Saturday, May 30, 2015

Ualimu ni Wito

Ualimu unahitaji moyo. Anayedhani ni mchezo, aiangalie na kuitafakari katuni hii.

Bahati mbaya jina la mchoraji sijalipata, ningemshukuru.

Friday, May 29, 2015

Toleo Jipya la "Green Hills of Africa" Linaandaliwa

Nilimpigia simu Mzee Patrick Hemingway tarehe 22 mwezi huu, tukaongea kwa saa moja na robo. Tuliongelea mambo mengi, kama nilivyogusia katika blogu yangu ya ki-Ingereza. Mzee Patrick Hemingway ni mtoto pekee aliyebaki wa mwandishi maarufu Ernest Hemingway.

Mwandishi huyu ni wa pekee, sio tu kwa kuwa alishinda tuzo ya Nobel, bali pia kwa kuwa mtindo wake wa kuandika ulichangia kubadilisha uandishi wa ki-Ingereza wa karne iliyopita. Katika mfumo wa elimu wa Tanzania wa miaka ya sitini na kitu na sabini na kitu, wanafunzi tulikuwa tunasoma angalau kitabu kimoja cha Ernest Hemingway, For Whom the Bell Tolls, sambamba na vitabu vingine maarufu vya waandishi mbali mbali.

Katika mazungumzo yetu, Mzee Patrick Hemingway aliniarifu kuwa toleo jipya la kitabu cha Green Hills of Africa litachapishwa miezi ya karibuni. Nilifurahi kusikia habari hii. Green Hills of Africa ni masimulizi ya Ernest Hemingway juu ya safari aliyofanya nchini Tanganyika, mwaka 1933-34. Nilisisimka Mzee Hemingway aliposema kuwa katika toleo hili kutakuwemo "diary" ya mama yake, Pauline, aliyoandika wakati wa safari hiyo.

Nilifahamu kuhusu kuwepo kwa hiyo "diary," na nilifahamu kuwa imehifadhiwa katika chuo kikuu cha Stanford. Kwa miaka kadhaa nilikuwa nikiwazia kwenda kuisoma. Kwa hivi, hii habari kwamba itachapishwa imenifurahisha kwa namna ambayo siwezi kuieleza.

Habari ya kuchapishwa toleo jipya la Green Hills of Africa ni muhimu sana. Tanzania ingeweza kuitumia hii kama fursa adimu ya kujitangaza kwa ajili ya utalii.  Lakini kutokana na kukosekana kwa utamadini wa kusoma vitabu, sitegemei jambo hilo litafanyika. Tofauti na zamani, Tanzania ya leo haimjui Hemingway.

Wenzetu katika nchi zingine wamechangamkia fursa za namna hii na wanafaidika. Mfano moja ni mji uitwao Pamplona, nchini Hispania. Mji ule tangu zamani una jadi yake ya mchezo wa "bull fighting" ambao unamshindanisha shujaa na fahali uwanjani. Ernest Hemingway alitembelea Pamplona mwaka 1923 akavutiwa na mchezo huo. Aliandika kitabu The Sun Also Rises, ambacho kilielezea "bull fighting" na kuufanya mji ule uwe maarufu sana, unaovutia maelfu ya watalii, ingawa haukuwa na umaarufu huo kabla. Sehemu zingine ambamo Hemingway aliishi au alipita na kuandika habari zake, kama vile Oak Park (Illinois), Michigan Kaskazini, Paris, Key West (Florida), Bimini, na Cuba, zinavuna faida kutokana na utalii. Nimewahi kuelezea hayo katika blogu hii.

