Sunday, September 20, 2015

Nimerejea Kutoka Kanisani

Nimetoka kanisani kusali, na ninaona ni sawa tu kuandika habari hiyo hapa katika blogu yangu. Hii si mara ya kwanza kwangu kuandika habari ya namna hiyo.

Kwanza napenda kuwajulisha ndugu, marafiki na wote wanaofuatilia habari zangu, kwamba afya yangu imeendelea kuwa bora. Zaidi ya huu mkongojo ninaotembea nao, uonekanao pichani, hakuna dalili ya tatizo. Naendesha gari mwenyewe, hata umbali mrefu. Natembea na mkongojo kwa kuwa daktari anataka nitembee nao. Nina kila sababu ya kumshukuru Mungu.

Kama ilivyo kawaida, katika ibada ya misa ya leo tumewaombea watu wote. Tumewakumbuka waumini wenzetu wanaosali makanisani, misikitini, na katika nyumba za ibada za dini zingine, tukiombea amani ulimwenguni. Wa-Katoliki hatujiombei wenyewe tu, bali wanadamu wote.

Kila Jumapili, tangu Baba Mtakatifu wa sasa, Papa Francis II, alipotoa waraka wake wa kichungaji, Laudato Si, tumekuwa tukisali sala yake ya kuiombea dunia:

A prayer for our earth

All-powerful God, you are present in the whole universe
and in the smallest of your creatures.
You embrace with your tenderness all that exists.
Pour out upon us the power of your love,
that we may protect life and beauty.
Fill us with peace, that we may live
as brothers and sisters, harming no one.
O God of the poor,
help us to rescue the abandoned and forgotten of this earth,
so precious in your eyes.
Bring healing to our lives,
that we may protect the world and not prey on it,
that we may sow beauty, not pollution and destruction.
Touch the hearts
of those who look only for gain
at the expense of the poor and the earth.
Teach us to discover the worth of each thing,
to be filled with awe and contemplation,
to recognize that we are profoundly united
with every creature
as we journey towards your infinite light.
We thank you for being with us each day.
Encourage us, we pray, in our struggle
for justice, love and peace.

Leo Papa Francis yuko upande huu wa dunia, ziarani Cuba, akiwa njiani kuja Marekani na kuhutubia bunge la Marekani na pia Umoja wa Mataifa. Kuna msisimko mioyoni mwa watu, wanapongojea kusikia mawaidha ya kiongozi huyu aliyejipambanua kwa kutetea wanyonge na uangalifu wa dunia hii ambayo ni msingi wa maisha yetu na ya viumbe vyote.

Wednesday, September 16, 2015

Filamu ya "Papa's Shadow:" Fursa ya Kuitangaza Tanzania

Nina furaha kuandika kuhusu filamu ambayo imeandaliwa iitwayo "Papa's Shadow," inayomhusu mwandishi maarufu Ernest Hemingway. Katika filamu hiyo, ninaonekana nikiongea na Mzee Patrick Hemingway, ambaye ni mtoto pekee wa Ernest Hemingway aliye hai. Ana umri wa miaka 87. Tunaongelea maisha, safari, maandishi na fikra za Hemingway, hasa kuhusu Afrika.

Sehemu nyingi hapa duniani ambako Hemingway alipita au kuishi na akaandika habari zake, zimejipatia umaarufu. na zinafaidika hasa katika utalii. Mifano ni Cuba na mji wa Pamplona nchini Hispania. Watu wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla tuna bahati hiyo, kwani Hemingway alikuja na kuishi kwetu mara mbili, mwaka 1933-34 na 1953-54, akaandika vitabu, hadithi, insha na barua kuhusu aliyoyaona.

Filamu ya "Papa's Shadow" ilitokana na kozi niliyofundisha Tanzania mwezi Januari mwaka 2013 juu ya Hemingway. Kozi ile ilimhamasisha Jimmy Gildea, mmoja wa wanafunzi wangu, kutengeneza filamu hiyo. Alianzisha kampuni, Ramble Pictures, akaanza kutegeneza hiyo filamu ya kuelimisha. Anaendelea kutengeneza filamu zingine zenye kuelimisha.

