Tuesday, May 12, 2015

Vitabu vya Shaaban Robert

Jina la Shaaban Robert ni maarufu miongoni mwa wa-Tanzania na wengine wa nchi zingine wanaokijua ki-Swahili. Lakini, tujiulize ni wa-Tanzania wepi ambao wamesoma angalau vitabu vichache vya Shaaban Robert. Ni wangapi wamesoma au wanasoma mashairi yake, tenzi zake, insha zake, barua zake, na riwaya zake?

Ni wangapi wamesoma vitabu vyake vingine, kama vile Wasifu wa Siti Binti Saad, Maisha Yangu na Baada ya Miaka Hamsini, na tafsiri yake ya mashairi ya Omar Khayyam? Kama hatuna majibu ya kuridhisha, tuache kujigamba, kujidanganya na kudanganyana kuwa tunamwenzi mwandishi wetu huyu maarufu.

Ingawa kulikuwa na kipindi cha uhaba, leo vitabu vya Shaaban Robert vinapatikana kirahisi Tanzania, baada ya kampuni ya uchapishaji ya Mkuki na Nyota kuanza kuvichapisha upya. Mwaka hadi mwaka, ninapokwenda Tanzania, nimekuwa nikijinunulia vitabu hivyo, kama hivi vinavyoonekana pichani, sambamba na vitabu vya waandishi wengine maarufu katika lugha ya ki-Swahili.

Imekuwa ni faraja kwangu kuvisoma, baada ya kuzinduka kutoka katika mazoea ya kusoma zaidi maandishi ya ki-Ingereza. Ninajiona kama vile nimeanza kujikomboa kimawazo. Lugha yako ni utambulisho wako, na kuifahamu na kuitumia vizuri ni ishara ya kuiheshimu lugha hiyo. Ni ishara ya kujiheshimu.

Pamoja na kununua na kusoma vitabu alivyoandika Shaaban Robert, ninajitahidi kupanua akili yangu kwa namna nyngine pia. Ninayo maandishi yanayochambua maandishi ya Shaaban Robert. Mfano ni vitabu vinavyoonekana hapa pichani, kimoja cha A.G. Gibbe, na kingine cha Clement Ndulute. Maandishi mengine yamo katika majarida na vitabu vingine ambavyo baadhi ninavyo pia.

Ninajitahidi, kwa uwezo wangu, kushiriki katika kuandika kuhusu kazi za Shaaban Robert. Nimechapisha insha juu ya Shaaban Robert katika Encyclopaedia of African Literature iliyohaririwa na Simon Gikandi. Katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii, kuna pia insha yangu iitwayo "Shaaban Robert: Mwalimu wa Jamii." Kadiri nitakavyokuwa naendelea kusoma maandishi yake, nategemea kuandika zaidi. Nina nafasi nzuri ya kufanya hivyo kwa kuwa ni mwalimu wa fasihi za kimataifa na nadharia ya fasihi.

Saturday, May 9, 2015

Neno Jingine Kuhusu Uandishi na Uchapishaji

Mimi ni mwandishi wa vitabu. Ninaandika vitabu vya tahakiki ya fasihi, juu ya masuala ya jamii, fasihi simulizi, na masuala ya athari za tofauti za tamaduni, hali halisi ya uandishi wa vitabu, mbinu za kujichapishia vitabu. Naandika kuhusu utangazaji na uuzaji wa vitabu, na kuhusu hali halisi ya usomaji wa vitabu Tanzania na ughaibuni.

Ninatoa ushauri kwa wengine kupitia blogu hii na katika kitabu changu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Yeyote anayetaka kujifunza kutoka kwangu anaweza kufanya hivyo, bila kipingamizi. Lakini namtegemea aanze kwa kusoma nilichoandika, mawasiano ya ziada yafuate baadaye.

