Tuesday, March 15, 2016

Kutana na Fundi Abdallah Ramadhani

Leo ninapenda kumtambulisha Abdallah Ramadhani, ambaye nimefahamiana naye siku chache tu zilizopita katika mtandao wa Facebook. Ilikuwa bahati tu kuwa nilianzisha mawasiliano naye, na ndipo nikaweza kujua habari zake. Nilivutiwa na shughuli za ufundi anazofanya.




Nilimwambia kuwa ningeweza kuzitangaza shughuli zake katika blogu yangu. Nilitambua tangu miaka iliyopita kuwa ninaweza kuitumia blogu yangu hii kutangazia shughuli za wa-Tanzania ninaokutana nao au ninaopata habari zao na kuvutiwa na namna wanavyojishughulisha. Ninawaunga mkono. Kwa mfano, niliwahi kuandika juu ya wajasiriamali wa Duka Asili na Super Muhogo.



Abdallah Ramadhani alizaliwa Temeke, Dar es Salaam, mwaka 11 Mei,1979.  Anatengeneza viatu vizuri kama inavyoonekana pichani katika ukurasa huu. Ufundi huu alijifunza kwa baba yake, ambaye alijifunza kwa wa-Hindi.

Wa-Tanzania tujijengee utamaduni wa kuvithamini vipaji vya wa-Tanzania wenzetu, na huduma wanazotoa. Tuwe na utamaduni wa kuzithamini kazi zao. Tuzithamini bidhaa zinazozalishwa nchini mwetu, kama nilivyowahi kuelezea katika blogu hii, na katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Manufaa yake ni kwa hao wahusika na kwa Taifa.

Unaweza kuwasiliana na Abdallah kwa simu, namba  255-682-588-583 au 255-719-588-583


Sunday, March 13, 2016

Piano Katika Nyumba ya Hemingway, Oak Park

Wanasema tembea uone. Ni njia ya uhakika ya kujipatia elimu. Tarehe 26 Februari, nilifika Oak Park, Illinois, kutembelea nyumba alimozaliwa mwandishi Ernest Hemingway na pia jumba la kumbukumbu juu yake. Niliandika kuhusu ziara hii katika blogu hii na katika blogu yangu ya ki-Ingereza.

Mimi kama msomaji wa maandishi na habari za Ernest Hemingway nilifurahi kufika eneo hilo ambalo habari zake nilikuwa nimezifahamu kwa miaka mingi. Kabla ya kuisogea nyumba, nilimwomba dreva wa teksi, mzaliwa wa Nigeria, anipige picha.



Humo ndani, baada ya kukaribishwa sehemu ya mapokezi na kulipia, nilijumuika, na wageni wengine, tukaanza ziara. Katika chumba cha kwanza, kuna viti, meza, na vitu vingine, na vile vile piano kama inavyoonekana pichani.

Mama ya Ernest, Grace Hall Hemingway, alikuwa mpenda muziki na uimbaji, na aliwahamasisha wanafamilia katika fani hizo. Mtoto Ernest hakupenda, lakini alilazimika.  Nilijifunza mengi. Nitajitahidi kuyaelezea kidogo kidogo siku za usoni.

Friday, March 4, 2016

Dini ni Siasa Tu, Asema Mwandishi Nawal el Saadawi



Katika kozi yangu ya Muslim Women Writers, tunajiandaa kusoma The Fall of the Imam, riwaya ya Nawal el Saadawi wa Misri. Nimeshawapa wanafunzi maelezo kuhusu historia ya fasihi andishi Misri, ambayo imekuwepo tangu miaka yapata elfu saba iliyopita. Hii ni kwa mujibu wa maandishi ya kale yaliyogundulika, kama vile hadithi na mafundisho ya dini, hasa The Egyptian Book of the Dead.

Miaka ilivyopita, fasihi ya Misri ilitajirika kwa kutokana na mikondo ya ndani na nje, na hiyo ya nje ni kutoka sehemu kama Mashariki ya Kati na Uarabuni, pande zingine za Afrika, na Ulaya. Kwa karne moja na kidogo iliyopita, wamejitokeza waandishi wengi maarufu nchini Misri. Mifano ni Naguib Mahfouz, Taha Hussein, Tawfiq al Hakim, Yusuf Idris, Nawal el Saadawi, Sonallah Ibrahim,  na Alifa Rifaat. Kwa ujumla wao, waandishi hao wametumia mikondo niliyoitaja.