Nina hakika kuwa mimi ni m-Tanzania wa kwanza kuifahamu habari ya toleo jipya la Green Hills of Africa, na nimeona niiweke hapa katika blogu yangu, nikijua kuwa kuna wa-Tanzania watakaoisoma. Laiti nchi yetu ingekuwa imeamka, ingeanza kujiandaa kuchuma faida za toleo jipya la kitabu hiki kwa kuitangaza Tanzania na sehemu zote alizopitia Hemingway nchini mwetu. Ingekuwa jamii yetu inathamini vitabu, ingeandaa matangazo na makaribisho ya toleo hili jipya. Hii ingekuwa pia fursa ya kuhamasisha utalii wa ndani. Lakini, sina imani yoyote kuwa haya yatafanyika. Ninaifahamu nchi yangu: ni kwenye miti ambako hakuna wajenzi.

Tuesday, May 26, 2015

Mwaliko Chuo Kikuu cha Winona

Nimepata mwaliko kutoka Chuo Kikuu cha Winona, Minnesota, kwenda kutoa mhadhara tarehe 23 Juni. Huu utakuwa ni mchango wangu katika semina ya mafunzo kwa wanafunzi kutoka sehemu mbali mbali itakayofanyika Juni 17-27. Kama ilivyo kawaida yangu, nimeona niweke kumbukumbu hapa.

Mafunzo haya yatalenga kuwaandaa wanafunzi hao kwa masomo ya juu, waweze kuifahamu hali halisi ya maisha ya chuoni na taratibu za taaluma, waweze kujijengea hali ya kujitambua na uwezo wa uongozi.

Mratibu wa mafunzo, Alexander Hines, ambaye anafahamu kiasi shughuli zangu,  aliniambia tuangalie ni kipi kati ya vitabu vyangu viwili kitafaa zaidi kwa semina hii: Africans and Americans: Embracing Cultural Differences au Matengo Folktales. Nilishauri kwamba hicho cha pili kingeendana vizuri zaidi na dhamira kuu ya semina.

Tumekubaliana. Tumekubaliana nikaelezee ni nini tunaweza kujifunza kutokana na tamaduni za jadi za Afrika katika masuala haya ya kujitambua, falsafa ya maisha, na uongozi katika dunia ya leo na kesho.

Kama ilivyo kawaida yangu, huwa napokea mialiko ya kutoa mchango wa mawazo kufuatana na mahitaji ya wale wanaonialika. Itabidi nitafakari na kuandaa mawazo yatakayotoa mchango unaohitajika katika semina. Wazo la kutumia kitabu cha Matengo Folktales kama msingi ni wazo muafaka, kwani masimulizi haya ya jadi yanathibitisha jinsi wahenga wetu walivyoyatafakari masuala muhimu ya maisha, mahusiano, na mengine yanatuhusu leo na yataendelea kuwa muhimu daima.
 

Sunday, May 24, 2015

Angalizo kwa Wenye Vyama: Tanzania ni Yetu Wote

Mimi ni m-Tanzania ambaye si mwanachama wa chama chochote cha siasa. Natoa angalizo kwa wa-Tanzania wenye vyama, hasa CCM, wazingatie kuwa Tanzania ni yetu wote. Naitaja CCM namna hii kwa sababu ni chama tawala, chenye wajibu wa kuongoza njia na kuwa mfano kwa wengine.

Wa-Tanzania wenye vyama wakumbuke kuwa wao ni wachache kwa kufananisha na idadi ya wa-Tanzania kwa ujumla. Wafanye siasa zao, ila wasisahau jambo hilo. Nasema hivyo kwa sababu wana tabia ya kujiona kuwa wao ndio Tanzania, na Tanzania ni wao.

Kinachonikera zaidi ni fujo. Wa-Tanzania wenye vyama wana tabia ya kuleta fujo na kuhujumu amani, hasa kinapokaribia kipindi cha uchaguzi. Ni aibu sana kwamba, kutokana na fujo za wa-Tanzania wenye vyama, tumefikia mahali sasa ambapo watu wanasali na kufanya ibada kuombea amani. Hii ni fedheha ambayo tumeletewa na wa-Tanzania wenye vyama.

Ni sahihi kumwomba Mungu atupate mvua ya kutosha kwa mazao yetu. Ni sahihi kumwomba atuepushe na majanga kama vile matetemeko ya ardhi. Ni sahihi kumwomba atupe uzima siku hadi siku tuweze kujenga nchi yetu na kutimiza majukumu yetu mengine.