"Papa's Shadow" inaitangaza Tanzania kwa namna ya pekee. Kuna kampeni ya kuchangisha fedha za kumalizia malipo ya usajili na taratibu zingine kabla ya filamu kuonyeshwa na kusambazwa. Naleta hapa ujumbe ambao umeandikwa na binti yangu Zawadi, mmoja wa watu wanaojitolea katika Ramble Pictures, unaoelezea kampeni hiyo.

Nitapenda ujumbe huu uwafikie wa-Tanzania popote duniani, hasa wanadiaspora, ofisi za ubalozi, Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, na wadau wengine wote. Nilitumia miaka kadhaa kusoma maandishi ya Hemingway na kuandaa kozi ambayo ni chimbuko la filamu hii. Ninapangia kuendelea kufundisha kozi hiyo. Nawe m-Tanzania mwenzangu una fursa ya kutoa mchango wako. Tushirikiane. Tutafanikiwa. Sisi tuliokuwepo wakati Tanganyika ilipopata Uhuru tunakumbuka kauli mbiu ya Mwalimu Nyerere ya kuhimiza maendeleo ya Taifa jipya: "It can be done; play your part."

=====================================================

Hello!

My name is Zawadi Mbele, and I am contacting you today to let you know about an amazing project. Ramble Pictures, a Minneapolis-based, independent film company, recently launched a 30-day "Kickstarter" campaign in order to raise funds for the distribution of our completed documentary, Papa's Shadow.

Papa's Shadow is a personal film about Ernest Hemingway in East Africa. It explores his hunting expeditions and holds key dialogues on subjects such as race, language, and the cultures that distinguish us as citizens of the world. Featuring exclusive testimony by Ernest's only living son, Patrick Hemingway, as well as Tanzanian author and Hemingway scholar, Dr. Joseph Mbele, this documentary explores the integral role of two safaris in their shaping of an author and demise of a legend. 

Over the past four years, hard work and creative energy has been poured into making this feature-length documentary. The film has already been completed, however, we cannot show or distribute the film until we finish paying for copyright licensing. Again, please visit our Kickstarter webpage to learn more about how you can play an important role in bringing this documentary to distribution. Also, with Kickstarter, we are offering exclusive rewards with every donation, such as the new Hemingway Library Edition of "Greens Hills of Africa," signed by Patrick Hemingway. 

If there is someone else from your organization you would recommend contacting, we would be grateful to have our information passed along. If you can, please take the time to explore our webpage and let me know if you have any questions at all. You can email me directly or email Elizabeth Turner at elizabeth@ramblepictures.com.

Thank you for your time, and we look forward to hearing back from you!

Sincerely,

Zawadi Mbele
email: zawadi.mbele@gmail.com

Saturday, September 12, 2015

Wazo Kuhusu Kuchagua Kiongozi

Tunavyoelekea kwenye uchaguzi, mwezi ujao, nchini Tanzania, tunaona malumbano yanashamiri. Tunataka kujua nani anafaa kuwa kiongozi. Napenda kuchangia kifupi malumbano haya. Mchango wangu unasimama katika taaluma na utafiti.

Suala la uongozi linaingia moja kwa moja katika utafiti juu ya akili na saikolojia. Miaka yetu hii, watafiti wamekuwa wakituambia kuwa kuna aina nyingi za akili. Kuna maandishi mengi juu ya suala hilo, ambalo kwa ki-Ingereza linajulikana kama "multiple intelligence" au "multiple intelligences."

Kwa mujibu wa utafiti huo, uongozi unahitaji aina ya akili iitwayo "emotional intelligence." Ni akili inayomfanya mtu awe na mvuto kwa watu kwa haiba na mwenendo wake, uwezo wa kuunganisha watu, uwezo wa kuwafanya wafuate njia fulani kwa kutumia ushawishi, si vinginevyo. Mtu mwenye "emotional intelligence" kubwa ndiye anayefaa kuwa kiongozi.

Katika malumbano yanayoendelea miongoni mwa wa-Tanzania wakati huu wa kuelekea uchaguzi, sijaona dhana hii ya "emotional intelligence" ikitajwa. Sijaona kigezo hiki kikitajwa. Watu wanaongelea vitu kama uchapa kazi kama kigezo, lakini si "emotional intelligence." Watu wanaongelea uwezo wa kutoa hotuba ndefu, au uwezo wa kutembea kwa ukakamavu. Lakini hawaongelei "emotional intelligence."