Katika kozi hii ya Muslim Women Writers, nimemchagua mwandishi mmoja tu kutoka Misri, ambaye ni huyu Nawal el Saadawi. Na nimechagua riwaya yake moja tu. Ningeweza kuchagua riwaya tofauti ya mwandishi huyu, au ningeweza kufundisha hadithi za Alifa Rifaat, Distant View of a Minaret.

Nawal el Saadawi si tu mwandishi, bali ni daktari na mwanaharakati maarufu. Amekuwa akipambana na mfumo wa kijamii wa nchi yake, ambao unawakandamiza wanawake. Anazikosoa na kuzipiga vita itikadi zozote, zikiwemo dini, zinazohalalisha ukandamizaji wa wanawake. Nawal el Saadawi ni mama shujaa ambaye anajiamini na hatishiki, kama inavyonekana katika video niliyoweka hapa ambayo nitawaonyesha wanafunzi wangu kama maandalizi ya kujadili The Fall of the Imam.

Wednesday, March 2, 2016

Picha za Mtoto Ernest Hemingway

Tarehe 27 Februari, nilitembelea Oak Park, pembeni mwa Chicago. kwa ajili ya kuzuru nyumba alimozaliwa mwandishi Ernest Hemingway na nyumba ya kumbukumbu, Hemingway Museum, kama nilivyoripoti katika blogu hii na blogu ya ki-Ingereza.

Katika Hemingway Museum, ambayo picha yake inaonekana hapa kushoto, niliona picha nyingi, zikiwemo za mtoto Ernest Hemingway.


Hapa kushoto anaonekana babu wa Ernest kwa upande wa mama yake, akiwa na wajukuu. Kushoto kabisa ni Ernest, na hao watoto wengine ni dada zake.








Hapa kushoto anaonekana mtoto Ernest, akiwa na bunduki na zana ya kuvulia samaki. Tangu utotoni, Ernest alifundishwa kuvua samaki na kuwinda.







Hapa kushoto, mtoto Ernest anaonekana akimlisha mnyama ambaye kwa ki-Ingereza huitwa squirrel. Nimeangalia mtandaoni nikaona kuwa mnyama huyu anaitwa kindi kwa ki-Swahili.

Nilipoiona picha hii nilivutiwa kuona mnyama ametulia namna hii, lakini nilipoisogelea na kusoma maelezo yanayoonekana chini kushoto, nilitambua kuwa huyu si mnyama hai. Ni mzoga ambao umekarabatiwa na kufanywa uonekane kama mnyama hai.

Hata hivyo picha inanivutia, kwa namna inavyowasilisha ukweli muhimu juu ya Hemingway, jinsi maisha yake na hisia zake zilivyofungamana na maisha ya viumbe kama wanyama, samaki na ndege.

Mtoto Ernest alipokuwa shuleni aliandika kuwa ndoto yake maishani ilikuwa ni kuwa mwandishi na pia mtu wa kusafiri. Ilikuwa kama amejitabiria, kwani akiwa kijana wa miaka 18, alipelekwa Kansas City ambako aliajiriwa kama ripota wa gazeti la Kansas City Star.

Katika kipindi hicho yeye na waandishi wengine wa gazeti hili waliwajibika kufuata orodha ya amri kali kuhusu uandishi uliotakiwa. Watafiti wote wanakubaliana kwamba kufanya kwake kazi katika Kansas City Star kulimjenga Hemingway katika aina ya uandishi aliyotumia maisha yake yote.

Hapa kushoto Ernest anaonekana akiwa ameshika bunduki na ndege. Sikuona maelezo juu ya picha hii, ila ninahisi ilipigwa baada ya Hemingway kumpiga huyu ndege kwa risasi.

Jadi ya kupiga picha ya mwindaji na mnyama au ndege aliyemwua imekuwepo tangu zamani. Kuna picha kadhaa za Hemingway za miaka ya baadaye akiwa na wanyama aliowaua, si tu huku Marekani, bali pia sehemu zingine, ikiwemo Afrika Mashariki. Wachambuzi wa saikolojia wanaweza kuelezea vizuri maana ya jadi hii ya kuthamini hiki kinachoitwa "trophy" kwa ki-Ingereza.

