Wednesday, February 8, 2012

Buriani: Mwandishi Faraji Katalambula

Jana tumepata habari kuwa mwandishi Faraji Katalambula, amefariki Dar es Salaam. Nilipokuwa mwanafunzi Mkwawa High School, 1971-72, Faraji Katalambula alikuwa anavuma kuliko waandishi wote wa ki-Swahili waliokuwa hai wakati ule. Picha ya Faraji Katalambula hapa kushoto nimeipata Hiluka Filmz.






Nakumbuka jinsi riwaya yake ya Simu ya Kifo ilivyoleta msisimko kwa wafuatiliaji wa riwaya za upelelezi. Laiti ningesoma maandishi yake tangu miaka ile. Leo ningeweza kuelezea hili au lile kwa kujiamini.

Lakini miaka ile mimi nilikuwa sijishughulishi sana na ki-Swahili. Nilizama katika maandishi ya ki-Ingereza. Vijana wenzangu waliopenda riwaya za ki-Ingereza walikuwa wanapenda sana riwaya kama za Ian Fleming na James Hadley Chase. Mimi sikuwahi kuzisoma hizo.

Nikirudi kwenye uandishi wa ki-Swahili, napenda kusema kuwa nashukuru kuwa miaka iliyofuata, nilijirudi, kama ninavyoelezea katika kitabu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Nami sasa nimejiunga na wasomaji wanaowaenzi waandishi wetu wanaotumia ki-Swahili.

Faraji Katalambula aliandika pia riwaya zingine, akaingia pia katika tasnia ya filamu. Ametoa mchango mkubwa kwa jamii, na ingawa ameondoka, kama walivyoondoka akina Mgeni bin Faqihi, Shaaban Robert, Amri Abedi, na Mathias Mnyampala, mchango wake utadumu duniani. Apumzike kwa amani.

No comments:

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...