Northfield, kuongea na wadau kuhusu riwaya yake mpya, Crossbones, ambayo imechapishwa mwaka huu.









Nilienda kumsikiliza. Kama ilivyo kawaida katika shughuli za aina hii, vitabu vyake vilikuwepo, vinauzwa. Kwa vile ninavyo vitabu vyake vingine, nilinunua hiki kipya. Hapa pichani mwandishi anasaini nakala yangu. Bei yake ni dola 27.95, yapata shilingi 50,000 za Tanzania. Hiki ni kiasi kidogo sana ukifananisha na hela tunazotumia wa-Tanzania kwenye ulabu na makamuzi mengine. Bora kununua kitabu.




Ingawa bado sijaisoma riwaya ya Crossbones, kwa kufuatilia mazungumzo ya jana na kuiangalia kijuu juu, ni riwaya inayohusu Somalia kabla tu na baada ya uvamizi wa kijeshi uliofanywa na Ethipia miaka michache iliyopita. Ni riwaya inayoelezea athari za matukio hayo katika maisha ya wahusika.













Kwa bahati, nimeshamwona Nuruddin Farah mara kadhaa akihutubia, hapa Marekani. Vile vile, nimepata kufundisha baadhi ya maandishi yake. Mara ya kwanza ilikuwa ni mwaka 1974. Nilikuwa mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, na kwa vile nilikuwa nasomea ualimu, nilienda shule ya wasichana ya Iringa kufanya mazoezi ya kufundisha. Kitabu cha Nuruddin Farah From a Crooked Rib kilikuwa kinatumika katika somo la "Literature."

Miaka ya hivi karibuni, hapa chuoni St. Olaf, nimefundisha pia riwaya zingine za Nuruddin Farah. Ni mmoja wa waandishi bora kabisa kutoka Afrika, ambaye ameshapata tuzo nyingi kwa uandishi wake.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...