Siwezi kuwasiliana na kila mtu na kuongelea hata yale ambayo tayari nimeshaandika. Nina kazi yangu na majukumu mengine kila siku. Nikisema niwasiliane na kila mtu hata kwa yale ambayo nimeshaandika, nitashindwa kufanya kazi zangu zinazoniwezesha kuishi, kulipia nyumba, matibabu, na mahitaji mengine.

Labda niache kazi niliyoajiriwa kufanya, nijiajiri kama mshauri. Ikiwa hivyo, kila anayetafuta ushauri kwangu atatakiwa alipie. Ndivyo wanavyofanya watoa ushauri. Nami ujuzi na uzoefu ninao, kama inavyodhihirika katika taarifa ninazoandika katika blogu hii ya hapakwetu na blogu ya ki-Ingereza.

Suali ambalo ninaulizwa tena na tena ni kuhusu mikakati ya kuchapisha miswada. Ni wazi kuwa watu bado wana fikra za jadi kuhusu uchapishaji. Nawashauri waondokane na fikra za kuwateemea wachapishaji. Badala yake, waingie katika ulimwengu wa kujichapishia vitabu.

Wafanyeje au waanzie wapi ndio aima ya masuala ninayoongelea katika blogu na katika kitabu cha CHANGAMOTO: Insha za Jamii. Kama mtu anataka mafanikio, ni lazima awekeze katika elimu inayohusiana na shughuli anayotaka kufanya. Kununua vitabu na kuvisoma ni uwekezaji, sawa na uwekezaji wa kununua trekta ya kilimo au nyavu za kuvulia samaki.

 Suala la kujichapishia vitabu ni tata, hasa kwa upande wa wanataaluma. Jadi iliyopo katika kuchapisha vitabu vya kitaaluma au makala za kitaaluma imekuwa ya kuzingatia umuhimu wa wanataaluma tofauti na mwandishi kufanya uhakiki na udhibiti wa andiko kabla ya kuchapishwa. Ninapangia kuandika zaidi kuhusu suala hilo.  

Friday, May 8, 2015

Vitabu vya Moyez Vassanji

Siku chache zilizopita niliandika taarifa kuhusu vitabu nilivyonunua hivi karibuni. Kati ya vitabu kilikuwepo kimoja cha Moyez Vassanji, The Gunny Sack. Wakati huo, nilikuwa navingojea vitabu vingine viwili vya Moyez Vassanji, ambavyo nilikuwa nimeshavilipia. Vimefika.

Kimoja ni Uhuru Street, mkusanyo wa hadithi za kubuniwa,ambazo zinatokea katika mtaa wa Uhuru, mjini Dar es Salaam. Nasikitika kuwa kitabu hiki sijakisoma ingawa nimetamani kukisoma kwa miaka mingi. Kutokana na taarifa, nilijua kuwa kwa yeyote anayeijua Dar es Salaam, hiki ni kitabu kinachogusa hisia. Nimeanza kukisoma na ninajionea mwenyewe ukweli huo.

Kitabu cha pili ambacho kimewasili ni The Book of Secrets, ambacho, kama nilivyosema, niliwahi kukifundisha katika semina ya walimu katika Chuo cha Colorado. Mtu akisoma kitabu hiki, naamini atapata hamu ya kusoma vitabu vingine vya Moyez Vassanji.

Kitabu cha tatu ambacho kimewasili ni The In-Between World of Vikram Lall. Sijaanza kukisoma, ila nimekuwa nikisoma habari zake.

Kitabu kingine nilichokitaja siku chache zilizopita ni Amriika, ambacho nilikinunua zamani kidogo, ila sijakisoma. Moyez Vassanji ameshaandika vitabu karibu kumi hadi sasa. Ambavyo sijavitaja ni The Assasin's Song, No New Land, The Magic of Saida, A Place Within, na  And Home Was Kariakoo. Orodha haiishii hapo, na kuvisoma vyote itakuwa kazi kubwa. Kwa vyo vyote, baadhi nitavitumia katika kozi yangu ya Post-colonial Literature.

