Wednesday, March 25, 2015

Picha Nilizopigwa Katika Studio ya Afric Tempo, Machi 21

Tarehe 21 Machi, nilifanyiwa mahojiano na Ndugu Petros Haile Beyene, mkurugenzi wa African Global Roots, katika studio ya Afric Tempo mjini Minneapolis. Aliomba tufanye mahojiano kuhusu kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences ambacho alikuwa amekisoma na kukipenda. Niliandika taarifa ya mahojiano hayo katika blogu hii.

Hapa naleta picha mbili alizopiga Ndugu Malick, mmiliki wa studio, aliyerekodi kipindi kwa ajili ya televisheni. Amenitumia leo hii. Hapa kushoto anaonekana Ndugu Petros Haile akiwa nami, tayari kwa mahojiano, ambayo watakaoyaona katika televisheni watayafurahia. Kama wasemavyo mitaani, kaeni mkao wa kula.

Nimeona niweke picha hizi hapa, nikizingatia kuwa wako ambao wangependa kuona sura yangu ilivyo kwa sasa, baada ya muda mrefu wa kuumwa. Ninaendelea kupona vizuri, ingawa pole pole. Hata safari kama hizi za Minneapolis, umbali wa maili 45, ninaendesha gari mwenyewe. Na majukumu yangu niliyozoea, kama vile kutoa mihadhara na kufundisha, nayamudu bila shida. Namtegemea Mungu daima; alichonipangia ndicho kitakachojiri.

Monday, March 23, 2015

Mwandishi Grace Ogot Amefariki

Wikiendi hii, habari zimetapakaa kuwa mwandishi Grace Ogot wa Kenya amefariki. Habari hizi zimenishtua na zimenikumbusha mengi kuhusiana na mwandishi huyu.

Nilipokuwa kijana, miaka ya sitini na kitu, ndipo nilianza kusikia habari zake. Nilikuwa nasoma masomo ya sekondari katika seminari ya Likonde. Shule ilikuwa na maktaba nzuri sana, chini ya usimamizi wa Padri Lambert, OSB, ambaye alikuwa mwalimu wetu wa ki-Ingereza na historia.

Nilikuwa msomaji makini wa vitabu, na nilikuwa nafuatilia kwa karibu uandishi katika Afrika Mashariki, Afrika, na sehemu zingine za dunia. Ndipo nilipoanza kuyafahamu maandishi ya Grace Ogot.

Riwaya yake, The Promised Land, ilikuwa na maana sana katika ujana wangu, kwani ilichangia kunifanya niipende zaidi fasihi. Hadithi fupi ya "The Rain Came" ilinigusa kwa namna ya pekee. Miaka ya mwishoni mwa sabini na kitu, wakati nafundisha katika Idara ya "Literature" ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, nakumbuka nilifundisha kitabu cha Gikuyu Folktales cha Grace Gecau. Humo niliona hadithi ambayo ilinikumbusha "The Rain Came," nikapata kuelewa vizuri jinsi Grace Ogot alivyotumia urithi wa hadithi za jadi katika uandishi wake.

Miaka ile nilikuwa navutiwa na waandishi wengine wa Afrika Mashariki, kama vile Okot p'Bitek, Taban lo Liyong, James Ngugi (ambaye baadaye alibadili jina lake na kujiita Ngugi wa Thiong'o), Austin Bukenya, Laban Erapu, Barbara Kimenye, na wengine kadha wa kadha.

Ile ilikuwa ni miaka ya kukumbukwa, kwani ni wakati ule ndio nami nilihamasika kuandika hadithi kwa ki-Ingereza. Nilifurahi kwa namna isiyoelezeka hadithi yangu ya "A Girl in the Bus" ilipochapishwa katika jarida maarifu la Busara, mwaka 1972, nilipokuwa mwanafunzi Mkwawa High School.

Kumbukumbu zote hizi, na nyingine kem kem zimenijia na zinazunguka kichwani mwangu tangu niliposikia kuwa Grace Ogot amefariki. Ametoa mchango uliotukuka katika fasihi. Astarehe kwa amani.

Sunday, March 22, 2015

Siendi Mahali Kuuza Vitabu

Mimi ni mwalimu, mwelimishaji, darasani na katika jamii. Ili kufanikisha majukumu yangu, ni mtafutaji wa elimu bila kuchoka. Ni mwanafunzi muda wote ili kujiimarisha katika ualimu na uelimishaji.

Nafundisha na kujufunza kwa kuongea na watu ana kwa ana, iwe ni darasani au nje ya darasa. Nafundisha na kujifunza kwa mawasiliano ya masafa marefu, iwe kwa barua pepe au kwa simu. Hivi karibuni, nimeanza pia kutumia Skpe. Hizi zote ni njia za kuelimisha sambamba na kujielimisha.