Saturday, February 27, 2016

Nimezuru Nyumba ya Hemingway, Oak Park

Leo nilizuru nyumba ya Hemingway, kitongoji cha Oak Park, karibu na Chicago. Kwa miaka kadhaa, nilikuwa nimewazia kufanya hivyo.  Nyumba hii ambayo ni namba 339 katika mtaa wa Oak Park Avenue, ndimo alimozaliwa Ernest Hemingway na kuishi hadi alipokuwa na miaka sita. Sasa ni nyumba ya hifadhi ya mambo mengi ya familia ya Hemingway.

Nimejifunza mengi katika kutembelea nyumba hii.  Nilipoingia, nilijumuika na wageni wengine wanne, tukafanya ziara pamoja, tukiongozwa na dada aliyejitambulisha kwa jina la Michelle ambaye anaonekana pichani. Alitupitisha sehemu zote za nyumba hii, akatuelezea historia yake na habari za vitu vilivyomo.

Alituelezea mambo muhimu yaliyomlea Ernest Hemingway katika nyumba hii. Mfano ni namna mama yake alivyotaka kila mtoto na mtu mwingine katika nyumba hii awe na ujuzi wa muziki. Kabla ya ziara hii, nilijua kuwa mama yake Ernest Hemingway alitaka Ernest ajifunze muziki, lakini sikujua kuwa alitaka hivyo kwa kila mtoto na wengine pia. Ziara hii pia imenifungua macho kuhusu namna mtindo wa usimuliaji hadithi aliokuwa akitumia Ernest Hemingway ulivyojengeka tangu utoto wake katika nyumba hii.

Friday, February 26, 2016

Jumuia ya Vyuo (ACM) Yakihitaji Kitabu

Leo nimeshinda hapa mjini Chicago nikihudhuria mkutano wa bodi ya programu ya Tanzania ya ACM. ACM ni jumuia ya vyuo vikuu 14 vya hapa Marekani ambayo inaendesha programu za masomo na utafiti sehemu mbali mbali za dunia. Kwa upande wa Afrika, kuna programu ya Tanzania na programu ya Botswana. Mimi ni mjumbe katika bodi za programu hizi mbili.

Mkutano kama wa leo tunafanya mara moja kwa mwaka kwa program ya Tanzania na vivyo hivyo kwa programu ya Botswana. Kila mwaka tunapeleka wanafunzi kwenye nchi hizi kwa muhula moja. Tunapokutana tunatathmini mwenendo wa masomo kwa mwaka husika. Tunapitia ripoti mbali mbali na kuzijadili, kubaini mapungufu na mafanikio na mapungufu, kutoa mapendekezo na kujiwekea malengo.

Leo, pamoja na yote hayo, limetokea jambo ambalo sikutegemea. Profesa Paul Overvoorde, aliyeambatana na wanafunzi Tanzania muhula uliopita, alianza hima kunieleza kuwa alikuwa ametumia kitabu changu cha Africans and Americans Embracing Cultural Differences na kilimsaidia sana katika kuendesha programu. Profesa huyu nilikuwa sijawahi kuonana naye, kwa sababu sikuwa nimehudhuria mikutano yetu kwa miaka mitatu. Alivyokuwa anaelezea kitabu hiki, nilijikuta nina hisia mchanganyiko: shukrani, furaha, na mshamgao.

Kama vile hii haikutosha, wakati wa mkutano, Profesa Karl Wirth naye akakitaja kitabu hiki. Huyu tumefahamiana tangu miaka ya mwanzo ya programu hizi. Wakati tulipokuwa tunahitimisha mkutano alitoa wazo kwa uongozi wa ACM kuwa kitabu hiki kifanywe msingi wa "webinar" itakayovihusisha vyuo vyetu vyote kwa ajili ya kufundishia mambo yiliyomo, na hii iwe ni mkakati wa kuwavutia wanafunzi kwenye programu.

Wazo hili limeshapita. Wakati wajumbe tulipokuwa tunaagana, mhusika wa tekinolojia za mawasiliano katika ACM aliniambia kuwa atanitafuta ili nichangie hiyo "webinar." Nami nilimwambia nangojea kwa hamu kushirikiana naye, kwani ninamini kuwa nitajifunza mambo mapya.