Lakini kuombea amani kwa kuwa inatishiwa na utovu wa nidhamu unaofanywa na wa-Tanzania wenye vyama ni jambo lisilokubalika. Kuombea amani kwa sababu ya utovu wa busara wa watu hao ambao wanadhani nchi hii ni yao peke yao, wanaodhani wana haki ya kujifanyia watakalo katika nchi hii, ni jambo lisilokubalika. Hili si suala la kuombea amani. Ni suala la kupambana na hao wahujumu wa amani.

Inashangaza kwamba hata Ikulu imeshindwa kutambua hilo. Haijawahi kutokea Ikulu ikawaita wa-Tanzania wasio na vyama kwa mazungumzo na mashauriano. Ikulu imekuwa tayari kuwaita wenye vyama na kuongea nao, lakini sio sisi tusio na vyama, ambao ndio wengi zaidi na ni mfano wa kuigwa.

Wa-Tanzania wenye vyama wazingatie kuwa sisi tusio na vyama hatujawahi na hatuna mpango wa kuhujumu amani ya Tanzania kama wanavyofanya wao. Tumetunza heshima ya Tanzania wakati wao wanaihujumu. Wajifunze kutoka kwetu ili wote tudumishe amani na tuipe nchi yetu heshima inayostahili.

Saturday, May 23, 2015

Leo Nimenunua Kitabu: "Jesus: Prophet of Islam"

Leo nilikwenda Minneapolis kwenye mkutano mdogo wa watu wanne ambao tulifanyia katika jengo la maduka na biashara mbali mbali liitwalo Somali Mall. Ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kuingia katika jingo hili. Nilipata fursa ya kuingia katika duka la vitabu liitwalo Akmal Bookstore, ambalo limejaa vitabu vya ki-Islam katika ki-Arabu na ki-Somali.

Niliuliza iwapo kuna vitabu vya ki-Ingereza, nikaonyeshwa. Niliviona vingi vilivyonivutia, nikanunua kimoja, Jesus: Prophet of Islam, kilichoandikwa na Muhammad 'Ata' ur-Rahim na Ahmad Thomson.

Nimefahamu kwa miaka mingi kuwa katika u-Islam, Yesu anatambulika kama mtume maarufu, ila sio mwana wa Mungu, kama tunavyomwona sisi wa-Kristu. Sioni tatizo, wala sikosi usingizi kwa sababu hiyo. Ninachozingatia ni waumini wa dini mbali mbali kuheshimiana, kila mtu na imani yake. Tukumbuke kwamba dini zinatofautiana, na kuna dini ambazo hamzimjui Yesu kabisa, iwe ni kama mtume au mwana wa Mungu.

Mara yangu ya kwanza kuelewa namna wa-Islam wanavyomwona Yesu ni wakati nilipokuwa nafundisha somo la "Epic" kwa wanafunzi wa uzamili (M.A.) katika idara ya "Literature," Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, mwaka 1986-88. Kati ya maandishi ya kitaaluma niliyoyaongelea darasani ni insha maarufu ya Alan Dundes, "The Hero Pattern and the Life of Jesus."

Ulipofika muda wa kuandaa tasnifu, mwanafunzi mojawapo, Hamza Njozi, aliniambia kuwa angepnda kuandika kuhusu masimulizi juu ya Yesu (Issa) katika Qur'an. Niliona ni mada murua. Alifanya utafiti na uchambuzi mzuri akamaliza tasnifu yake. Katika kumwelekeza kwa miezi yote ya utafiti na uandishi wa tasnifu, nami niliweza kufahamu msimamo wa Qur'an juu ya Yesu (Issa).

Hii leo, nilipokiona kitabu cha Jesus: Prophet of Islam, nilikumbuka yote hayo, nikakinunua bila kusita. Nangojea kwa hamu kukisoma.