Lakini vile vile, mimi ni mwandishi wa makala na vitabu. Kwa kawaida uandishi wa nakala huchukua muda mwingi, na vitabu ndio zaidi, kwani kitabu kinaweza kuchukua miaka kukiandaa na kukiandika. Kwa ujumla unaandika katika upweke. Nakubaliana na kauli ya Ernest Hemingway, "Writing, at its best, is a lonely life."

Kwangu mimi kama mwalimu naona uandishi wa aina ya vitabu ninavyoandika kuwa ni mwendelezo wa ufundishaji. Ninapokwenda na vitabu vyangu kwenye tamasha au maonesho, ninakwenda kama mwalimu. Siendi kufanya biashara.

Ni tofauti na mvuvi anapoenda na tenga lake la samaki sokoni, au mkulima anapoenda na mkungu wake wa ndizi. Hao wanaenda kuuza samaki au ndizi. Ikifika mwisho wa siku hawajauza hizo samaki au ndizi, wanaona wameshindwa biashara siku hiyo, au wanaona wamepata hasara.

Mimi, pamoja na kuwa ninaenda maoneshoni na vitabu vyangu, nisipouza hata kimoja sioni kama nimeshindwa kwani ninakuwa nimeshaongea na watu wengi, kuwaelimisha na kuelimishwa nao. Wengine huulizia kuhusu uandishi au uchapishaji wa vitabu. Wengine huulizia kuhusu masomo ninayofundisha au kuhusu utafiti wangu. Niligusia masuala haya katika blogu hii.

Hutokea, mara kwa mara, kuwa katika kuongelea mambo hayo, watu hao hupenda wenyewe kununua vitabu vyangu. Labda wanataka kufahamu zaidi fikra na mitazamo yangu. Labda wanataka kumbukumbu ya kukutana kwetu na maongezi yetu. Na hapo ndipo linapoingia suala la watu kutaka kusainiwa kitabu. Ni kumbukumbu.

Nikirejea tena kwa mvuvi muuza samaki au mkulima na mkungu wa ndizi, sijui kama kuna watu wanapokuwa sokoni wanaenda kumwuliza mvuvi habari za uvuvi au wanaenda kwa muuza ndizi kupata elimu kuhusu kilimo cha ndizi. Na sijui kama muuza samaki mwenyewe au muuza ndizi mwenyewe anategemea hivyo.

Zaidi ya yote, mimi kama mwalimu sina masaa ya kazi. Najiona niko kazini muda wote, tangu asuhuhi mpaka usiku, labda tu ninapokuwa katika majukumu mengine ya binafsi, familia, au jamii. Kama siko darasani, niko ofisini, maktabani, au nyumbani, ninasoma. Niko mahali ninatayarisha masomo au ninasahihisha kazi za wanafunzi. Hakuna jamii hapa duniani ambayo inamlipa mwalimu kwa masaa yote hayo anayokuwa kazini.

Kwa kurudia, ninapokuwa maoneshoni na vitabu vyangu, niko pale kama mwalimu. Si mfanyabiashara, ambaye anahesabu mafanikio yake kwa kigezo cha fedha anachopata siku hiyo.

Saturday, March 21, 2015

Leo Nimehojiwa na "African Global Roots"

Nimerejea mchana huu kutoka Minneapolis, kwenye mahojiano na African Global Roots (AGR). Wiki mbili hivi zilizopita, Ndugu Petros Haile, mkurugenzi wa AGR alikuwa ameniomba tufanye mahojiano hayo.

Ndugu Haile nami tumefahamiana kwa miaka kadhaa. Nimewahi kushiriki katika program zake kwa kupeleka vitabu vyangu. Vile vile, alivyovyofahamu kuwa nimepeleka wanafunzi Tanzania kwenye kozi ya Hemingway, aliniomba niandike makala, ambayo aliichapisha.

Kwa mahojiano ya leo, Ndugu Haile alitaka tuongelee kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences, ambacho alishakisoma miaka iliyopita. Alitamani, kwa kutumia mawasiliano ya AGR kusambaza ujumbe katika jamii ya wa-Afrika hapa Marekani na ulimwenguni na kwa watu wengine, kuhusu umuhimu wa kuyaelewa masuala ninayoongelea katika kitabu changu.

