Waliniletea ujumbe siku zilizopita, wakisema kuwa siku ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwangu wangependa kunipeleka mahali tukale chakula cha mchana. Siku zilivyopita, walikuwa wananikumbusha. Leo, nilipomaliza kufundisha, Larry alinifuata chuoni St. Olaf tukaenda kwenye hoteli ambapo tulipata chakula na kupiga michapo.
Namshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuishuhudia siku hii. Ni neema ambayo sistahili. Napaswa kutambua kwamba kila siku katika maisha yangu ni dhamana, niitumie kwa mambo mema. Nizingatie wajibu wa kuvitumia kikamilifu vipaji alivyonipa Mungu kwa manufaa ya wanadamu.
Wengi hawakupata bahati ya kufikia umri niliofikia, lakini wamefanya makubwa, yasiyo kifani. Kama ilivyo kawaida yangu, nawakumbuka hasa waandishi maarufu, kama William Shakespeare, Alexander Pushkin, Ernest Hemingway, na Shaaban Robert. Hawakuishi miaka mingi kama yangu. Kuwafikiria watu kama hao kunanifundisha unyenyekevu. Siwezi kujivunia chochote nilichoweza kufanya, bali ni kumshukuru Mungu na kuendelea kumtegemea.Inavyoonekana, kila ninaposherehekea kumbumbuku ya siku ya kuzaliwa kwangu, fikra zangu za msingi kuhusu maisha yangu zinajirudia. Ninajikuta nikifananisha mchango wangu ulimwenguni na ule wa watu maarufu, na kukiri kuwa, ingawa ninajitahidi, mchango wangu bado ni hafifu. Nimekuwa nikiandika hivyo katika blogu hii. Hii ni changamoto kwangu, daima na siku zijazo.