Friday, May 22, 2015

Msikiti Wachomwa Moto Saudia

Nimeona taarifa leo kuwa msikiti umechomwa moto huko Saudi Arabia. Ni msikiti wa dhehebu la Shia. Kwa wale wasiofahamu, wa-Islam, kama walivyo wa-Kristu, wana madhehebu mengi, kama vile Sunni, Shia, Ismailia, Ahmadiya na Tijanniya.

Habari ya msikiti kuchomwa moto imenikera, kama ninavyokerwa na habari za kuchomwa moto kanisa au nyumba nyingine ya ibada ya dini yoyote. Nimesema tena na tena kuwa ninaziheshimu dini zote, ninaiheshimu misahafu ya dini zote, na ninazihehimu nyumba za ibada za dini zote. Ninaamini kuwa hiyo ndiyo njia pekee ya busara ambayo tunapaswa kuifuata.

Sawa na waumini wa dini zingine, nami nililelewa katika imani kwamba dini yangu ndiyo pekee dini ya kweli. Nilifundishwa kwamba nje ya dini yangu, nje ya u-Katoliki, hakuna wokovu. Ninajua kuwa wa-Islamu nao wanafundishwa hivyo hivyo, kuwa nje ya u-Islamu hakuna wokovu. Niliwahi kuwa mwanachama katika mtandao wa Radio Imaan, wa wa-Islam. Waliniambia kuwa mimi ni kafiri na kwamba nisiposilimu sitaingia ahera.

Hii ndio hali halisi. Binafsi nimeamua kujitungia mwelekeo nilioutaja hapa juu, ingawa ninajihesabu kama m-Katoliki. Katika hilo, simtumikii wala kumfuata binadamu. Natumia akili yangu na kufuata dhamiri yangu.

Kwa nini mtu uchome moto msikiti wowote, kanisa lolote, au nyumba ya ibada ya dini yoyote? Kwa nini usikemee kuchomwa moto kwa msikiti wa Shia kwa vile tu wewe ni Sunni, au ni m-Kristu, au ni m-Hindu? Kwa nini usikemee kuchomwa moto kanisa, kwa vile tu wewe si m-Kristu?

Kama hukemei, unaufumbia macho uozo ambao siku moja utakuja kusababisha nyumba ya ibada yako ichomwe moto. Usishangae ikitokea hivyo, wala usikasirike, kwani roho yako haina tofauti na ya yule atakayefanya uhalifu huo. Kilichopo ni kujitambua.

Tumelelewa na tunalelewa katika njia ya giza. Tuamke. Tuanze kujijengea mtazamo mpya wa kuheshimiana wanadamu wote, kila watu na imani yao, wenye dini na wasio na dini, na tuwalee watoto wetu katika njia hiyo.

Hayo ndio mawazo yaliyonijia niliposoma taarifa ya kuchomwa msikiti wa Shia kule Saudia. Ni mawazo yanayoendelea kunisonga na kuisumbua akili yangu. Kama unaona nimepotoka au ninapotosha, nawe ni muumini wa dini, kumbuka kuwa una wajibu wa kujitokeza, kukosoa, na kurekebisha. Ukiacha kufanya hivyo, kumbuka kuna jehenam au motoni, kama tunavyoita wa-Kristu. Na ukichangia, ukajiita "anonymous," unajisumbua na unajidanganya, kwani ingawa mimi sitakutambua, Mungu (Allah) anakuona na atakufichua siku ya kiyama. Kazi kwako.

Thursday, May 21, 2015

Kusonga Mbele na Kutoyumbishwa

Naandika makala hii kuwapa moyo wengine, hasa vijana, wanaojituma kujiendeleza katika fani yoyote na kimaisha kwa ujumla. Kwa ujumla, mawaidha haya yanapatikana vitabuni.

Katika vitabu vinavyoelezea mikakati ya mafanikio, kitu kimoja kinachosisitizwa ni kutambua kwamba unaposonga mbele, kuna watu watakaokuandama kwa mategemeo ya kukukatisha tamaa na kukurudisha nyuma. Watabeza shughuli zako na mafanikio yako.