Kwani kutoa hotuba ndefu ndio nini? Mtu unaweza kuongea kwa masaa lakini ukawa unasema umbea na upupu. Mtu mwingine anaweza kuongea kifupi, lakini akawa anatoa hoja thabiti.

Kwani nguvu za mwili na kifua kama cha mpiga ndondi ndio nini? Inahusiana vipi na uongozi? Lakini hivyo ndivyo vigezo vinavyoshabikiwa katika malumbano ya wa-Tanzania.

Hii haishangazi. Tanzania ni nchi ya watu wasio na utamaduni wa kusoma vitabu vya kuelimisha. Watanzania ni wavivu kutafuta elimu. Ndivyo walivyo, na ndivyo wanavyojiandaa kwa uchaguzi.

Wednesday, September 9, 2015

Vijana Wameonana Na Mzee Patrick Hemingway

Leo nimepata ujumbe na picha kutoka kwa Jimmy Gildea, anayeonekana kushoto kabisa pichani hapa kushoto, kwamba walikuwa mjini Bozeman, Montana, wakingojea kuonana na Mzee Patrick Hemingway na mkewe Mama Carol.

Jimmy alikuwa ni mmoja wa wanafunzi wangu katika kozi ya Hemingway in East Africaambayo nilifundisha Tanzania mwezi Januari mwaka 2013. Kutokana na kozi ile, na pia safari tuliyofunga kwenda Montana kuonana na Mzee Patrick Hemingway, Jimmy ametengeneza filamu iitwayo Papa's Shadow, ambayo kwa kiasi kikubwa inatokana na kozi ile.

Katika filamu hii, ambayo si ya maigizo, Mzee Patrick Hemingway na mimi tunaongelea maisha na maandishi ya baba yake, Ernest Hemingway, na tunaongelea kwa undani zaidi maisha na mizunguko yake Afrika Mashariki, miaka ya 1933-34 na 1953-54, na pia falsafa yake kuhusu masuala ya maisha na uandishi. Katika kutengeneza filamu hiyo, Jimmy ameshirikiana na hao vijana wanaoonekana pichani, na wengine ambao hawamo pichani.

Nimetamani sana kama nami ningekuwa Bozeman leo kuonana na Mzee Patrick Hemingway na Mama Carol. Hata hivi, nafarijika kwamba ninampigia simu wakati wowote nikipenda. Kwa kuwa aliishi miaka yapata 25 Tanganyika (na hatimaye Tanzania), ameniambia kuwa anafurahi kuongea na mimi, kwa kuwa hana watu wa kuongea nao kuhusu Tanzania na Afrika.

Kwa upande wangu, najifunza mengi kutoka kwa Mzee Patrick Hemingway, juu ya Ernest Hemingway, waandishi wengine, historia ya Tanganyika, na mambo mengine mengine. Pia ninaguswa kwa jinsi anavyokipenda kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences. Hata katika filamu ya Papa's Shadow anakitaja na kukinukuu. Katika hiyo picha ya pili, tuliyopiga nyumbani mwake mjini Craig, Montana, anaonekana Mzee na Mama Carol Hemingway, na kitabu kiko mezani hapo mbele yake.

Tuesday, September 8, 2015

Udini Katika Kampeni za Urais

Katika kipindi hiki cha kampeni za urais nchini Tanzania, tunashuhudia mengi. Kwa mfano, kwa siku mbili tatu hivi tumekuwa tukisikia shutuma nyingi dhidi ya mgombea wa UKAWA, Edward Lowassa kwamba anafanya udini. Chanzo cha shutuma ni kauli anayoonekana akitoa katika video alipokuwa anaongea na waumini wa ki-Luteri. Anasikika akiomba wamwunge mkono, awe m-Luteri wa kwanza kuwa rais.

Kauli hiyo imewasha moto miongoni mwa wapinzani wake, kwa mfano CCM. Wamekazana kupaaza sauti wakisema kuwa mgombea huyu hafai; anatugawanya kwa msingi wa dini, na atatuletea maafa akiwa rais.