Nimeandika habari hii kwa sababu maalum. Kwanza ni kujiwekea kumbukumbu, kama ilivyo desturi yangu katika blogu hii. Pili ni kwa sababu ninawakumbuka watu kadhaa ambao wamejaribu kuzibeza juhudi zangu, nami nikawa siyumbishwi. Ninafanya shughuli zangu kwa bidii na umakini niwezavyo na baada ya hapo ninayathamini matokeo yake. Mtu lazima ujiamini na ujithamini. Ukithamini kile unachokifanya. Ukiwa na mtazamo huu, huwezi kuyumbishwa. Matokeo yanakuja kuonekana baadaye. Chambilecho wa-Swahili wa zamani mgaagaa na upwa, hali wali mkavu.

Tuesday, February 23, 2016

"So Long a Letter" Katika Kozi ya "Muslim Women Writers"

Kozi yangu ya Muslim Women Writers inaendelea vizuri. Tulianzia India, na hadithi ya Sultana's Dream ya Rokeya Sakhawat Hossain. Baada ya hapo tunasoma So Long a Letter, utungo wa Mariama Ba wa Senegal, nchi mojawapo maarufu katika uwanja wa fasihi ya Afrika.

Senegal imetoa watunzi kama Leopold Sedar Senghor, Cheikh Hamidou Kane, Birago Diop, na Sembene Ousmane, kwa upande wa wanaume, na kwa upande wa wanawake kuna watunzi kama Aminata Sow Fall na Mariama Ba.

So Long a Letter ni utungo ulioandikwa kwa mtindo wa barua, ambayo mhusika mkuu anamwandikia mwanamke mwenzake, rafiki yake. Kwa hali hiyo, utungo huu unafuata jadi ambayo wanafasihi huiita "epistolary." Neno "epistolary" linatokana na neno la ki-Latini ambalo maana yake ni barua.

Suala moja muhimu linaloongelewa ni la wake wenza. Ni suala lenye chimbuko lake katika Qur'an, Sura iv aya 3:

     If ye fear that ye shall not
Bes able to deal justly
With the orphans,
Marry women of your choice,
Two, or three, or four;
But if ye fear that ye shall not
Be able to deal justly (with them),
Then only one, or (a captive)
That your right hand possess.
That will be more suitable,
To prevent you
From doing injustice.

Yusuf Ali, ambaye tafsiri yake ya Qur'an nimeinukuu hapa juu, anafafanua aya hii vizuri. Anakumbushia kwamba aya hii ilitokea katika mazingira maalum, ambamo kutokana na vita ya Uhud, jamii ya wa-Islam ilikuwa na wajane na yatima wengi, pamoja na mateka wa vita. Ilikuwa lazima watu hao watendewe kwa ubinadamu na haki kwa kiwango cha juu kabisa. Ruhusa ya kuwaoa wajane hao imewekewa masherti.

Kabla ya u-Islam, watu walikuwa wanaoa walivyopenda, lakini aya hii inaweka mipaka. Mtu anaweza kuoa hadi wake wanne, si zaidi, lakini kama Yusuf Ali anavyosema, "provided you could treat them with equality, in material things as well as in affection and immaterial things." Yaani masherti ni kwamba uweze kuwatendea wake hao kwa usawa katika mahitaji ya vitu, katika upendo, na mengine ya aina hiyo.

Kutokana na masherti hayo, Yusuf Ali anasema: "As this condition is most difficult to fulfill, I understand the recommendation to be towards monogamy." Yaani, kwa jinsi masherti yalivyo magumu kutekelezeka, nachukulia kwamba agizo hili linaegemea kwenye kuwa na mke moja.

Huu ndio msingi katika Qur'an wa suala la mitara. Wanawake wa-Islam wamekuwa wakilalamika kwamba fundisho la Qur'an limepotoshwa. Wanaume wamejitwalia mamlaka ya kupindisha mafundisho ya Qur'an na kuhalalisha mambo wanayoyapenda wao.  Hii ndio hali inayojitokeza katika So Long a Letter.

So Longer a Letter ni andiko linalohuzunisha kwa jinsi Ramatulaye anavyoelezea roho mbaya ya baadhi ya wanaume. Mume wake mwenyewe alijiolea binti kinyemela, na wanawake wengine wanakutana na adha za aina hiyo. Lakini, hasemi kuwa wanawake muda wote hawana dosari. Anakiri kuwa katika ndoa zingine, wanawake wanawatesa wanaume.

Hatimaye, So Long a Letter inaelezea matumaini ya kubadili mambo na kuwawezesha wanawake kushika nafasi wanazostahili katika jamii, wakitumia vipaji ambavyo wanavyo.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...