Kwa mujibu wa vitabu hivyo, hao ni watu wa kuwapuuza. Ni muhimu pia kuwapuuza wale wasio na mtazamo wa maendeleo yao wenyewe. Badala ya kupoteza muda kuwa na watu wa namna hiyo, andamana na watu waliomo katika njia ya mafanikio, au waliofanikiwa. Utajifunza kutoka kwao.

Watu wenye mafanikio, wanajiamini, na hawaoni shida kuwashauri au kuwasaidia wengine nao wafanikiwe. Napenda kunukuu maneno ya Henry Rogers mtu maarufu aliyeanzisha na kuendesha Rogers & Cowan, kampuni ya mahusiano ya jamii:

Not only is it essential to make someone feel important, the art of psychorelations demands that we also make the person feel at ease. As I reflect back on my life, I find that powerful and important people have always made an effort to make me feel comfortable. My experience has been that the more important they are, the more gracious they are. Could it be that their ability to reach out graciously to others has helped make them important? I believe so. (Henry C. Rogers, Rogers' Rules for Success, uk. 44.)

Sijui kama wewe ni mmoja wa hao wanaobeza au wanaohimiza juhudi na mafanikio ya wenzao. Siku chache tu zilizopita, nilisoma kauli za Wema Sepetu, dada m-Tanzania maarufu katika maigizo ya filamu. Alielezea jinsi watu wanavyombeza, kumtukana, na kufanya kila juhudi ya kumkatisha tamaa, hadi amewahi kufikiria kuwa hakuna sababu ya kuendelea kuishi.

Ni ushuhuda ambao ulinigusa sana. Ni ukweli usiopingika kwamba wako wa-Tanzania wengi wa ovyo kama ilivyoelezwa hapa juu. Hata mimi wananiandama kwa kejeli na mabezo humo mitandaoni, lakini hawajitambulishi. Kwa mfano, nimekumbana na watu wanaokibeza kitabu changu cha Africans and Americans: Embracing Cultural Differences ambacho kinapendwa na kutumiwa sana, hasa hapa Marekani, na ni msingi mojawapo wa mialiko ya mara kwa mara ya kwenda kutoa mihadhara, kama inavyoonekana pichani hapo juu, katika Chuo cha South Central, Minnesota.

Lakini, utakuta mtu anajitokeza na kutoa kauli ya kubeza bila maelezo wala ushahidi, ili mradi amerusha maneno yanayoweza kukatisha tamaa. Wala hatoi ushauri muafaka, kama anaona mapungufu, ili kuisaidia jamii. Ukitaka mfano, soma ujumbe huu. Kuna wakati hao waropokaji niliamua kuwapa vidonge vyao, kama tunavyosema, kwa kuwaambia waandike vitabu vyao, tuone.

Kwa upande wangu, watu wa namna hiyo wanajisumbua bure. Wanapoteza muda ambao wangeutumia kujiendeleza kwa kusoma. Bora hata wangenitafuta niwape mawazo na uzoefu kama wanavyonitafuta wa-Marekani. Ninawaheshimu wa-Marekani kwa hilo. Ni wasikivu wanapoelezwa mambo wasioyafahamu, kama haya ninayowalezea kuhusu athari za tofauti za tamaduni katika dunia ya utandawazi wa leo. Ni watu wanaotaka mafanikio katika ulimwengu huu.

Hao watu aliowaongelea Wema Sepetu na ambao nami ninawaongelea, nawaonea huruma. Labda siku itafika watakapoanza kuwa na mtazamo mpya. Binafsi nina furaha maishani kwa kuwa ninazingatia malengo niliyojiwekea, na mafanikio ninayaona, hasa katika kuwagusa watu na kuwaneemesha. Nimeshasema kabla kuwa lengo langu kuu ni hilo, sio utajiri wa fedha.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...