Binafsi, sioni kama watu hao wana hoja ya msingi. Lowassa hana tabia hiyo inayosemwa. Tumemshuhudia kwa miaka anavyojumuika na waumini wa dini mbali mbali katika shughuli zao. Tumemwona akiongoza harambee za kuchangia misikiti na makanisa ya madhehebu mbali mbali sehemu mbali mbali za nchi. Kwa kufahamu alivyo na ushawishi mkubwa, viongozi na waumini wa dini mbali mbali wanafurahi kumwalika kwenye shughuli zao hizo.

Kwa kuizingatia hayo, ni wazi kuwa alichosema kwa waumini wenzake akiwaomba wampe kura siwezi kukiita udini. Siamini kama alikuwa na nia mbaya. Ni jambo la kawaida kabisa tunapokuwa na watu wa aina yetu tunazungumza kwa namna tofauti na tunapokuwa katika mazingira mengine.

Lowassa hakuwa anaongea na umma wa wa-Tanzania. Alikuwa anaongea na wa-Luteri wenzake, sawa na mimi ninavyoweza kuongea na wa-Matengo wenzangu au wa-Katoliki wenzangu, si kwa nia mbaya ya kibaguzi hata kidogo. Naweza kukubali kuwa labda Lowassa aliteleza katika kauli yake, lakini sikubali kuwa yeye anafanya udini.

Kinachonishangaza ni kuwa katibu mwenezi wa CCM, Nape Nnauye, ambaye ndiye, kama msemaji wa CCM, alitoa tamko la kumshutumu Lowassa, alisema siku kadhaa zilizopita kuwa CCM lazima ishinde uchaguzi, hata kwa goli la mkono. Aliwaambia hivyo wanahabari. Yaani aliitangazia dunia dhamira hii ya kuhatarisha amani. Ni tofauti na Lowassa ambaye alikuwa anaongea na wa-Luteri wenzake kanisani.

Nape Nnauye angekuwa ameongea na wanaCCM wenzake peke yao, huenda hata sisi wengine hatungesikia kauli yake. Hata kama tungesikia, yaani kama kauli yake ingevuja, kama ilivyovuja ya Lowassa, ningemhukumu kwa namna hiyo ninayomhukumu Lowassa. Lakini yeye amevuka mstari na kuutangazia ulimwengu dhamira ambayo ni mbaya kwa Taifa. Haoni hilo kosa lake kubwa, ila anajipa jukumu la kumshutumu Lowassa. Inanishangaza.

Friday, September 4, 2015

Gazeti la "MwanaHalisi" Lafunguliwa

Nimefurahi kuona taarifa kuwa mahakama kuu ya Tanzania imeamuru kufunguliwa kwa gazeti la MwanaHalisi ambalo serikali ya CCM ililifungia mwaka 2012. Ni ushindi kwa mmiliki wa MwanaHalisi, Saed Kubenea, na timu yake. Ni ushindi kwa watetezi wa uhuru wa vyombo vya habari.

Nilikuwa mmojawapo wa watu waliopinga wazi wazi hatua ya serikali ya kulifungia gazeti la MwanaHalisi. Ninasimamia uhuru wa kutoa mawazo, uhuru wa waandishi, kama ilivyofafanuliwa katika tangazo la kimataifa la haki za binadamu.

Taarifa tulizozipata leo ni kwamba mahakama imetamka kwamba ni juu ya Saed Kubenea kuamua kuendelea kuchapisha gazeti lake au kutoendelea. Vile vile, mahakama imeacha mlango wazi kwa Saeed Kubenea kuishtaki serikali na kudai fidia kwa kipindi chote ambapo gazeti lake lilikuwa limezuiwa.

Ni wazi kwamba, endapo Saed Kubenea atadai fidia, ambayo ni haki yake, walipa kodi wa Tanzania watabeba mzigo mkubwa. Labda watajifunza hasara ya kuiweka madarakani serikali isiyo makini, isiyoheshimu haki za binadamu ipasavyo, au kuwaweka madarakani watu wasio makini, wasioheshimu haki za binadamu ipasavyo. Tusifiche ukweli: kulifungia gazeti la MwanaHalisi, sawa na vitendo vingine vya uvunjwaji wa haki za binadamu, kumechafua jina la Tanzania.