Moyez Vassanji ni mwandishi maarufu, nasi wa-Tanzania tuna haki ya kusema ni mtu wetu, kwani mnali ya kukulia Tanzania, amekuwa akiipeperusha vizuri sana bendera ya nchi yetu katika ulimwengu wa fasihi. Ninaamini tunawajibika kuwa naye bega kwa bega kwa kusoma vitabu vyake.

Ninakiri kuwa si jambo la kuridhisha kwamba vitabu vingi vilivyovitaja hapo juu ambavyo vilichapishwa miaka iliyopita, sikuvisoma na bado sijavisoma. Hiyo ni dosari. Ninapaswa kumfahamu mwandishi kama Moyez Vassanji kama ninavyowafahamu waandishi ninaowasoma katika ki-Ingereza kama Wole Soyinka, Nadine Gordimer, Derek Walcott, J.M. Coetzee, Anita Desai, Athol Fugard, Ngugi wa Thiong'o, Chinua Achebe, Sembene Ousmane, Salman Rushdie, na kadhalika.

Panapo majaliwa, nitaandika katika blogu hii juu ya Abdulrazak Gurnah na Tololwa Mollel, ambao ni waandishi wengine maarufu wa ki-Tanzania huku ughaibuni wanaoandika kwa ki-Ingereza. Tuwe nao bega kwa bega. Ni aibu kwetu kwamba waandishi hao wanasifika nchi za ng'ambo lakini si nyumbani Tanzania.

Going Visual: Kitabu Kuhusu Mawasiliano Kwa Taswira

Leo napenda kukiongelea kitabu kiitwacho Going Visual: Using Images to Enhance Productivity, Decision-Making and Profits, kilichoandikwa na Alexis Gerard na Bob Goldstein. Nilikinunua kitabu hiki miaka michache iliyopita. Kama ilivyo kawaid yangu ninaponunua kitabu, sikiweki katika maktaba yangu bila kukipitia angalau juu juu, ili nijue kinahusu nini.

Hivi ndivyo nilivyofanya niliponunua Going Visual. Niliona ni kitabu kinachoelezea maendeleo katika utumiaji wa taswira katika mawasiliano, kitabu kinachoelezea matokeo ya utafiti na uzoefu na mikakati ya matumizi ya taswira katika biashara na ujasiriamali. Kitabu kinaelezea jinsi tekinolojia ya kuzalisha, kuhifadhi, kuandaa, na kusambaza taswira, kuanzia za digitali hadi video, zinavyowezesha ufanisi katika biashara na ujasiriamali katika ulimwengu wa leo.

Wakati nilipokinunua kitabu hiki, nilikipitia juu juu, nikaelewa haya niliyoelezea. Lakini leo nimekitoa maktabani ili nikisome ipasavyo. Mada yake inanivutia, na ukweli kwamba sina ufahamu wa masuala yaliyomo umenipa shauku ya kufahamu.

Suala la mawasiliano tunalishughulikia katika usomaji na ufundishaji wa fasihi, kwani fasihi hutumia lugha, ambayo ni chombo mahsusi cha mawasiliano. Nadharia za lugha na fasihi zinatueleza mengi kuhusu mawasiliano. Mvuto wa kitabu cha Going Visual kwangu, na duku duku inayonisukuma kukisoma, ni hiyo mikakati na mbinu za kutumia taswira ambazo waandishi wa kitabu wanasema zinawanufaisha wafanya biashara na wajisiriamali wa leo.

Ninajiuliza: hizi mbinu ni zipi? Na hiyo mikakati ni ipi? Kwa hivi, ninaona ni muhimu nikisome kitabu hiki nielimike, ingawa siwezi kujiita mfanyabiashara au mjasiriamali. Elimu haina mwenyewe, haina mipaka, wala haina mwisho.