Kwa kuwa nilijua kuwa Ndugu Haile alitaka kunihoji kuhusu dhughuli zangu za kuelimisha umma, nilichukua pia nakala ya kitabu changu cha Matengo Folktales, ambacho ni ushahidi wa namna ninavyojitahidi kujifunza kutokana na masimulizi ya jadi ya mababu na mabibi zetu wa Afrika, na namna ninavyotumia hazina hii kuuelimisha ulimwengu kuhusu mchango wa wahenga wetu katika dunia.

Mahojiano yalikuwa mazuri. Ndugu Haile alitunga masuali muhimu kutokana na yaliyomo katika kitabu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences na pia aliniuliza masuali kuhusu utafiti wangu ulioniwezesha kuandika kitabu cha Matengo Folktales.

 Mahojiano haya tumefanyia katika kituo cha Afric Tempo, kinachomilikiwa na Ndugu Malick wa Senegal. Leo ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kufika mahali hapo, ambapo pana mgahawa, stoo, na studio ya kurekodia programu za televisheni.

Sitaandika zaidi kwa leo. Nangojea hadi mahojiano yatakapopatikana mtandaoni, ndipo niwaeleze walimwengu. Inafurahisha sana kuweza kukutana na kushirikiana na watu kama Malick na Petros, wenye kupenda kujitolea kwa hali na mali ili kujenga maelewano katika jamii. Jambo moja tuliloongelea leo na kukubaliana ni kuwa tunaamini kuwa Mungu ametuweka duniani kwa madhumuni kama hayo.


Wednesday, March 18, 2015

Neema Komba Ashinda Tuzo ya Uandishi

Neema Komba ni mwandishi chipukizi wa ki-Tanzania. Kama wewe ni mfuatiliaji wa uandishi wa Tanzania wa siku hizi, huenda tayari unafahamu habari zake. Mbali na uandishi, Neema ni mhamasishaji wa uandishi na sanaa husika kupitia jukwaa liitwalo la Poetista.

Mwaka 2011 Neema alichapisha kitabu cha mashairi yake, See Through the Complicated. Nilikisoma muda si mrefu baada ya kuchapishwa. Mwishoni mwa mwezi Julai, 2012, nilipokuwa Tanzania, tulikutana Lion Hotel, Dar es Salaam, tukaongelea uandishi wake.

Pamoja na mashairi, Neema ni mwandishi wa insha. Hivi karibuni nilianza kufahamu kuwa anaandika pia hadithi, niliposoma kuwa hadithi yake "Setting Babu on Fire" imeteuliwa kuwemo kati ya hadithi tatu zilizoteuliwa kushindania tuzo ya "Flash Fiction" ya Etisalat. Hayo yalikuwa mashindano makubwa ya uandishi barani Afrika. Hatimaye, "Setting Babu on Fire" imeshinda tuzo ya kwanza.




Ushindi huu ni sifa kubwa kwa Neema mwenyewe na kwa Tanzania. Nikizingatia kuwa huyu ni mwandishi chipukizi, lakini mwenye ubunifu wa hali ya juu na mwenye kukimudu vizuri ki-Ingereza, sina shaka kuwa nyota yake itazidi kutukuka na kung'ara miaka ya usoni. Nampa hongera sana na kumtakia kila la heri.

Sunday, March 15, 2015

Darasa la "Hemingway in East Africa 2013" Kando ya Ziwa Babati

Mwezi Januari, 2013, nilikuwa Tanzania na wanafunzi kutoka Chuo cha St. Olaf katika kozi ya "Hemingway in East Africa."

Niliitunga kozi hii mwaka 2006, kwa ajili ya Chuo cha Colorado. Kwa miaka kadhaa, kabla ya kutunga kozi hiyo, nilisoma maandishi ya Ernest Hemingway aliyoandika kufuatia safari zake mbili Afrika Mashariki, miaka ya 1933-34 na 1953-54.

Lengo la kozi lilikuwa kuwafundisha wanafanuzi kwa kusafiri nao katika baadhi ya maeneo alimopita Hemingway, huku tukisoma maandishi yake kuhusu safari zake katika maeneo haya. Maandishi hayo ni pamoja na kitabu cha Green Hills of Africa na Under Kilimanjaro, hadithi ya "The Short Happy Life of Francis Macomber," barua, na insha kadhaa katika magazeti.

Pichani wanaonekana wanafunzi na madereva wetu pembeni mwa Ziwa Babati. Katika Green Hills of Africa, Hemingway aliandika kuhusu Babati na Ziwa Babati:

     We left, soon after midnight, ahead of the outfit, who were to strike camp and follow in the two lorries. We stopped in Babati at the little hotel overlooking the lake and bought some more Pan-Yam pickles and had some cold beer (uk. 143).