 

Wednesday, September 2, 2015

Hotuba ya Dr. Wilbroad Slaa Kuacha Siasa

Kuhusu hotuba ya Dr. Slaa kwa waandishi wa habari akitangaza kuondokana na siasa, mengi muhimu yamesemwa na wenye upeo na tafakari nzito kunizidi. Ila nami kama raia mwingine yeyote, nina uhuru kamili wa kuongelea suala hili, kama mwananchi anavyoongea mtaani, ambayo ni haki yake.

Napenda nianze kwa kujikumbusha kwamba kwa miaka mingi, CCM wamekuwa wakimbeza Dr. Slaa, kwamba ni mzushi na mropokaji. Alipoanza kusema kuna ufisadi, CCM walimkatalia katakata, wakasema ni mzushi. Baadaye, vijana wa UVCCM wakawa wanafanya kibarua cha kumtukana Dr. Slaa.

Sasa, baada ya huyu mzushi na mropokaji kutema cheche juzi, mbele ya waandishi wa habari, nasubiri kuwasikia CCM wanasemaje. Wakisema tumpuuze kwa vile ni mzushi na mropokaji, basi ina maana kuwa UKAWA hawana sababu ya kukosa usingizi wala kujibishana naye. Kwa nini mtu ukose usingizi kwa sababu ya maneno ya mtu anayefahamika wazi kuwa ni mzushi na mropokaji?

Nitawashangaa CCM iwapo watashangilia mashambulizi ya Dr. Slaa dhidi ya Lowassa na UKAWA. Nitawashangaa.

Dr. Slaa amewaponda kabisa CCM. Sio tu kwa jinsi alivyoifananisha CCM na choo kichafu, bali kwa kauli yake kwamba serikali ya CCM ni waoga wa kuwachukulia hatua watuhumiwa wa ufisadi. Amesema kuwa CCM ni mfumo unaofuga mafisadi. Sio hivyo tu, bali amewaumbua pia wabunge wa CCM, kwamba hawasomi wanayopaswa kusoma.

Alivyosema hayo kuhusu wabunge wa CCM, nimekubaliana naye kabisa, kwani nami nilishaandika kuhusu wabunge hao nikiwaita mbumbumbu. Ushahidi ulikuwa jinsi walivyotoroka midahalo wakati wa uchaguzi wa mwaka 2010. Midahalo inaheshimiwa na watu wote wenye akili, lakini mbumbumbu hawaelewi umuhimu wake.

Umbumbumbu wa wabunge wa CCM umejidhihirisha tena na tena kwa tabia yao ya kuzomea Bungeni, na tabia ya kuunga mkono chochote kinachosemwa na serikali ya CCM. Kwa hayo yote, ninaichukulia kwa uzito upasao kauli ya Dr. Slaa kuwa wabunge wa CCM hawasomi.

Dr. Slaa hajawaonea CCM kwa hilo. Nakumbuka ule mwaka Mwalimu Nyerere alipojiandaa kung'atuka uenyekiti wa CCM, alizunguka nchi nzima akikagua uhai wa chama hicho. Inaonekana hakuridhika, kwani kuna siku alisema kuwa wako watu katika CCM ambao hata mtihani kuhusu "Azimio la Arusha" hawawezi kupasi. Kwa hivyo Mwalimu alishabaini umbumbumbu katika CCM tangu miaka ile ya katikati ya themanini na kitu.

Sasa, nikijumlisha hayo yote, nakuta kwamba Dr. Slaa ametuambia kuwa Tanzania inaendeshwa na mbumbumbu wasiosoma. Inaendeshwa na vipofu. Hilo ni janga kwa Taifa. Halafu ukiongezea na lile wazo la kuwa CCM ni kama choo kichafu, unaona wazi kuwa Dr. Slaa amemwaga hadharani mambo mazito dhidi ya CCM.

Sasa katika hali hii, nikiangalia wagombea wawili wa urais, yaani Magufuli na Lowassa, naona kuwa tafsiri ya kauli za Dr. Slaa ni kuwa UKAWA wamemtoa Lowassa chooni, lakini Magufuli ameng'ang'ania kubaki chooni. Ningekuwa mpiga kura, kura yangu ningempa huyu Lowassa aliyelopolewa kutoka chooni kuliko huyu Magufuli ambaye amepania kufia humo chooni.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...