Wednesday, May 6, 2015

Leo Nimepata Bendera ya Tanzania

Leo nimepata bendera ya Tanzania. Niliwahi kuandika katika blogu hii kuwa mara kwa mara ninashiriki matamasha hapa Marekani ambapo watu huja na bendera za nchi zao, nami nilijisikia vibaya kwa kutokuwa na bendera kubwa ya nchi yangu. Nilifanya uamuzi muafaka, nikaagiza, na leo nimeipata.

Mwaka jana, nilipoandika ujumbe wangu, nilikuwa napeleleza katika tovuti kadhaa zinazouza bendera. Lakini safari hii, kwa kubahatisha tu, nimeingia katika tovuti ya Amazon nikaona bendera ziko, tena kwa bei rahisi sana.




Nimejionea hapa Marekani jinsi wa-Kenya walivyo hodari kwa suala hilo, na hapa naleta picha niliyopiga katika tamasha la Afrifest, tarehe 2 Agosti, mwaka jana, mjini Brooklyn Park, Minnesota. Inamwonyesha m-Kenya akitamba na bendera ya nchi yake.

Jiulize mwenyewe, ungejisikiaje kuwepo mahali ambapo wenzako wanatamba na bendera za nchi zao, nawe huna. Kwa nini ukae mahali hivyo, kama vile huna nchi? Hisia hizi ni kubwa unapokuwa ughaibuni. Sikutaka kuendelea kudhalilika namna hiyo.



Picha nyingine, inayoonekana hapa kushoto, nilipiga tarehe 11 Aprili, 2015, mjini Rochester, Minnesota, kwenye tamasha la tamaduni za ulimwengu. Inaonyesha meza ya wa-Kenya na bendera yao.

Kuna matamasha yanayokuja ambayo nitashiriki, kama vile tamasha la Afrifest, tarehe 1 Agosti, 2015. Nitakapokuwa naandika taarifa za matamasha hayo na maonesho, wadau mtajionea wenyewe bendera ya Tanzania ikipepea kwenye eneo la meza ya vitabu vyangu.

Monday, May 4, 2015

Kuiheshimu Misahafu ya Dini Zote

Pichani hapa kushoto ninaonekana nimeshika nakala yangu ya Bhagavad Gita, msahafu wa dini ya Hindu. Ingawa mimi ni m-Kristu (m-Katoliki), ninaamini kwa dhati kuwa ni wajibu kuiheshimu misahafu ya dini zote.

Kwa mfano, ninayo Qur'an. Siku moja nilimwuliza kijana mmoja mu-Islam kuhusu heshima itakiwayo kwa Qur'an. Kuna baadhi ya mambo niliyajua, lakini kijana aliniambia jambo la ziada. Alisema kwamba pasiwekwe chchote juu ya Qur'an.

Basi, daima ninakumbuka na ninazingatia hilo. Ingawa ofisi yangu imefurika vitabu, na  mezani pangu panakuwa pamefurika vitabu, na Qur'an yangu iko hapa hapa mezani muda wote, siwezi kuweka kitabu, karatasi, au kitu chochote juu yake. Nafanya hivi kwa kufuata dhamiri yangu, si kwa kuogopa labda atafika mtu ofisini akute hali nyingine.

Ninaamini kuwa kama dini yoyote inajinadi kuwa ni dini ya amani, ni lazima idhihirishe jambo hilo kwa kuziheshimu dini zingine. Ni lazima iwaheshimu waumini wa dini zingine, na misahafu yao. Kufanya kinyume ni kuhatarisha amani. Amani inajumlisha pia amani ya akilini na moyoni.

Amani haijengwi kwa kuwadharau wengine. Haijengwi kwa kudharau imani za wengine. Inasikitisha kuona jinsi baadhi ya watu nchini Tanzania wanavyozibeza dini za wenzao, wanavyoibeza misahafu ya wenzao, katika malumbano ambayo hayajengi amani bali yanaweka misingi ya kuhujumu amani.