Thursday, March 12, 2015

Vitabu Nilivyonunua Jana na Leo

Kila mtu ana mambo anayoyapenda sana, na yuko tayari kuyapata au kuyafanya kwa gharama yoyote. Vitabu ni kati ya vitu ninavyovipenda sana, na niko tayari kutumia gharama yoyote kuvipata. Imekuwa hivyo tangu nilipokuwa shule ya msingi.

Mara kwa mara, katika blogu hii, nimeandika taarifa ya vitabu nilivyonunua. Siandiki taarifa ya kila kitabu, kwani wakati mwingine nasahau. Lakini leo nimekumbuka. Naandika kuhusu vitabu nilivyonunua jana na leo.

Nilitoka zangu ofisini, nikaelekea kwenye duka la vitabu. Nje ya duka kulikuwa na "seli" ya vitabu. Kulikuwa na vitabu vingi sana vikiuzwa kwa bei nafuu. Hapo hapo nilijiunga na wengine waliokuwa wanavichambua vitabu hivyo na kuvinunua.

Jungu kuu halikosi ukoko. Niliviona vitabu vinne vilivyonivutia kwa namna ya pekee, nikavinunua.

Kimojawapo ni Wine to Water: How One Man Saved Himself While Trying to Save the World. Hilo jina tu lilinivutia, nikakumbuka hadithi ya muujiza wa Yesu wa kugeuza maji kuwa divai. Katika kukiangalia, niliona kuwa mtungaji wake, Doc Hendley, ameandika kitabu hiki kuelezea harakati zake za kuwasaidia watu wa Darfur kuchimba visima vya maji, akipambana na hatari zote zilizoko Darfur. Niliona kitabu hiki kitanifundisha mengi, na nilitaka kiwemo kati ya vitabu vya nyumbani mwangu.

Kitabu cha pili ni Walk in Their Shoes: Can One Person Change the World? kilichoandikwa na Jim Ziolkowski. Hicho nacho kilinivutia. Jina lake lilinikumbusha kitabu ambacho nilikinunua miaka michache iliyopita, kiitwacho Leaving Microsoft to Change the World: An Enterpreneur's Odyssey to Educate the World's Children, kilichoandikwa na John Wood. Mtu unaposoma vitabu vya aina hii, unajikuta ukijifunza sio tu uwezekano bali umuhimu wa kujitoa katika ubinafsi na badala yake kutumia vipaji na uwezo wako kuwanufaisha walimwengu.

Nilikiona kitabu kingine, And Then Life Happens: A Memoir, chenye jina la Auma Obama kama mwandishi, na picha yake. Hilo jina peke yake lilinifanya nikiangalie, nikaona kuwa huyu dada ni binti wa Barack Hussein Obama, baba mzazi wa Rais Obama wa Marekani. Binti huyu alizaliwa Kenya, akaishi miaka mingi na kusoma Ujerumani. Kitabu chake hiki, ambacho ni juu ya maisha yake, alikiandika kwa ki-Jerumani, kikatafsiriwa na Ross Benjamin. Nilivutiwa na taarifa hizo, nikakichukua bila kusita.

Kitabu cha nne nilichokinunua hiyo jana ni Indigenizing The Academy: Transforming Scholarship and Empowering Communities. Wahariri wake ni Devon Abbot Mihesuah na Angela Cavender Wilson. Mimi kama mwanataaluma, nilivutiwa moja kwa moja na kitabu hiki. Nilivutiwa zaidi nilipogundua kuwa kinahusu utafiti na uandishi juu ya wenyeji asili wa Marekani, ambao tunawaita Wahindi Wekundu. Niliona kuwa ni kitabu kinachohoji jadi ya utafiti, taaluma, na uandishi kuwahusu hao Wahindi Wekundu, na, inavyoonekana, kinaleta fikra za kimapinduzi, kama yale ambayo kwetu Afrika yalianzishwa na wataalam kama Cheikh Anta Diop na Walter Rodney.

Katika maisha yangu, kununua vitabu na kuvisoma ni kama ugonjwa usiotibika. Leo nilipita tena pale kwenye duka la vitabu, nikaona "seli" bado inaendelea. Nilijitosa tena katika kuchambua vitabu, nikaibuka na kitabu kikubwa sana kiitwacho Beyond Human Nature: How Culture and Experience Shape the Human Mind, kilichotungwa na Jesse J. Prinz. Nilikiangalia, nikafahamu kuwa, kwa kutumia utafiti wa "neuroscience," "psychology," na "anthropology," mwandishi analeta fikra mpya juu ya mambo yanayomjenga binadamu kitabia. Bila kusita, nilikikwapua kitabu hiki. Kitabu chochote kinacholeta fikra mpya ni dhahabu.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...