Wa-Kristu tunawajibika kufanya kila juhudi kufuata agizo la Yesu la kumpenda Mungu kwa uwezo wetu wote, akili yetu yote, roho yetu yote, na kwa moyo wetu wote. Tunawajibika pia kumpenda jirani kama tunavyojipenda wenyewe. Katika mafundisho yake, inadhihirika pia kuwa Yesu alituasa kuwapenda hata maadui zetu. Wa-Kristu tunakatazwa kulipiza kisasi.

Kwa kuwa fundisho la msingi la u-Kristu ni hilo, ambalo linathibitisha kuwa ni dini ya amani, kwa nini nisifanye juhudi ya kuwaelewa wanadamu, kuzielewa tamaduni zao, na kuzielewa dini zao? Mtu asishangae akinikuta ninasoma Bhagavad Gita, Qur'an, au msahafu mwingine, sambamba na Biblia yangu. 

Sunday, May 3, 2015

Vitabu Nilivyonunua Karibuni

Napenda kuendelea na jadi yangu ya kuvitaja vitabu nilivyoongeza katika maktaba yangu katika siku chache zilizopita.

Kitabu kimoja ni The Poetic Edda: Stories of the Norse Gods and Heroes, kilichotafsiriwa na Jackson Crowford. The Poetic Edda ni kitabu maarufu sana ambacho nimekisikia kwa miaka mingi. Ni mkusanyo wa hadithi na mashairi ya mapokeo juu ya miungu na mashujaa wa Iceland.

Nimeamua kujipatia nakala wakati huu ambapo nimekuwa nafundisha utungo maarufu wa Finland uitwao Kalevala. Kwa pembeni nimekuwa nayapitia pia mashairi ya mapokeo ya Finland yaliyokusanya na Elias Lonnrot katika kitabu kiitwacho Kanteletar. Nina hamu ya kuona kama The Poetic Edda inahusiana na hizo tungo zingine, kwa kuzingatia kuwa zote ni za Ulaya ya kaskazini.

Kitabu kingine nilichonunua ni The Village by the Sea, cha Anita Desai wa India. Nilipangia kukifundisha muhula huu katika kozi yangu ya Post-colonial Literature, lakini tumeishiwa muda. Nimeshafundisha riwaya kadhaa za Anita Desai. Ni mwandishi bora sana. Ndio maana nikaamua kukiweka kitabu chake cha The Village by the Sea katika orodha ya muhula huu.

Kitabu kingine nilichonunua ni Monkfish Moon. Ni mkusanyo wa hadithi fupi za Romesh Gunesekera wa Sri Lanka, ambaye riwaya yake ya Reef nimeifundisha. Gunesekera ni mwandishi hodari sana. Nilikijumlisha kitabu chake cha Monkfish Moon katika orodha yangu ya Post colonial Literature. Lakini, muda umeshindikana.

Kitabu kingine nilichonunua, yapata wiki moja iliyopita, ni See Now Then cha Jamaica Kincaid wa Antigua, Carribean. Niliwahi kuhudhuria mhadhara wake katika Chuo Kikuu cha Minnesota.

Kitabu kingine nilichonunua, ambacho nimekipata leo, ni The Gunny Sack, cha Moyez Vassanji. Moyez Vassanji alizaliwa Kenya lakini alikulia Dar es Salaam. Ni mwandishi maarufu ambaye anaishi Canada. Kati ya vitabu vyake vinavyovuma sana ni Uhuru Street na The Book of Secrets., ambacho niliwahi kukifundisha katika semina ya waalimu Chuo cha Colorado. Kinavutia sana kwa ustadi uliotumika katika kukiandika. Kitabu chake kingine, Amriika, nilikinunua miezi mingi iliyopita ila sijakisoma bado.

Tangazo la Maongezi Yangu Books on Central, Faribault

Kwa miaka mingi, nimeongea na hadhira mbali mbali hasa kuhusu tofauti za tamaduni. Matangazo huandaliwa na kusambazwaa kabla ya mikutano. Ka...